Na,Moses Mashalla,


Mkuu wa wilaya ya Arusha,Said Mtanda amewataka wazazi wote wilayani hapa kuhakikisha wanawapeleka watoto wao kwenye vituo vya afya na zahanati ifikapo Septemba Mosi mwaka huu ili wakapatiwe chanjo ya ugonjwa wa Polio .


Mtanda ametoa kauli hiyo leo wakati akizungumza na wajumbe mbalimbali wa kamati ya chanjo ya Polio jijini Arusha.


Akizungumza katika kikao hicho Mtanda alisema kuwa ni jukumu la kila mzazi kuhakikisha anampeleka mtoto wake aliye chini ya umri wa miaka mitano katika zahanati au kituo cha afya ifikapo tarehe hiyo ili aweze kupata chanjo hiyo ambayo inalenga kuzuia maambukizi ya ugonjwa wa Polio.


Mtanda alisema kwamba chanjo ya polio inatolewa kwa matone na sio sindano kwa watoto walio chini ya umri wa miaka mitano na kuwaondoa hofu wakazi wa Arusha kwamba haina madhara yoyote.


“Serikali haiwezi kuleta chanjo yenye madhara nawahimiza wazazi wote ifikapo Septemba mosi mpaka nne wahakikishe wanawapeleka watoto wao kwenye vituo vya afya na zahanati wakapate chanjo ya polio “alisema Mtanda 


Naye mwenyekiti wa kamati ya chanjo jijini Arusha,Florence Solomon alisema kuwa maandalizi mpaka sasa maandalizi ya zoezi la utoaji wa chanjo hiyo linaenda vizuri na kazi iliyobaki ni kupeleka elimu kwa wananchi.


Mwenyekiti huyo amesema kwamba baadhi ya wananchi bado wanafikiri ya kwamba chanjo itakayotolewa ni ile ya UVIKO-19 na kuvitaka vyombo vya habari kujikita kutoa elimu ya kutosha juu ya chanjo ya Polio.


“Tupeleke elimu kwa wananchi wengi kwa kuwa kuna baadhi ya watu wanadhani chanjo ya Polio ni ya UVIKO-19 waandishi wa habari mtusaidie kwa hili “alisema Solomon 


Mratibu wa chanjo hiyo jijini Arusha,Hashim Mtiti kwa sasa maandalizi yote ya utoaji wa chanjo hiyo yamekamilika na kazi iliyobaki ni kupeleka hamasa kwa jamii.


Mtiti alisema kwamba kuna ushirikishwaji mkubwa sana katika zoezi hilo la utoaji wa chanjo ya polio kupitia makundi mbalimbali na safari hii wanatarajia kuvuka lengo kwa asilimia 100 .

Mwisho









Share To:

JUSLINE

Post A Comment: