MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, Mariam Ditopile amekutana na Madereva Bodaboda na Bajaji wa Halmashauri ya Mji wa Kondoa ili kuwahamasisha kutoa elimu kwa wananchi juu ya kushiriki zoezi la Sensa na Makazi ifikapo Agosti 23 mwaka huu.


Akizungumza na Madereva hao, Ditopile amesema anatambua nguvu kubwa waliyonayo  katika jamii na kwamba anaamini kupitia wao wananchi wengi wanaweza kupata elimu ya sensa na kushiriki zoezi hilo.


" Niwashukuru kwa kuitikia kwa wingi wito wangu, nitoe wito kwenu kumuunga mkono Rais wetu Samia Suluhu Hassan na Serikali yetu katika kuhamasisha wananchi wetu kushiriki zoezi la Sensa ya Watu na Makazi ili isaidie Serikali kujua idadi yetu jambo ambalo litachochea pia maendeleo kwenye maeneo yetu.


Ili serikali iweze kupanga mipango endelevu kutenga bajeti kwa usahihi na ufasaha lazima ijue Halmashauri ya Mji Kondoa wako wangapi wanahitaji nini kwahiyo ni muhimu sana sisi sote kuweza kuhesabiwa''. Amesema Mbunge Ditopile.


Mbunge Ditopile pia ametoa wito kwa Madereva hao kuanzisha umoja wao pamoja na kuchagua viongozi ambao watakua wanatatua changamoto zao ambazo wamekua wakikutana nazo kama Madereva wa Bodaboda na Bajaji lakini pia kupitia Umoja huo amewaeleza kuwa itakua ni rahisi kwao kupata fursa mbalimbali.


" Niwaombe muanzishe Umoja wenu na mchague viongozi ambao watakua wanawasemea na kutatua changamoto zenu lakini pia watakaotumika kama daraja baina yenu na Serikali, mkiwa na umoja ni rahisi kupata fursa mbalimbali ikiwemo mikopo ambayo itawawezesha kujikwamua Kiuchumi," 


Najua changamoto ya Daraja letu la Kondoa, naiomba Serikali iliangalie daraja letu, lijengwe kubwa na la kisasa ambalo litawezesha vyombo vyote vya Usafiri kupishana sambamba na watembea kwa miguu, daraja lililopo ni la zamani haliendani na ukuaji wa Mji wetu wa Kondoa," Amesema Ditopile.


Katika mkutao huo pia Mbunge Ditopile aliwakabidhi Madereva hao viakisi 'reflector' zenye ujumbe wa kuhamasisha zoezi la Sensa na kuwataka kuzivaa ili kufikisha ujumbe kwa wananchi wanaowabeba.

Share To:

Post A Comment: