Serikali ya awamu ya Sita Chini ya Rais Samia Suluhu Hassan  imeweka mpango wa kununua ndege mpya na kuifanyia matengenezo nyingine moja kwa lengo la kukabiliana na wadudu waharibifu wa mazao ya wakulima.

Hayo yamesemwa leo tarehe 28 Mei, 2022 na Naibu Waziri wa Kilimo Mh Anthony Mavunde alipotembelea shamba la Soya na kukabidhi rasmi zana za kilimo za Chama cha Ushirika cha Msingi cha Wakulima Wanawake Dodoma Mjini (CHAUWAWADO) katika kijiji cha Narakauo, Kata ya Loiborsiret, Wilayani Simanjiro, Mkoani Manyara.

Zana za kilimo ambazo CHAUWAWADO wamezizindua leo zimetokana na mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB). Zana hizo ni Trekta, jembe la kusawazishia, mashine ya kupanga na jembe la kulimia.

"Nimeisikia changamoto kubwa mliyoisema juu ya uharibifu wa mazao kutokana na wadudu wasumbufu,tumejipanga kuimarisha kilimo anga kwa kununua ndege mpya ya kunyunyiza na kuifanyia matengenezo moja iliyopo ili tuwasaidie wakulima wa nchi hii kutopata hasara ya uharibifu wa mazao unaofanywa na wadudu waharibifu.

Tunamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa utashi wake wa kuikuza sekta ya kilimo,hivi sasa bajeti ya kilimo imeongezeka kutoka Bilioni 294 mpaka Bilioni 751,haya ni mapinduzi makubwa sana kwenye sekta ya kilimo.

Nimefurahishwa sana na jinsi ninyi akina mama, mmetoka Dodoma na kuja kufanya kilimo hapa kijiji cha Narakauo, mmeonesha udhubutu mkubwa. Nawapongeza sana kwani mmeonesha kwa vitendo namna mnavyounga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania" Alisema Mavunde.


Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa CHAUWAWADO AMCOS, Bi. Winifrida Kario alieleza kuwa wameweza kulima ekari 160 za soya, ambazo wameingia mkataba wa masoko na kampuni ya Dar Lyon na kwamba, wana malengo ya kuendelea kuongeza eneo la kulima mwaka hadi mwaka. Aidha, alibainisha moja ya changamoto kubwa ni chama Chao kukosa ardhi, hali inayowafanya kukodi eneo la kuendesha shughuli zao za kilimo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Dkt. Suleiman Serera amemuhakikishia Naibu Waziri Mavunde kuwa atahakikisha CHAUWAWADO wanapata ardhi, na kuahidi kuendelea kuwasaidia ili waendelee kuzalisha kwa tija na hatimaye kukuza uchumi wa Kijiji cha Narakauo na wilaya ya Simanjiro kwa ujumla.










Share To:

Post A Comment: