WAZIRI wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe, amewahakikishia wadau wa Sekta ya Kilimo kuwa kipaumbele cha Serikali ni kuimarisha Sekta ya Kilimo cha umwagiliaji ili kupunguza adha ya kutegemea kilimo cha mvua.

Ameyazungumza hayo Mkoani Morogoro wakati anafungua mkutano wa wadau wa kilimo cha Umwagiliaji ulioandaliwa na Benki ya Dunia kwa kushirikiana na Tume ya Taifa ya Umwagiliaji  Juni 15, 2022.

Waziri Bashe amesema katika bajeti ya fedha ya mwaka 2022/23, Serikali imetenga shilingi Bilioni 364 katika Sekta ya Kilimo cha Umwagiliaji, pia kuna ongezeko la Bilioni 50 ambazo zimetengwa ili kuleta mafanikio chanya katika Sekta hiyo.

Aidha Serikali kupitia Wizara ya Kilimo itatangaza hekta elfu 10 kwa ajili ya Kilimo cha Umwagiliaji.

Waziri Bashe ameongeza kuwa kutokana na Rais Wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kuwa na utashi wa kisiasa katika Sekta ya Kilimo, Serikali imedhamiria kuwekeza katika kilimo cha Umwagiliaji.

Serikali imetenga hekta Elfu 20 kwa ajili ya mashamba ya Vijana ambayo yatatengenezewa miundombinu ya Umwagiliaji ili kupunguza tatizo la ajira nchini.

Waziri Bashe alimalizia kwa kuwa Serikali imefungua milango kwa wadau wote wa Sekta ya Kilimo kupeleka mawazo yatakayochochea matokeo chanya na kuinua Sekta ya Kilimo nchini.
Share To:

JUSLINE

Post A Comment: