Mheshimiwa Spika,
kufuatia taarifa iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini iliyochambua bajeti ya Wizara ya Madini, naomba kutoa hoja kwamba, Bunge lako Tukufu sasa likubali kupokea, kujadili na kupitisha Taarifa ya Utekelezaji wa Majukumu ya Wizara ya Madini kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Kawaida na Maendeleo ya Wizara ya Madini na Taasisi zake kwa Mwaka 2022/2023.


 Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee sana ninamshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, kwa kunijalia afya njema na kunipa nafasi ya upendeleo ya kusimama kwa mara nyingine tena mbele ya Bunge lako Tukufu nikiwa Waziri wa Madini kuwasilisha Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa Mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa naomba nitumie fursa hii kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kuniamini kuendelea kusimamia Sekta ya Madini. Namhakikishia kuwa nafasi aliyonipa nitaendelea kuitumikia kwa uaminifu na kwa uwezo alionijalia Mwenyezi Mungu ili kufikia matarajio ya Watanzania ya kuona Sekta ya Madini ikiboresha maisha yao na kuongeza mchango wake kwenye Pato la Taifa. 

Mheshimiwa Spika, chini ya uongozi makini wa Rais wetu tumeshuhudia uthubutu, ujasiri, uchapakazi na ubunifu wake mkubwa ambao umekuwa chachu ya mafanikio makubwa ya kijamii na kiuchumi kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali kama ujenzi wa vituo vya afya na madarasa, uendelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo ujenzi wa reli mpya ya standard gauge na mradi wa bwawa la kuzalisha umeme la Julius Nyerere (JNHP). 

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru tena Mheshimiwa Rais, kwa hatua madhubuti anazoendelea kuchukua katika kuzilinda rasilimali madini na kuvutia uwekezaji katika shughuli za uchimbaji madini ambapo baada ya kipindi kirefu, 3 Serikali imetoa leseni mbili (2) kwa kampuni za uchimbaji mkubwa na kuingia makubaliano na kampuni nne (4) kwa lengo la kuongeza ushiriki wake katika shughuli za madini. Kupitia utendaji wake uliotukuka katika kipindi kifupi ambacho yuko madarakani, Watanzania wanaimani kubwa kuwa Rais wetu mpendwa ataendelea kufanya mengi mema na mazuri kwa taifa letu.

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru kwa dhati Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, kwa miongozo yake mbalimbali yenye lengo la kuhakikisha kuwa rasilimali madini zinawanufaisha Watanzania na Taifa kwa ujumla. Vilevile, napenda kumshukuru Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wake makini na maelekezo anayoyatoa ili kufanikisha utendaji kazi Serikalini, ikiwemo Wizara ya Madini. Viongozi hawa wamekuwa tayari kutusikiliza na kutupa miongozo na maelekezo mbalimbali na hivyo busara zao zimekuwa ni msaada mkubwa katika kufanya maamuzi. 

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kukupongeza wewe binafsi kwa kuaminiwa na 4 kuchaguliwa kwa kishindo kuliongoza Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia, ninatumia fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mussa Azan Zungu (Mb.) kwa kuchaguliwa kwa kishindo kuwa Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ushindi huo unaashiria imani kubwa tuliyonayo waheshimiwa wabunge kwenu. Ni imani yetu kuwa mtaendelea kuliongoza Bunge kwa umahiri na busara katika kufanya maamuzi kwa maslahi mapana ya Taifa letu. 

Mheshimiwa Spika, naomba niwapongeze Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula (Mb.), Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mheshimiwa Seif Khamis Gulamali (Mb.), Makamu Mwenyekiti wa Kamati pamoja na wajumbe wa Kamati hiyo kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutoa ushauri na maelekezo mbalimbali ambayo yanasaidia kuongeza ufanisi wa utendaji kazi wa Wizara. Naahidi kuendelea kuwapa ushirikiano wa dhati katika kuhakikisha kuwa Sekta ya Madini inaendelea kuwanufaisha watanzania. 

Mheshimiwa Spika, ninapenda kutoa shukrani na pongezi kwa Bunge lako Tukufu kwa kazi nzuri ambazo limekuwa likifanya katika kuisimamia na kuishauri Serikali, ikiwemo Wizara ya 5 Madini. Kupitia kwako, naliomba Bunge liendelee kutupatia ushirikiano ili kuiendeleza Sekta hii muhimu katika kujenga uchumi imara na maendeleo endelevu ya Taifa letu. Aidha, napenda kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri wote kwa kuaminiwa na kuteuliwa kuongoza Wizara mbalimbali. Kadhalika, niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri wote kwa ushirikiano wanaonipatia katika kutekeleza majukumu ya kusimamia Sekta ya Madini. 

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa, nitumie fursa hii kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Bukombe kwa kuendelea kunivumilia na kunipa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yangu kama Mbunge wao. Najua kuna wakati wananikosa jimboni kama Mbunge wao kutokana na majukumu ya kitaifa kama Waziri wa Madini, lakini kwa wema wao wanaendelea kunivumilia na kunipa ushirikiano mkubwa. Nawaahidi kuendelea kuwa mtumishi wao mwaminifu katika kutekeleza shughuli za maendeleo ya Jimbo letu kwa ufanisi. 

Mheshimiwa Spika, napenda niwapongeze Dkt. Steven Lemomo Kiruswa (Mb.), Naibu Waziri, Bw. Adolf Hyasinth Ndunguru, Katibu Mkuu, Bw. Msafiri Lameck Mbibo, Naibu Katibu Mkuu na Dkt. 6 Abdulrahman Shabani Mwanga, Kamishna wa Madini, kwa kuaminiwa na kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kuisimamia Sekta ya Madini katika nyadhifa zao. Aidha, nawashukuru viongozi wenzangu, Wenyeviti wa Bodi, Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Madini pamoja na wafanyakazi wote kwa ushirikiano na utendaji kazi mzuri katika kutekeleza majukumu ya Wizara. 

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kumshukuru mke wangu kipenzi Benadetha Clement Mathayo kwa maombi na upendo wake wa dhati kwangu na watoto wetu. Amekuwa mvumilivu kipindi chote ninapokuwa natekeleza majukumu ya ubunge na uwaziri na kukubali kubeba baadhi ya majukumu yangu ya kifamilia. Aidha, nawashukuru watoto wangu pamoja na familia yangu kwa ujumla kwa upendo, uvumilivu, ushirikiano na maombi yao wakati wote ninapotekeleza majukumu yangu. Namuomba Mwenyezi Mungu aendelee kuwabariki na kuwalinda.

Mheshimiwa Spika, kwa masikitiko makubwa niungane na wenzangu kutoa pole kwa wananchi wa Majimbo ya Ushetu, Ngorongoro na Konde kwa kuondokewa na waliokuwa Wabunge wao Waheshimiwa Elias John Kwandikwa, William Ole 7 Nasha na Khatib Said Haji mtawalia. Aidha, nitoe pole kwako kufuatia kifo cha Mheshimiwa Irene Alex Ndyamkama, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa (CCM) kilichotokea tarehe 24 Aprili, 2022. Vilevile, natoa pole za dhati kwa wananchi kwa ujumla wao ambao walipoteza ndugu na mali zao kutokana na ajali, maafa na maradhi yaliyotokea sehemu mbalimbali hapa nchini. Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu wote mahali pema peponi. Amina. 

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa shukrani na pole naomba sasa nijielekeze katika maeneo mahsusi ya hotuba hii ambayo ni: Mwenendo wa biashara ya madini duniani; Mapitio ya Utekelezaji wa Mpango na Bajeti kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022; na Mpango na Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2022/2023. B. MWENENDO WA BIASHARA YA MADINI DUNIANI 

Mheshimiwa Spika, uchumi wa madini nchini kwa kiasi kikubwa unatokana na madini ya dhahabu, ambayo huchangia takriban asilimia 80 ya mapato yatokanayo na rasilimali madini. Wachambuzi wa masuala ya uchumi duniani walitarajia bei ya dhahabu kuendelea kuwa tulivu kwa mwaka 2022. Hata hivyo, bei ya madini ya dhahabu kwa wakia imepanda kutoka wastani wa 8 dola za Marekani 1,412.98 Julai 2019 hadi kufikia 1,947.83 Machi, 2022 (Kielelezo Na. 1). Kuongezeka kwa bei ya dhahabu kunatokana na sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na uwepo wa UVIKO-19. Kielelezo Na1: Mwenendo wa bei ya dhahabu Julai 2019 hadi Machi 2022 Chanzo: London Bullion Metal Association – LBMA 9 

Mheshimiwa Spika, changamoto ya vita kati ya Urusi na Ukraine inaweza kusababisha mahitaji makubwa ya madini ya dhahabu. Hii ni kwa sababu watu na taasisi duniani hupendelea kuhifadhi thamani ya fedha zao katika madini ya dhahabu kwa kuwa ni amana iliyo salama zaidi hasa wakati wa mitikisiko ya kiuchumi. Kwa upande mwingine, ukuaji wa teknolojia umesababisha ongezeko la mahitaji ya madini ya palladium, nickel, aluminium, cobalt na madini ya kinywe (graphite). Hivyo, bei ya madini hayo inatarajiwa kupanda na kuongeza fursa za uwekezaji. 

Mheshimiwa Spika, mwaka 2021 bei ya madini ya almasi katika soko la dunia iliongezeka na kufikia wastani wa dola za Marekani 241 kwa karati ikilinganishwa na wastani wa dola za Marekani 150 kwa karati mwaka 2020. Hadi Februari 2022, bei ya almasi iliendelea kuongezeka na kufikia wastani wa dola za Marekani 369 kwa karati. Ongezeko hilo limetokana na kupungua kwa mlipuko wa UVIKO-19 na uhitaji mkubwa wa bidhaa za usonara zinazotumia almasi (diamond jewellery) uliojitokeza katika kipindi cha sikukuu za krismasi na mwaka mpya. Hata hivyo, kuna viashiria vya bei ya madini ya almasi kwa mwaka 2022 kubadilika kwa kupanda 10 au kushuka kutokana na nchi ya Urusi ambayo ni mzalishaji mkubwa wa almasi duniani kuwa katika vita na Ukraine. 

Mheshimiwa Spika, ili kunufaika na ongezeko la bei za madini, Wizara inakusudia kuchukua hatua mbalimbali, ikiwemo kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji na kuangalia uwezekano wa kupunguzwa kwa baadhi ya kodi na tozo kwa wachimbaji ili kuwaongezea wigo wa faida na kuchochea uzalishaji zaidi. Aidha, Wizara inaendelea kuhimiza uwekezaji katika madini ya kimkakati ikiwemo palladium, nickel, aluminium, cobalt na kinywe (graphite) ili kunufaika na ongezeko la mahitaji ya madini hayo duniani. Vilevile, Wizara inaendelea kuhimiza uongezaji thamani madini nchini ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa bidhaa zinazotokana na madini. C. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI KWA MWAKA WA FEDHA 2021/2022 I. Mapato 

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2021/2022, Wizara ya Madini ilipangiwa kukusanya jumla ya shilingi bilioni 696.4 kutoka katika vyanzo 11 mbalimbali. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 650.0, sawa na asilimia 93.3 zilipangwa kukusanywa na kuwasilishwa Hazina na shilingi bilioni 46.4, sawa na asilimia 6.67 zilipangwa kukusanywa na kutumiwa na taasisi zilizo chini ya Wizara. 

 I. hadi kufikia Machi, 2022, Wizara ya Madini imekusanya jumla ya shilingi bilioni 484.6, sawa na asilimia 70 ya lengo la mwaka. Kati ya fedha hizo shilingi bilioni 461.6 zilipelekwa Hazina na shilingi bilioni 23.0 zimekusanywa na taasisi zilizo chini ya Wizara kwa ajili ya matumizi ya taasisi husika. 

II. Matumizi 21. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2021/2022 Wizara ilitengewa bajeti ya shilingi bilioni 66.8 kwa ajili ya matumizi ya Wizara na taasisi zake. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 15.0 zilitengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo na shilingi bilioni 51.8 kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Kati ya fedha za matumizi ya kawaida, shilingi bilioni18.5 ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi na shilingi bilioni 33.3 , kwa ajili ya matumizi mengineyo. 

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Machi, 2022, Wizara imepokea jumla ya shilingi bilioni 39.0 12 kutoka Wizara ya Fedha na Mipango. Kati ya fedha hizo, shilingi bilioni1.5 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo na shilingi bilioni 37.5 kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Kati ya fedha za matumizi ya kawaida zilizopokelewa, shilingi bilioni 13.7zimetumika kulipa mishahara ya watumishi na shilingi bilioni 23.8 ni matumizi mengineyo. III. Utekelezaji wa Vipaumbele vya Wizara vya Mwaka wa Fedha 2021/2022 

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2021/2022, Wizara ilipanga kutekeleza vipaumbele vifuatavyo: kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli na kuongeza mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa; kuwaendeleza wachimbaji wadogo na kuwawezesha wananchi kushiriki katika uchumi wa madini; kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini; kuhamasisha biashara na uwekezaji katika Sekta ya Madini; kusimamia mfumo wa ukaguzi wa shughuli za migodi; kuzijengea uwezo taasisi zilizo chini ya Wizara ili ziweze kutekeleza majukumu kwa ufanisi; na kuendeleza rasilimaliwatu na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi. 

Mheshimiwa Spika, katika kuongeza maduhuli ya Serikali na kuongeza mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa, Wizara imeimarisha usimamizi na 13 ukaguzi kwenye maeneo ya uchimbaji, mipaka ya nchi pamoja na kuanzisha na kuimarisha masoko na vituo vya uuzaji wa madini. Tangu kuanzishwa kwake hadi kufikia Machi, 2022 jumla ya masoko 42 na vituo vya ununuzi wa madini 75 vimeanzishwa. Uanzishaji na uimarishaji huo umechangia kwa kiasi kikubwa kwenye ukusanyaji wa maduhuli. 

Mheshimiwa Spika, hatua nyingine za kuimarisha ukusanyaji maduhuli zilizochukuliwa ni pamoja na kuimarisha udhibiti wa biashara haramu na utoroshaji wa madini. Kazi hii hufanywa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Mamlaka ya Mapato Tanzania, Ofisi ya Usalama wa Taifa, Jeshi la Polisi, Idara ya Uhamiaji, Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya pamoja na raia wema. Katika kipindi cha Julai 2021 hadi Machi, 2022, madini ya aina mbalimbali yakiwemo dhahabu, vito, mchanga na madini ya viwandani yenye jumla ya thamani ya shilingi milioni 501.2 yalikamatwa katika matukio ya utoroshaji na biashara haramu ya madini katika mikoa ya Mbeya, Morogoro, Manyara, Dodoma, Lindi, Geita, Kilimanjaro, Dar es Salaam na Mwanza. 

Mheshimiwa Spika, kutokana na juhudi hizo kumekuwa na ongezeko la ukusanyaji wa maduhuli 14 ambapo katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 shilingi bilioni 461.6 zimekusanywa na kuwasilishwa Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ikilinganishwa na shilingi bilioni 445.2 zillizokusanywa katika kipindi kama hicho mwaka 2020/2021, sawa na ongezeko la asilimia 4. 

 Mheshimiwa Spika, mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa umeendelea kuimarika. Katika kipindi cha Januari hadi Septemba, 2021 mchango wa sekta uliongezeka hadi kufikia wastani wa asilimia 7.3 kutoka wastani wa asilimia 6.5 katika kipindi kama hicho mwaka 2020. Aidha, katika robo mwaka ya Julai hadi Septemba 2021 mchango wa sekta uliongezeka hadi kufikia asilimia 7.9 ikilinganishwa na mchango wa asilimia 7.3 kwa kipindi kama hicho mwaka 2020. Mwenendo huu wa mchango unatoa mwelekeo chanya kuwa Sekta ya Madini itaweza kuchangia hadi asilimia 10 kwenye Pato la Taifa ifikapo mwaka 2025 kama ilivyotarajiwa kwenye Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na Mpango wa Taifa wa Maendeleo 2021/22-2025/26. 

Mheshimiwa Spika, mchango wa Sekta ya Madini katika kuliingizia Taifa fedha za kigeni umekuwa ukiimarika. Mwaka 2021, sekta hii ilichangia asilimia 45.9 ya thamani ya bidhaa zote 15 zilizouzwa nje ya nchi na kuliingizia Taifa dola za Marekani milioni 3,103.20. Kwa kipindi cha takribani miaka mitano (5) iliyopita Sekta ya Madini imeendelea kuongoza katika kuliingizia taifa fedha za kigeni. 

 Mheshimiwa Spika, pamoja na mapato yaliyotokana na maduhuli na fedha za kigeni kutokana na mauzo ya madini nje ya nchi, Sekta ya Madini pia iliiwezesha Serikali kukusanya shilingi trilioni 1.58 kutoka vyanzo mbalimbali vya kodi mwaka 2021 ikilinganishwa na shilingi trilioni 1.34 mwaka 2020. Ongezeko hilo ni sawa na asilimia 17.9. 

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhamasisha wawekezaji kuwekeza katika Sekta ya Madini ili kuongeza mchango wa sekta katika Pato la Taifa. Katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022, Wizara kupitia Tume ya Madini imetoa leseni mbili (2) za uchimbaji mkubwa wa madini ya dhahabu kwa kampuni ya Sotta Mining Corporation Limited inayomilikiwa na Nyanzaga Mining Company Limited na Serikali na leseni ya madini ya nikeli kwa kampuni ya Tembo Nickel Corporation Limited inayomilikiwa kwa ubia kati ya Kabanga Nickel Limited na Serikali. Serikali inamiliki hisa asilimia 16 16 zisizoshuka thamani (non-dilutable) katika kila kampuni. 

Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha mazungumzo na kampuni ya uchimbaji wa madini ya almasi ya Williamson Diamond Limited ambapo hisa za Serikali zimeongezeka kutoka asilimia 25 hadi asilimia 37. Aidha, Serikali imesaini mikataba na kampuni za uchimbaji wa madini ya graphite kwa kampuni ya Mahenge Resources Limited (Black Rock Mining Ltd) na madini ya heavy mineral sands Kampuni ya Jacana Resources Limited (Strandline Resources Ltd) na kuunda Kampuni za ubia za Faru Graphite Corporation na Nyati Mineral Sands Ltd mtawalia. Serikali ni mbia katika kila kampuni kwa kumiliki hisa asilimia 16 zisizoshuka thamani. Picha Na. 1: Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akishuhudia utiaji saini wa miradi ya uwekezaji ya uchimbaji wa madini tarehe 13 Desemba 2021 17 

Mheshimiwa Spika, thamani ya uwekezaji katika miradi hii unatarajiwa kuwa na thamani ya kiasi cha takriban dola za Marekani milioni 1,672.57. Aidha, uwekezaji huu ni mkubwa kuwahi kutokea katika kipindi cha takriban miongo miwili iliyopita. Vilevile, uwekezaji huu utaongeza ajira na manufaa yatokanayo na uwajibikaji wa kampuni za madini kwa jamii (CSR) na ushiriki wa watanzania katika uuzaji wa bidhaa na utoaji huduma katika shughuli za madini (Local Content). 

Mheshimiwa Spika, katika kuwaendeleza wachimbaji wadogo na kuwawezesha wananchi kushiriki katika uchumi wa madini, Wizara imeendelea kuzihamasisha taasisi za fedha na benki nchini zikiwemo NMB, NBC, CRDB na KCB kutoa mikopo. Hadi sasa baadhi ya benki hizo zimeridhia na kuanza kutoa mikopo ambapo jumla ya shilingi bilioni 36 zimekopeshwa kwa wachimbaji wadogo. Aidha, Wizara inaendelea na jitihada za kuzihamasisha taasisi hizo pia kuona uwezekano wa kuwakopesha vifaa wachimbaji hao. 

 Mheshimiwa Spika, hatua nyingine za uendelezaji wachimbaji wadogo zilizochukuliwa ni pamoja na: kuwapa elimu na kuwagawia nakala zipatazo 1,000 za Mwongozo wa Wachimbaji Wadogo; 18 kutoa mafunzo na huduma mbalimbali kwa wachimbaji wadogo wapatao 1,144 waliotembelea vituo vya mfano vya Katente, Lwamgasa na Itumbi; na vikundi vitano (5) vya wachimbaji wadogo kutoka Singida, Kilindi na Morogoro vimewezeshwa kujua jiolojia ya maeneo wanayomiliki. Aidha, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limekamilisha ujenzi wa miundombinu ya kuhifadhia vilipuzi na kemikali katika kituo cha Lwamgasa. 

Mheshimiwa Spika, STAMICO na Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) walitoa mafunzo mbalimbali kwa wachimbaji wadogo wapatao 945, wakiwemo wenye usikivu hafifu. Mafunzo hayo yalihusisha, uchimbaji salama, biashara ya madini na namna bora ya uchukuaji sampuli na yaliendeshwa katika maeneo ya Nh’oli (Dodoma), Mirerani, Chunya, Simiyu, Geita na Mwanza. Aidha, GST ilifanya utafiti maalumu wa jiolojia, jiofizikia na jiokemia katika maeneo ya wachimbaji wadogo wilayani Biharamulo ambapo matokeo yalibaini uwepo wa madini ya kaolini na dhahabu. 19 Picha 2: GST ikitoa mafunzo ya nadharia na vitendo kwa wachimbaji wadogo wa madini juu ya namna bora ya uchukuaji wa sampuli za uchunguzi na uchenjuaji - Geita 

Mheshimiwa Spika, STAMICO imeendelea kusimamia na kuimarisha vituo vya mfano na kutoa huduma mbalimbali kwa wachimbaji wadogo. Kuanzia Julai, 2021 hadi Machi, 2022 jumla ya tani 4,235.80 za mbale za dhahabu zimechenjuliwa katika vituo vya Lwamgasa, Katente na Itumbi, ambapo jumla ya wakia 3,692.77 za dhahabu zilizalishwa zikiwa na thamani ya shilingi 12,321,425,618.65 na kulipa serikalini tozo za shilingi 969,607,414.32. 

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kuwa shughuli za uchimbaji mdogo zinaendelea kufanyika kwa ufanisi, Serikali imeendelea kuwarasimisha wachimbaji wadogo. Hadi kufikia Machi 2022, 20 Wizara kupitia Tume ya Madini imetoa leseni 5,937 za uchimbaji mdogo wa madini, sawa na asilimia 72.65 ya leseni zote zilitolewa ikilinganishwa na leseni 3,540 zilizotolewa katika kipindi kama hicho mwaka 2021. Aidha, kufuatia kurasimishwa na kutambuliwa kwa wachimbaji wadogo, mchango wao umeendelea kuongezeka kutoka asilimia 4 kabla ya marekebisho ya Sheria ya Madini, Sura 123 hadi asilimia 30 kwa sasa. 

Mheshimiwa Spika, katika kuhamasisha na kuhakikisha shughuli za uongezaji thamani madini nchini zinaimarika, Serikali imeendelea kukiimarisha Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) kwa kuongeza fedha katika Mwaka wa fedha 2022/23 kwa ajili ya kuboresha miundombinu na kununua vifaa vya kujifunzia. Kituo hicho kinatoa mafunzo ya uongezaji thamani madini ikiwemo utambuzi, ukataji, uchongaji, ung’arishaji madini ya vito na utengenezaji wa bidhaa za usonara katika ngazi ya Astashada na Stashahada. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa vijana wengi wanapata ujuzi katika nyanja hizo na kuwaongezea fursa za kupata ajira au kujiajiri. 

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia STAMICO imejenga na kusimika miundombinu na mtambo wa 21 kuzalisha makaa ya mawe kwa matumizi ya nyumbani (coal briquettes) katika eneo la TIRDO - Dar es Salaam. Uzalishaji wa majaribio ulifanyika kwa ufanisi. Aidha, Shirika limeagiza mitambo miwili (2) yenye uwezo wa kuzalisha tani 20 za coal briquettes kwa saa ili kuongeza uzalishaji. Mradi huo utawanufaisha watanzania kwa kutoa ajira zaidi ya 200 na kupunguza ukataji miti kwa ajili ya mkaa hivyo kuchangia kutunza mazingira. Picha Na. 3 inaonesha makaa ya mawe kwa ajili ya matumizi ya nyumbani (Rafiki Briquettes). Picha Na. 3: Makaa ya mawe kwa ajili ya matumizi ya nyumbani (Coal briquettes) 

Mheshimiwa Spika, viwanda mbalimbali nchini vimeendelea kutumia madini ya viwandani kama malighafi kwa ajili ya kuzalisha bidhaa mbalimbali. Kuanzia julai 2021 hadi Machi 2022 22 kiasi cha madini ya viwandani kilichozalishwa na kutumiwa na viwanda vya ndani kilikuwa tani milioni 7.6. Uzalishaji na utumiaji wa madini hayo ni muhimu katika kukuza na kuendeleza viwanda vya ndani. 

 Mheshimiwa Spika, Wizara iliandaa na kushiriki maonesho, makongamano na mikutano katika majukwaa mbalimbali. Tarehe 21 hadi 23 Februari 2022, Wizara iliandaa na kushiriki Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Uwekezaji katika Sekta ya Madini uliofanyika Dar es Salaam; Septemba, 2021 Wizara ilishiriki katika Maonesho ya Teknolojia ya Madini yaliyofanyika mkoani Geita; maonesho kuelekea sherehe za miaka 60 ya Uhuru yaliyofanyika Zanzibar tarehe 03 hadi 09 Desemba, 2021; maonesho ya 45 ya Kimataifa ya biashara ya Sabasaba, 2021; na tarehe 31 Agosti, hadi 2 Septemba, 2021 Wizara ilishiriki warsha kuhusu rasilimali madini katika Nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) iliyofanyika Khartoum, Sudan. 23 Picha Na. 4: Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akiwa kwenye banda la maonesho la Wizara ya Madini katika Maonesho ya Teknolojia na Uwekezaji katika Sekta ya Madini Mkoani Geita 

Mheshimiwa Spika, pia Wizara ilishiriki katika jukwaa la uwekezaji kati ya Tanzania na Uingereza lililofanyika Dar es Salaam Novemba, 2021; maonesho ya Dunia ya Expo 2020 yaliyofanyika Dubai Novemba, 2021; jukwaa la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Italia lililofanyika Roma nchini Italia Desemba, 2021; na kongamano la madini ya teknolojia nchini Saudi Arabia lililofanyika tarehe 12 hadi 13 Januari, 2022. Ushiriki huo umekuwa na mafanikio ikiwa ni pamoja 24 na kusainiwa kwa mkataba wa ushirikiano katika utafiti na uendelezaji wa leseni za madini kati ya STAMICO na Kampuni ya ACME Consultancy Engineers Pte. Ltd wenye thamani ya takriban dola za Marekani milioni 300. Picha Na. 5: Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko akishuhudia utiaji saini wa makubaliano kati ya STAMICO na kampuni ya ACME Consultant 

Mheshimiwa Spika, biashara ya madini nchini imeendelea kuimarika ambapo katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi 2022 jumla ya kilogramu 39,682.94 za dhahabu, kilogramu 7,102.96 za fedha, karati 155,117.10 za almasi, kilogramu 15,377.44 za Tanzanite ghafi, kilogramu 130,582.28 za Tanzanite za ubora wa chini (beads), karati 81,305.42 za tanzanite iliyokatwa na kusanifiwa, 25 tani 19,355.13 za madini ya shaba na tani 322.49 za madini ya bati zilizalishwa. 

Mheshimiwa Spika, vilevile, kilogramu 6,835,746.73 na karati 12,863.29 za madini mengine ya vito ghafi na vito vilivyokatwa na kusanifiwa mtawalia, tani 18,462,591.96 za madini ya ujenzi, tani 956,688.08 za makaa ya mawe, tani 7,843,634.41 za madini mengine ya viwandani, na tani 51,132.33 za madini mengine ya metali zilizalishwa na kuuzwa. Katika kipindi hicho shilingi 429,191,348,141.87 zilikusanywa kama malipo ya mrabaha na ada ya ukaguzi kutoka kwenye madini hayo yenye thamani ya shilingi 6,439,691,493,817.11. makusanyo hao ni ongezeko la asilimia 2.5 ikilinganishwa na shilingi 418,727,438,816.59 zilizokusanywa katika kipindi kama hicho kwa mwaka 2020/2021. 

 Mheshimiwa Spika, shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa madini huambatana na athari mbalimbali za afya na mazingira. Ili kuhakikisha shughuli za madini zinakuwa na tija na athari zake zinadhibitiwa, kaguzi mbalimbali hufanyika kwa ajili ya kuhakikisha usalama wa watu na mazingira katika maeneo yenye shughuli za madini. Katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022, ukaguzi 26 umefanyika katika migodi mikubwa ya Geita Gold Mine (GGM), Williamson Diamond Limited (WDL) na North Mara (NMGM). 46. Mheshimiwa Spika, pia ukaguzi ulifanyika katika migodi ya kati sita (6) ambayo ni: migodi ya dhahabu ya Shanta (Singida Gold Project); PU BO Mining Ltd; Sunshine (Singida), ZEM (T) Co. Ltd; Cata Mining Co. Ltd (Mara) na Busolwa Mining Ltd (Geita). Aidha, leseni 5,246 za uchimbaji mdogo zilikaguliwa katika mikoa mbalimbali ya kimadini nchini. 

Mheshimiwa Spika, kutokana na kaguzi zilizofanyika, migodi mingi imeonekana kuwa inazingatia taratibu za uendeshaji migodi kwa mujibu wa sheria. Hata hivyo, katika baadhi ya migodi, kaguzi zilibainisha kuwepo kwa hali ya kutozingatiwa kwa taratibu za uendeshaji wa migodi. Hali hiyo ni pamoja na: uwepo wa makazi na shughuli za uchimbaji mdogo karibu na migodi, kutozingatiwa kwa utaratibu wa utunzaji wa mazingira, kutokuwepo kwa wataalamu na wasimamizi wa masuala ya usalama wa wafanyakazi na mazingira migodini, ukosefu wa vifaa vya usalama kwa wafanyakazi na kutokuwepo kwa stoo za kuhifadhia baruti. 27 

Mheshimiwa Spika, kutokana na mapungufu yaliyobainika katika baadhi ya migodi, Wizara kupitia Tume ya Madini imechukua hatua kadhaa zenye lengo la kuhakikisha kuwa kasoro zilizobainika zinarekebishwa. Hatua hizo ni pamoja na kutoa maelekezo mahsusi kwa wamiliki wa migodi hiyo kuchukua hatua za kuondoa upungufu uliobainika wakati wa kaguzi. 

Mheshimiwa Spika, Wizara pia imeandaa mpango wa kutoa mafunzo kwa ajili ya uchimbaji salama, utunzaji wa mazingira, usalama wa wafanyakazi pamoja na usimamizi salama wa baruti kwa wachimbaji wadogo na utekelezaji wake umeanza. Nitoe wito kwa wachimbaji madini wote hapa nchini kufanya shughuli zao kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zinazosimamia Sekta ya Madini ili kuhakikisha shughuli za uchimbaji zinakuwa endelevu kwa kuzingatia afya, usalama wa watu na mazingira katika maeneo ya migodi. 

Mheshimiwa Spika, katika kuzijengea uwezo taasisi zake, Wizara imewezesha ununuzi wa vitendea kazi kwa ajili ya maabara pamoja na kuanza ujenzi wa jengo la kuhifadhia sampuli za miamba (coreshed) linalojengwa eneo la Kizota – Dodoma kwa ajili ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa 28 Madini Tanzania (GST). Aidha, ili kuimarisha usimamizi, ufuatiliaji na ukusanyaji wa maduhuli, Tume ya Madini iliwezeshwa kupata fedha za kununua magari 40 ambapo hadi sasa magari saba (7) yamekwishapokelewa (Picha Na. 6). Vilevile, STAMICO iliwezeshwa kupata vifaa vya utafutaji na uchimbaji wa madini ambavyo ni excavator, drill rig, crane na survey equipment ili kuimarisha shughuli hizo. Picha Na. 6: Waziri wa Madini Mhe. Dkt. Doto Biteko akizindua Magari kwa ajili ya Tume ya Madini. 

Mheshimiwa Spika, watumishi ni rasilimali muhimu zaidi katika taasisi yoyote kwa sababu ndiyo inayowezesha rasilimali nyingine kutumika kwa tija na kuleta mafanikio katika sekta zote za 29 uchumi ikiwemo Sekta ya Madini. Katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, watumishi 400 wa Wizara na taasisi zake wamepandishwa vyeo. Aidha, watumishi 94 wamehudhuria mafunzo ya muda mrefu na Watumishi 55 wamewezeshwa kuhudhuria mafunzo ya muda mfupi katika nyanja mbalimbali nje na ndani ya nchi. 

 Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kuboresha mazingira ya kazi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa majengo matatu (3) ya ofisi. Majengo hayo ni ofisi za Makao Makuu ya Wizara katika Mji wa Serikali - Mtumba, ofisi ya Makao Makuu ya Tume ya Madini – eneo la Kilimani Dodoma na ofisi ya Afisa Madini Mkazi (RMO) - Geita. Aidha, vitendea kazi mbalimbali vimenunuliwa vikiwemo magari na kompyuta kwa ajili ya kuwawezesha watumishi kufanya kazi kwa ufanisi. IV. Utekelezaji wa Miradi ya Maendeleo 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha kuanzia Julai, 2021 hadi Machi, 2022, Fedha za Maendeleo kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali zilizopokelewa ni shilingi bilioni 7.4, ambapo shilingi bilioni 1.52ni kutoka kwenye bajeti ya maendeleo ya mwaka wa fedha unaoendelea na shilingi bilioni 5.9 ni kutoka katika Akaunti ya 30 Amana. Miradi iliyotekelezwa ni pamoja na: ukamilishaji wa ujenzi wa vituo vya umahiri vya Songea, Mpanda na Chunya; ujenzi wa ofisi za Makao Makuu ya Wizara awamu ya pili katika Mji wa Serikali – Mtumba; ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Tume ya Madini – eneo la Kilimani Dodoma; kuanza hatua za awali za ujenzi wa jengo la ofisi ya Afisa Madini Mkazi – Geita na ununuzi wa vifaa vya maabara na vitendea kazi kwa ajili ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST). V. Utekelezaji katika Maeneo Mengine (a) Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania na Wajibu wa Kampuni kwa Jamii katika Sekta ya Madini 

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa wananchi kushiriki katika shughuli za uzalishaji kwa kuzifungamanisha Sekta ya Madini na nyingine ili kuendelea kukuza uchumi wao na wa Taifa kwa ujumla. Ili kulitekeleza hilo, Serikali imeweka Sheria na Kanuni za Mpango wa Ushirikishaji wa Watanzania (Local Content) na wajibu wa kampuni kwa jamii (Corporate Social Responsibility). Kwa mujibu wa Sheria ya Madini Sura 123, kila mgodi unapaswa kuajiri wataalam wa ndani na kutumia bidhaa na huduma kwa kadri 31 zinavyopatikana nchini. Suala hili linasimamiwa kwa kuzitaka kampuni zote zinazojishughulisha na utafutaji, uchimbaji, usafishaji na biashara ya madini kuwasilisha Mipango ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika shughuli zao. 

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha Julai 2021 hadi Machi 2022, Wizara kupitia Tume ya Madini ilipokea na kuchambua jumla ya mipango 378 ya ushirikishwaji wa watanzania katika Sekta ya Madini kutoka kwa wamiliki wa leseni za madini na watoa huduma migodini, ambapo mipango 366 kati ya hiyo ilikidhi vigezo na kuidhinishwa. Mipango 12 iliyobaki haikukidhi vigezo na wahusika walielekezwa kuifanyia maboresho kwa mujibu wa Sheria ya Madini Sura 123. 

Mheshimiwa Spika, kati ya kampuni 378 zilizowasilisha na kuidhinishiwa mipango ya ushirikishwaji wa watanzania, kampuni 10 ni za uchimbaji mkubwa, 14 uchimbaji wa kati, 4 uchimbaji mdogo, 7 za utafutaji wa madini, 3 leseni ya usafishaji na kampuni 340 za watoa huduma migodini. 

Mheshimiwa Spika, ushiriki wa Watanzania katika shughuli za madini umeendelea kuimarika na 32 kuongezeka. Katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022, idadi ya watanzania walioajiriwa katika kampuni za utafutaji, uchimbaji, usafishaji na watoa huduma imefikia 14,308 ikilinganishwa na 7,151 katika kipindi kama hicho Mwaka wa Fedha 2020/2021. Ongezeko hilo ni sawa na asilimia 100. Aidha, katika kipindi rejewa shilingi trilioni 5.2 zimetumiwa na migodi kulipia bidhaa na huduma mbalimbali zinzozalishwa nchini zilizotolewa katika migodi hiyo ikilinganishwa na shilingi trilioni 2.4 zilizotumika katika kipindi kama hicho Mwaka wa Fedha 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kufuatilia na kusimamia wajibu wa kampuni kwa jamii zinazozunguka migodi (CSR). Katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022, migodi 13 ilitoa jumla ya shilingi 16,078,138,114.00 kwa ajili ya miradi ya afya, elimu, maji, barabara, na miradi ya kiuchumi katika Halmashauri za Wilaya ya Tarime, Msalala, Nyang’hwale, Kahama, Songwe, Geita na Geita Mji. Miradi hii imeboresha hali za maisha ya wananchi wa maeneo hayo na kuleta maendeleo katika Halmashauri zinazozunguka migodi. 33 (b) Uboreshaji wa Sheria, Kanuni na Miongozo katika Sekta ya Madini 

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhakikisha kuwa wawekezaji katika Sekta ya Madini wanafanya kazi zao katika mazingira ya kisheria yenye tija kwa pande zote mbili yaani Serikali na Wawekezaji. Katika kutekeleza hilo, maboresho mbalimbali katika Sheria, na Kanuni zinazosimamia Sekta ya Madini yamefanyika. Miongoni mwa maboresho hayo ni pamoja na marekebisho katika Kanuni za Madini (Eneo Tengefu la Mirerani), (The Mining (Mirerani Controlled Area) (Amendment) Regulations, 2021).

Mheshimiwa Spika, marekebisho hayo yanaelekeza kuwa biashara ya madini ya Tanzanite pamoja na shughuli zote za ukataji, ung’arishaji au shughuli za uongezaji thamani madini kufanyika ndani ya Eneo Tengefu la Mirerani au eneo lolote la Mirerani litakaloidhinishwa kwa maandishi. Kanuni hizo zilizoanza kutumika tarehe 9 Julai, 2021 zilitangazwa katika Tangazo la Serikali Na. 592 la tarehe 9 Julai, 2021.

Mheshimiwa Spika, marekebisho mengine yamefanyika katika Kanuni za Madini (Haki Madini) za Mwaka 2018 ambayo yanamwezesha Waziri 34 kuondoa masharti ya kanuni zinazohusu haki madini kwa waombaji wa leseni za Uchimbaji wa Kati (Mining Licence) na Leseni za Uchimbaji Mkubwa (Special Mining Licence) ambao watakuwa na makubaliano maalum na Serikali ambayo kwayo Serikali ni mwanahisa au itakuwa mwanahisa. Marekebisho hayo yamefanyika kupitia Tangazo la Serikali Na. 593 la tarehe 9 Julai, 2021. Lengo la marekebisho hayo ni kuiwezesha Serikali kushiriki kikamilifu kama mbia katika uendeshaji wa shughuli za uchimbaji wa madini. (c) Kuelimisha Umma Kuhusu Sekta ya Madini 

Mheshimiwa Spika, katika kutoa elimu kwa umma kuhusu Sekta ya Madini, masuala yanayopewa kipaumbele ni pamoja na: uelewa kuhusu Sera na Sheria; wajibu wa kampuni kwa jamii; ushiriki wa watanzania; matumizi ya teknolojia bora katika uchimbaji na uchenjuaji wa madini; uhifadhi na matumizi bora ya baruti; taratibu za utoaji wa leseni za madini; umuhimu wa masoko ya madini; fursa za uwekezaji; na usalama, afya na utunzaji wa mazingira. Katika kutoa elimu kwa umma njia mbalimbali hutumika ikiwa ni pamoja na 35 mikutano, maonesho, redio, runinga, magazeti, tovuti na mitandao ya kijamii. (d) Uendelezaji na Uboreshaji wa Eneo Tengefu la Mirerani 

Mheshimiwa Spika, kufuatia kukamilika kwa ujenzi na usimikaji wa miundombinu ikiwemo taa, kangavuke, kamera za ulinzi na barabara inayozunguka ukuta kwa ndani katika Eneo Tengefu la Mirerani, hivyo udhibiti wa utoroshaji wa madini ya Tanzanite umeimarika. Hatua zilizochukuliwa na Serikali zimeboresha upatikanaji wa tozo stahiki zinazotokana na biashara ya madini hayo. Kabla ya ujenzi na usimikaji wa miundombinu, uzalishaji ulikuwa kilogramu 1,964.75 kwa mwaka 2018/2019 ikilinganishwa na kilogramu 3,198.65 za tanzanite zilizozalishwa kipindi cha kuanzia Julai 2021 hadi Machi 2022. (e) Kusimamia Shughuli za Baruti na Utekelezaji wa Sheria ya Baruti.

Mheshimiwa Spika, baruti ni muhimu katika shughuli za uchimbaji wa madini na hutumika kulipua miamba migumu wakati wa uchimbaji wa madini. Pamoja na umuhimu wake katika shughuli za madini, baruti ina madhara makubwa ikitumika au kuhifadhiwa isivyo salama. Ili kuhakikisha kuwa 36 baruti haileti madhara kwa jamii na mazingira, Serikali imeweka utaratibu wa utoaji wa vibali vya uagizaji, utengenezaji, usafirishaji, utunzaji na utumiaji wa baruti. 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 vibali vya baruti vilitolewa kwa kampuni na wafanyabiashara mbalimbali kama ifuatavyo: vibali 225 vya kuingiza baruti nchini; vibali 21 vya kufanya biashara ya baruti; vibali 21 vya kusafirisha baruti kwenda nje ya nchi; na vibali 37 vya kupitisha baruti nchini kwenda nchi nyingine. Aidha, vibali saba (7) vya kutengeneza baruti vimetolewa kwa kampuni tatu ambazo ni Dangote Company Limited (Mtwara), Mbogo Mining and General Supply Limited (Pwani na Mbinga) na Orica (T) Limited (Geita). 

Mheshimiwa Spika, leseni tatu (3) za viwanda vya kutengeneza baruti zimetolewa kwa kampuni mbili (2) ambazo ni Mbogo Mining and General Supply Limited (Leseni ya kutengeneza detonator explosives Wilaya ya Magu - Mwanza) na kampuni ya Solar Nitrochemicals Limited (Leseni ya kutengeneza ANFO na Emulsion na leseni ya kutengeneza detonators explosives Kisarawe – Pwani). Aidha, leseni sita (6) za kutengeneza baruti kwa kutumia magari maalum 37 (Mobile Manufacturing Unit - MMU) zilitolewa kwa kampuni mbili (2) za Solar Nitrochemicals Limited na Nitro explosive (T) Limited. Solar Nitrochemicals Limited imepewa leseni nne (4) na Nitro explosive (T) Limited imepewa leseni mbili (2). Pia, leseni 18 za maghala ya kuhifadhia baruti zimetolewa kwa kampuni na wafanyabiashara wa baruti. Vibali na leseni za baruti vilivyotolewa zimeipatia Serikali jumla ya shilingi 453,053,800.0.

Mheshimiwa Spika, kutolewa kwa leseni za viwanda vya kuzalisha baruti nchini ni hatua muhimu kiuchumi kwani viwanda hivyo vitakapoanza uzalishaji vitakuwa na manufaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutoa ajira, kulipa kodi Serikalini na uhakika wa upatikanaji wa baruti kwa wakati na kwa gharama nafuu. 

Mheshimiwa Spika, kutokana na madhara yanayoweza kusababishwa na matumizi yasiyokuwa sahihi ya baruti, ukaguzi ulifanyika ili kufuatilia utengenezaji na utunzaji wa baruti katika viwanda vya kutengeneza baruti katika kampuni tatu (3) ambazo ni Mbogo Mining & General Supply Limited mkoani Mwanza, Solar Nitrochemical Limited mkoani Pwani na Nitro Explosive (T) Limited mkoani Lindi ambapo kampuni ya Mbogo Mining & General Supply 38 Limited na Solar Nitrochemicals Limited zilikidhi vigezo na kupewa leseni. Aidha, kampuni ya Nitro Explosive (T) Limited haikupewa leseni kwa kuwa ujenzi wake haukukidhi matakwa ya Sheria ya Baruti. 

Mheshimiwa Spika, kaguzi nyingine za baruti zilifanyika kwenye ujenzi wa maghala ya kuhifadhia baruti kwa kampuni za Zem Development Co. Limited Mkoa wa Shinyanga na Ilolo Investment Limited Mkoa wa Lindi na leseni za maghala ya kuhifadhia baruti zilitolewa kwa kampuni hizo. Aidha, ukaguzi ulifanyika kwenye eneo la ujenzi wa kiwanda cha kutengeneza baruti cha kampuni ya Tan Nobel Company Limited katika kijiji cha Makombe – Bagamoyo. Kibali kilitolewa kwa kampuni hiyo baada ya kukidhi matakwa ya Sheria ya Baruti na Kanuni zake. 

Mheshimiwa Spika, kaguzi tatu (3) zilifanyika kwenye maeneo ya ujenzi wa maghala ya kuhifadhia baruti katika vijiji vya Kinzagu na Makombe, Wilaya ya Bagamoyo na kijiji cha Makanga Vigoli, Wilaya ya Ulanga. Kupitia kaguzi hizo vibali vya ujenzi wa maghala ya kuhifadhia baruti vilitolewa kwa wahusika baada ya kujiridhisha kuwa maeneo 39 yaliyopendekezwa yanafaa kwa mujibu wa Sheria ya Baruti. (f) Masuala Mtambuka 

Mheshimiwa Spika, moja ya masuala mtambuka yanayotekelezwa na Wizara ni pamoja na kutoa elimu na huduma kwa waathirika wa UKIMWI na Magonjwa Sugu Yasiyoambukizwa (MSY). Wizara imeendelea kutoa huduma kwa watumishi waliojitokeza wanaoishi na Virusi vya UKIMWI kwa kutoa fedha kwa ajili ya lishe bora, dawa na vifaa kinga ili kuimarisha afya zao. Aidha, mafunzo kuhusu udhibiti wa MSY kwa watumishi na upimaji wa hiari umekuwa ukifanyika mara kwa mara. 

Mheshimiwa Spika, kwa lengo la kuboresha afya za watumishi na kuimarisha ushirikiano mahali pa kazi, Wizara imeshiriki katika mabonanza na michezo mbalimbali iliyofanyika nchini, ikiwemo SHIMIWI. Pia, Wizara imeendelea kuhamasisha watumishi kujua afya zao na kujikinga na magonjwa yanayoambukizwa ukiwemo UVIKO-19. VI. Utekelezaji wa Shughuli za Taasisi Zilizo Chini ya Wizara 

Mheshimiwa Spika, Wizara inasimamia taasisi tano (5), ambazo ni Tume ya Madini; Taasisi 40 ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST); Shirika la Madini la Taifa (STAMICO); Taasisi ya Uhamasishaji Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali za Madini, Mafuta na Gesi Asilia (TEITI) na Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC). 

Mheshimiwa Spika, taasisi hizi zimekasimiwa majukumu mbalimbali kama ifuatavyo: Tume ya Madini ina jukumu la kusimamia na kudhibiti shughuli zote zinazohusiana na Sekta ya Madini zikiwemo utafutaji, uchimbaji, uongezaji thamani na biashara ya madini; Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) lina majukumu ya kuwekeza katika miradi ya kimkakati kwa niaba ya Serikali na kuwaendeleza wachimbaji wadogo; GST ina jukumu la kutoa takwimu na taarifa za jiosayansi na majanga asili ya jiolojia ili kuwezesha kufanya maamuzi sahihi katika uwekezaji endelevu; TEITI ina jukumu la kuhakikisha uwazi na uwajibikaji katika uvunaji wa rasilimali madini, mafuta na gesi asilia; na TGC ina jukumu la kutoa mafunzo ya uongezaji thamani madini ikiwa ni pamoja na utambuzi, ukataji, uchongaji, ung’arishaji wa madini ya vito na utengenezaji wa bidhaa za usonara. Utekelezaji kwa kila taasisi ni kama ifuatavyo: - 41 (a) Tume ya Madini 

Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2021/2022 pamoja na kutekeleza jukumu la kusimamia uzalishaji wa madini na ukusanyaji wa maduhuli kama ilivyoainishwa hapo awali, Tume ya Madini imetekeleza kazi zifuatazo: - (i) Utoaji wa Leseni za Madini 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022, Tume ya Madini imetoa jumla ya leseni 8,172 ikilinganishwa na leseni 6,314 katika kipindi kama hicho Mwaka wa Fedha 2020/2021, sawa na ongezeko la asilimia 17.3. Leseni hizo zinajumuisha leseni mbili (2) za uchimbaji mkubwa, leseni 5 za uchimbaji wa kati, leseni 282 za utafutaji wa madini, leseni 5,937 za uchimbaji mdogo, leseni 49 za uchenjuaji wa madini, leseni mbili (2) za usafishaji wa madini na leseni 1,895 za biashara ya madini. (ii) Usimamizi wa Masoko ya Madini Nchini 

Mheshimiwa Spika, tangu kuanzishwa kwa utaratibu wa kuwa na masoko ya madini mwaka 2019, idadi ya masoko na vituo vya ununuzi vilivyoanzishwa hadi kufikia Machi, 2022 ni 42 na 75 mtawalia. Kwa mwaka 2021/2022 yameanzishwa 42 masoko mawili (2) na vituo 17 vya ununuzi wa madini. Masoko na vituo hivi vimeongeza ufanisi na tija kwenye usimamizi wa biashara ya madini na ukusanyaji wa maduhuli hapa nchini. Aidha, utaratibu huo umechangia kupunguza utoroshaji na biashara haramu ya madini. Niendelee kuwasihi wananchi na wadau wote kuuza na kununua madini katika masoko na vituo vinavyotambulika. 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 thamani ya biashara ya madini katika masoko ya madini imeongezeka na kufikia takribani shilingi trilioni 1.782. Kutokana na biashara hiyo Serikali imekusanya mrabaha na ada ya ukaguzi ya takribani shilingi bilioni 123.58, ikilinganishwa na shilingi bilioni 109.23 katika kipindi kama hicho Mwaka wa Fedha 2020/2021 sawa na ongezeko la asilimia 13.14. (iii) Utambuzi na Uthaminishaji wa Madini Yanayosafirishwa Nje ya Nchi 

Mheshimiwa Spika, ili Serikali iweze kupata mapato yake stahiki kutokana na madini yanayosafirishwa nje ya nchi, Sheria inaitaka Tume ya Madini kufanya utambuzi na uthaminishaji wa madini pamoja na kutoa vibali vya usafirishaji. 43 Katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 madini yaliyosafirishwa nje ya nchi yalihusisha dhahabu, almasi, madini ya vito ghafi, vito vilivyokatwa na kusanifiwa, madini ya ujenzi, madini ya bati (tin), madini ya shaba, makaa ya mawe na mengineyo yenye jumla ya thamani ya takribani shilingi trilioni 8.3 na kuipatia Serikali mapato ya shilingi bilioni 597.53. (iv) Ukaguzi wa Hesabu za Fedha na Kodi 

Mheshimiwa Spika, Tume ya Madini ina jukumu la kukagua hesabu za fedha za migodi mikubwa na ya kati ili kubaini gharama za uwekezaji na uendeshaji kwa madhumuni ya kukusanya taarifa za kikodi na kuziwasilisha Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na mamlaka nyingine zinazohusika. Katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 Tume ya Madini ilifanya kaguzi za hesabu za fedha na mapitio ya kodi kwa kampuni nane (8). Kati ya hizo, kaguzi tano (5) zilihusu miradi ya barabara inayotumia madini ujenzi na kaguzi tatu (3) zilihusu migodi ya kati ya uchimbaji wa madini ya dhahabu ambayo ni CATA Mining Company Ltd, Zem Tanzania Company Ltd na MMG Gold Limited zilizopo mkoani Mara. 44 

Mheshimiwa Spika, kaguzi hizo zilibaini kutolipwa ipasavyo kwa mrabaha pamoja na ada ya ukaguzi; kujumuishwa kwa gharama zisizostahili katika ukokotoaji wa kodi; na kuwepo kwa baadhi ya watoa huduma ambao hawakutozwa kodi ya zuio. Aidha, ilibainika kuwa kuna utekelezaji hafifu wa matakwa ya Sheria ya Madini kuhusu uwajibikaji wa kampuni kwa jamii na ukiukwaji wa baadhi ya kanuni za ushirikishwaji wa watanzania na hatua stahiki zilichukuliwa. 

Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika kwa ukaguzi kwa kampuni tano za ujenzi wa barabara, ilibainika uwepo wa malipo pungufu ya maduhuli mbalimbali ya Serikali kiasi cha shilingi 2,214,129,611.72. Kampuni hizo zimekubali kulipa maduhuli hayo ambayo awali hayakulipwa. (v) Huduma za Maabara 

Mheshimiwa Spika, Tume ya Madini ina maabara moja iliyopo jijini Dar es Salaam. Maabara hiyo hutumika katika uchunguzi wa ubora, kiasi cha madini na aina za madini yaliyozalishwa na wachimbaji wakubwa, wa kati na wadogo hapa nchini. Hadi Machi 2022, sampuli 1,398 za mikuo ya dhahabu (gold bars) 45 na sampuli 851 za madini ya shaba kutoka katika migodi mikubwa na ya kati zilifanyiwa uchunguzi katika maabara hiyo. Uchunguzi huo ulilenga kupata kiasi halisi na thamani ya madini kwa ajili ya kuhakiki kiasi cha tozo ambacho Serikali inapaswa kulipwa kutokana na thamani halisi ya madini hayo. 

Mheshimiwa Spika, maabara hii pia inatoa huduma kwa wadau mbalimbali wa madini ambapo katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 imefanya uchunguzi wa sampuli 2,267 na kukusanya ada ya huduma kiasi cha shilingi 195,524,000. (vi) Uendelezaji na Usimamizi wa Mifumo ya TEHAMA 

Mheshimiwa Spika, Tume ya Madini imeendelea na ujenzi wa mfumo mpya wa utoaji na usimamizi wa leseni za madini. Hadi Machi, 2022 ujenzi wa mfumo huo umefikia asilimia 52. Ujenzi na uendelezaji wa mfumo huo unafanywa na wataalamu wa ndani ya nchi. 

Mheshimiwa Spika, Tume ya Madini imeendelea kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa maduhuli yatokanayo na madini ya ujenzi 46 na viwandani kwa kutumia mashine za Point of Sale (PoS). Utaratibu wa kutumia PoS umeonesha matokeo chanya katika ukusanyaji wa maduhuli. Takwimu zinaonesha kuwa, kabla ya matumizi ya PoS wastani wa makusanyo kwa kipindi cha Oktoba 2020 hadi Februari 2021 makusanyo yatokanayo na madini ya ujenzi yalikuwa shilingi 5,852,566,156.38 ikilinganishwa na shilingi 6,489,501,216.12 baada ya matumizi ya PoS kwa kipindi kama hicho Mwaka 2021/2022 ikiwa ni ongezeko la asilimia 9.3. Kutokana na mafanikio hayo, Tume ya Madini inaendelea kuimarisha matumizi ya mashine za PoS katika vyanzo vyote vya ukusanyaji wa maduhuli yatokanayo na madini ya ujenzi na ya viwandani. (b) Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) 

Mheshimiwa Spika, STAMICO imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya utafutaji, uchimbaji, uchenjuaji, usafishaji na uuzaji wa madini pamoja na kutoa huduma mbalimbali katika Sekta ya Madini ikiwemo uchorongaji na utoaji wa ushauri wa kitaalam. Utekelezaji wa majukumu hayo unafanyika kupitia njia tatu (3) ambazo ni: kuanzisha na kuendeleza miradi yake yenyewe ikiwa 47 ni pamoja na kutoa huduma za uchorongaji na ushauri wa kitaalam; kuendeleza na kusimamia kampuni tanzu; na kuendesha kampuni za ubia. (i) Kuanzisha na Kuendeleza Miradi yake Yenyewe 

 Mheshimiwa Spika, Shirika linatekeleza miradi mitatu (3) kupitia vyanzo vyake vya mapato mbalimbali. Miradi hiyo ni: mradi wa makaa ya mawe wa Kabulo-Kiwira; mradi wa makaa ya kupikia (coal briquettes); na mradi wa kuuza kemikali na vilipuzi. 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022, katika mradi wa Kabulo, tani 17,324 za makaa ya mawe zilichimbwa ambapo tani 12,792 zenye thamani ya shilingi 1,063,312,091.0 ziliuzwa na kulipa serikalini shilingi 174,191,290.87 ikiwa ni mrabaha na ada ya ukaguzi. Aidha, shirika limeingia makubaliano ya awali na TANESCO ya kuendeleza mradi wa Kiwira ambapo shirika litakuwa na jukumu la kuchimba makaa ya mawe na TANESCO kuzalisha umeme wa MW 200 na kuusambaza. 48 

Mheshimiwa Spika, shirika limeanza kutekeleza Mpango Mkakati wa Uchimbaji wa Makaa ya Mawe kwa wingi (Massive Coal Mining Plan – 1,200,000 tons/year) ambao unalenga kuongeza ubora na uzalishaji ili kumudu ushindani katika soko na kuongeza mauzo. Ili kufikia lengo hilo STAMICO imekamilisha ukarabati wa mgodi wa chini wa Kiwira na inaendelea na matengenezo ya barabara kupitia mto Mwalisi ambayo inaunganisha mgodi wa Kabulo na Kiwira. Ukarabati wa barabara unaendelea na matengenezo ya daraja yamekamilika na linapitika. Barabara hiyo itapunguza gharama ya usafirishaji wa makaa ya mawe kutokana na kupungua kwa umbali kutoka kilometa 38 mpaka kilometa 7. Picha Na. 7: Daraja la Mto Mwalisi 49 

Mheshimiwa Spika, ili kupunguza changamoto ya uharibifu wa mazingira, STAMICO imeanzisha mradi wa makaa ya kupikia (Coal briquettes). Kwa kuanzia shirika limenunua na kusimika mtambo wa majaribio wenye uwezo wa kuzalisha tani 2 kwa saa ambao umejaribiwa na kuonesha mafanikio. Aidha, shirika limeagiza mitambo miwili mingine yenye uwezo wa kuzalisha tani 20 kwa saa kwa kila mmoja inayotegemewa kuwasili nchini ifikapo Juni, 2022. Tayari TBS wameshawapatia STAMICO cheti cha ubora wa makaa hayo na hivyo uzalishaji mkubwa unatarajia kuanza. 

Mheshimiwa Spika, shirika limeanzisha mradi wa kuuza kemikali, baruti na vilipuzi kwa wachimbaji wadogo. Mradi huu unatekelezwa kwenye vituo vya mfano vya Lwamgasa, Katente na Itumbi na katika mgodi wa STAMIGOLD. Aidha, shirika linategemea kuanza kuuza kemikali na vilipuzi katika migodi mingine ya kati na mikubwa nchini ili kuongeza wigo wa wateja wake na kusogeza huduma hiyo karibu na wachimbaji. Shirika limeanza hatua za ununuzi wa baruti, vilipuzi na kemikali ili kuwawezesha wachimbaji wadogo kupata zana hizo karibu na maeneo yao ya kazi. Hadi Machi, 50 2022 shirika limepata mapato ya shilingi 568,983,500 kutokana na mauzo ya kemikali na vilipuzi. (ii) Huduma za Uchorongaji na Ushauri wa Kitaalam 

Mheshimiwa Spika, hadi Machi, 2022 STAMICO ina mitambo tisa (9) ya uchorongaji. Aidha, shirika limenunua mitambo mitano (5) ya uchorongaji ambayo inatarajiwa kuwasili nchini kabla ya Juni, 2022 na kufanya shirika kuwa na jumla ya mitambo 14. Ongezeko la mitambo hiyo litawezesha shirika kutekeleza kandarasi za uchorongaji kwa mfumo wa RC na DD kwa ufanisi. Naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa mafanikio hayo yanatokana na maboresho ya kimuundo pamoja na usimamizi wa shirika yaliyofanywa na Serikali kupitia Wizara ya Madini. Vilevile, kwa kipindi cha Mwaka wa Fedha 2021/2022 shirika limepata kandarasi kubwa tatu (3) za uchorongaji zenye thamani ya shilingi bilioni 17.5. 51 (iii) Kampuni Tanzu ya STAMIGOLD 

Mheshimiwa Spika, kampuni ya STAMIGOLD inamilikiwa na STAMICO kwa hisa asilimia 99 na Ofisi ya Msajili wa Hazina inamiliki asilimia 1 ya hisa. Katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 mgodi umezalisha wakia 7,106 za dhahabu na wakia 1,059 za madini ya fedha zote kwa pamoja zikiwa na thamani ya shilingi bilioni 29.84. kutokana na mauzo hayo, shilingi bilioni 2.09 zimelipwa Serikalini kama mrabaha, ada ya ukaguzi, tozo mbalimbali na kutoa huduma kwa jamii inayozunguka mgodi.

Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kuongeza uhai wa mgodi, STAMIGOLD ilifanya utafiti kwenye eneo la mgodi na kubaini uwepo wa akiba ya tani 2,769,919 za mashapo ya dhahabu zenye kiwango cha 1.00g/t ambazo ni sawa na wakia 88,800. Uwepo wa mashapo hayo utaongeza uhai wa mgodi kwa miaka mitano (5) kuanzia Juni, 2021. Aidha, mgodi bado una mashapo dhaniwa (Inferred Resource) ndani ya SML157/2003 yenye wakia 106,854 za dhahabu ambazo utafiti wake bado unaendelea. Inakadiriwa kwamba matokeo ya utafiti huo yataongeza uhai wa mgodi kwa miaka 7 na hivyo 52 kufanya maisha ya mgodi kuongezeka hadi miaka 12. 

Mheshimiwa Spika, mgodi wa STAMIGOLD umekuwa na changamoto ya gharama kubwa za uzalishaji kutokana na kutumia nishati ya mafuta katika kuzalisha umeme. Ili kuondoa changamoto hiyo, kazi ya kuunganisha mgodi katika gridi ya Taifa kupitia TANESCO imeendelea ambapo umeme umeshafika katika eneo la mgodi na hatua ya kukamilisha kituo kidogo cha kupozea umeme (sub station) ili uanze kutumika inaendelea. Mgodi unatarajiwa kuokoa takribani shilingi milioni 700 kwa mwezi baada ya kuanza kutumia umeme wa TANESCO. 

Mheshimiwa Spika, mgodi pia umeendelea kulipa deni la wazabuni na watoa huduma ambapo hadi Desemba, 2021 kampuni ya STAMIGOLD ilikuwa inadaiwa shilingi bilioni 21.032. Deni hilo lilianza kulipwa Januari, 2022 kwa mujibu wa makubaliano yaliyofanyika ya kulipa shilingi 572,000,000 kila mwezi ambapo hadi Machi, 2022 malipo ya shilingi 1,716,000,000 yamefanyika. STAMIGOLD itaendelea kulipa deni kulingana na makubaliano. 53 (iv) Miradi inayotekelezwa kwa Ubia Kiwanda cha Kusafisha Dhahabu - Mwanza 

Mheshimiwa Spika, kiwanda cha Mwanza Precious Metal Refinery kina uwezo wa kusafisha dhahabu kwa kiwango cha kimataifa cha 999.9 purity. Kiwanda hiki bado kinafanya kazi kwa kiwango cha chini ikilinganishwa na uwezo wake wa uzalishaji. Ili kukabiliana na changamoto hiyo na kuongeza uzalishaji kiwanda kimetenga dola za Marekani milioni 150 ikiwa ni mtaji wa kununua dhahabu ghafi. 9

Mheshimiwa Spika, kiwanda pia kimeanzisha kampuni ya Aurun Pinnacle Company Ltd (APCL) kwa lengo la kuwasaidia wachimbaji wadogo kuongeza uzalishaji na kukiuzia kiwanda dhahabu ghafi. Vilevile, STAMICO imesaini mkataba wa makubaliano wenye thamani ya dola za Marekani milioni 300 na kampuni ya ACME kwa ajili ya kufanya utafiti. Utafiti huo utahusisha uchorongaji katika leseni mbalimbali ili kuongeza uzalishaji wa dhahabu ghafi kwa ajili ya kiwanda hicho. Kadhalika, ili kuwezesha dhahabu iliyosafishwa 54 kutambulika kimataifa kiwanda kinaendelea na taratibu za kupata ithibati (ISO Accreditation). Picha Na. 8: Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizindua kiwanda cha kusafisha madini ya dhahabu cha Mwanza Precious Metals Gold Refinery kilichopo jijini Mwanza. Mradi wa Dhahabu wa Buhemba 

Mheshimiwa Spika, mradi wa Buhemba ni wa ubia kati ya STAMICO inayomiliki hisa asilimia 35 na kampuni ya GOODFIELD International DMCC ya Dubai inayomiliki hisa asilimia 65 kupitia leseni ya uchimbaji madini Na. ML 646/2021. Mgodi uliingia makubaliano ya uchorongaji ya awamu ya kwanza na STAMICO (mita 4,000 kwa njia ya RC na mita 55 1,200 DD) yenye thamani ya shilingi bilioni 1.25 ili kuongeza kiasi cha mashapo. 

Aidha, Februari, 2022 shirika lilisaini makubaliano kwa ajili ya awamu ya pili ya uchorongaji wa mita 40,000 (mita 10,000 DD na mita 30,000 RC) katika mgodi wa Buhemba yenye thamani ya shilingi bilioni 11.5. 101. Mheshimiwa Spika, uanzishwaji wa mradi huo utakuwa na manufaa makubwa kwa Taifa kupitia malipo ya mrabaha na tozo mbalimbali ikiwemo ushuru wa huduma kwa Halmashauri ya Wilaya ya Butiama na ajira zaidi ya 300. Mgodi katika mwaka 2022, unatarajia kutoa kiasi cha dola za Marekani 200,000 kwa jamii inayoishi maeneo ya jirani na mgodi. Mgodi wa Dhahabu wa Buckreef 

Mheshimiwa Spika, shirika na mbia mwenza TANZAM2000 wanamiliki mradi wa uchimbaji dhahabu wa Buckreef uliopo Mkoa wa Geita chini ya kampuni ya ubia ya Buckreef Gold Company (BGC). Katika ubia huu STAMICO inamiliki hisa asilimia 45 na mbia mwenza hisa asilimia 55. Thamani ya uwekezaji katika mradi 56 huu ni dola za Marekani milioni 19.6. Mgodi wa Buckreef ulikamilisha uzalishaji wa majaribio Novemba, 2021. Kufuatia kukamilika kwa majaribio hayo, mgodi wa Buckreef umeanza uzalishaji mkubwa wa dhahabu kwa kutumia mtambo wenye uwezo wa kuchakata tani 15 za mbale kwa saa.

Mheshimiwa Spika, kuanzia Novemba, 2021 hadi Machi, 2022 Buckreef imezalisha kilo 60.98 zenye thamani ya shilingi 7,112,327,740.68 na kulipa mrabaha na tozo nyingine Serikalini zenye jumla ya shilingi 497,862,941.85. Aidha, kwa sasa mtambo mkubwa wenye uwezo wa kuchakata tani 30 za mbale kwa saa umefika nchini na usimikaji wake unaendelea. Usimikaji huo utakapokamilika mgodi utakuwa na uwezo wa kuchakata tani 45 za mbale kwa saa. Vilevile, shirika limeanza kutoa huduma ya uchorongaji wa miamba kwa kandarasi ya uchorongaji yenye thamani ya shilingi bilioni 4.3 ikiwa ni uendelezaji wa uchimbaji mkubwa. 57 Picha Na. 9: Shughuli za Uchorongaji zikiendelea katika Mgodi wa Buckreef.

Mheshimiwa Spika, mgodi pia, umelipa fidia ya shilingi 5,639,262,063.82 ambayo ni sawa na asilimia 96 ya fidia yote kwa wananchi 960 walio ndani ya eneo la mradi lenye ukubwa wa kilomita za mraba 9.4. Eneo hilo linahusisha vijiji vya Lwamgasa, Mnekezi na Lubanda. Aidha, Januari, 2022 mgodi uliingia makubaliano na Halmashauri ya Geita ya utekelezaji wa mpango wa wajibu wa kampuni kwa jamii zinazozunguka mgodi (CSR) wenye thamani ya shilingi 321,000,000. 58 (c) Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) 

Mheshimiwa Spika, kazi zilizotekelezwa na GST katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 ni kama ifuatavyo: (i) Kufanya Tafiti za Jiosayansi na Kuboresha Kanzidata ya Taifa ya Taarifa za Miamba na Madini 106. Mheshimiwa Spika, GST ilifanya ugani wa jiolojia kwa lengo la kubaini miamba na madini yanayopatikana kwenye QDS 278 na 290 zilizopo kwenye Hifadhi ya Taifa ya Mwalimu Nyerere na Pori la Akiba la Selous kwenye Mikoa ya Lindi (Liwale), Morogoro (Ulanga) na Ruvuma (Tunduru na Namtumbo). 59 Picha Na. 10: Wataalam wa GST wakiendelea na ugani wa jiolojia katika Pori la Akiba la Selous. 

Mheshimiwa Spika, Matokeo ya utafiti huu yalibaini uwepo wa madini ya urani, chuma na heavy minerals. Aidha, utafiti katika eneo la QDS 316 ulibaini uwepo wa madini ya dhahabu katika Kijiji cha Lukwika Wilaya ya Nanyumbu na utafiti katika QDS 264 ulibaini uwepo wa madini ya dhahabu kwenye eneo la Lumbanga Wilaya ya Malinyi. 60 Picha Na. 11: Wataalamu wa GST wakitoa mrejesho wa utafiti wa madini uliofanyika katika Wilaya ya Malinyi kwa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya. 

Mheshimiwa Spika, GST ilitoa ushauri elekezi (consultancy) wa jiosayansi kwa taasisi za Serikali kuhusu maeneo salama kwa ajili ya ujenzi wa ofisi. Taasisi za Serikali zilizofanyiwa ushauri elekezi ni pamoja na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kwenye eneo la mradi wa ujenzi Njedengwa; Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa ya Kulevya kwenye viwanja vya Njedengwa – Dodoma na Tume ya Nguvu za Atomiki kwenye eneo la Kikombo - Dodoma. 

Mheshimiwa Spika, GST ilikusanya taarifa 260 kutoka kwa wamiliki wa leseni za utafiti na uchimbaji madini ambazo zinaendelea kuchakatwa. Utafiti na uhakiki wa taarifa za 61 uwepo wa madini (Mineral Occurrences) katika mikoa ya Arusha, Manyara, Lindi, Mtwara na Kilimanjaro ulifanyika. Lengo la utafiti huo ni kuandaa ramani za uwepo wa madini katika kila mkoa na kuboresha kanzidata ya madini na Kitabu cha Madini Yapatikanayo Tanzania. Aidha, utafiti wa madini ya viwandani ulikamilika na jumla ya ramani 28 za kuonesha uwepo wa madini mbalimbali ya viwandani zilichorwa. Vilevile, GST ilifanya utafiti na kutoa ushauri elekezi kuhusu madini ya kinywe (graphite) katika Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa. (ii) Kuboresha Huduma za Maabara 

Mheshimiwa Spika, GST ina maabara ya kisasa ya madini ambayo imeendelea kuimarika na majibu ya uchunguzi wa sampuli zinazofanywa na maabara hiyo yanatambulika kimataifa. Katika kuimarisha huduma za maabara hiyo GST imeongeza wigo wa ithibati (ISO Accreditation) katika uchunguzi wa sampuli za dhahabu kwa njia ya uyeyushaji kwa kutumia kemikali (Aqua Regia) na uchunguzi wa makaa ya mawe (ash content) kwa njia ya utofauti wa uzito (gravimetric). 62 

Mheshimiwa Spika, ithibati hizo zinawezesha majibu ya uchunguzi wa sampuli kupitia njia hizo kutambulika na kuaminika kimataifa. Nitoe rai kwa watafiti na wachimbaji wa madini ya dhahabu na makaa ya mawe kutumia maabara ya GST ili kupata majibu yenye uhakika kwa sampuli zao. Picha Na. 12: Wataalam wa GST wakifanya uchunguzi wa sampuli za miamba na udongo katika maabara 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai, 2021 hadi Machi, 2022 maabara ya GST imefanya uchunguzi wa jumla ya sampuli 12,525 za miamba na udongo zilizowasilishwa na wateja mbalimbali sawa na asilimia 83.5 ya lengo la mwaka. Aidha, GST ilitengeneza vyungu (crucibles) 7,930 vya kuyeyushia sampuli za miamba na 63 udongo kwa ajili ya matumizi ya maabara yake. Pia, majaribio ya kupima ubora na uimara wa miamba (geotechnical), petrolojia, jiokemia na uchenjuaji yanaendelea kufanyika kwenye sampuli zinazowasilishwa na wateja mbalimbali. (iii) Majanga ya Asili ya Jiolojia na Kuelimisha Wananchi Namna Bora za Kupunguza Athari za Majanga Hayo 

 Mheshimiwa Spika, moja kati ya majukumu ya GST ni kuratibu majanga ya asili ya jiolojia kama vile matetemeko ya ardhi; milipuko ya volkano na maporomoko ya ardhi kwa lengo la kutoa ushauri wa namna bora ya kupunguza madhara yanayoweza kutokana na majanga hayo. 

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza jukumu hilo, GST ilifanya uchunguzi wa mvuke uliokuwa ukitoka ardhini katika Kijiji cha Kale, Wilaya ya Kalambo, Mkoa wa Rukwa. Matokeo ya uchunguzi huo yalibaini kuwa tukio hilo la mvuke kutoka ardhini linatokana na mabadiliko ya jiolojia yanayosababishwa na nguvu za asili hasa kwa kuzingatia kwamba Mkoa wa Rukwa upo katika ukanda wa bonde la ufa. Baada ya uchunguzi huo, 64 GST ilitoa taarifa kwa umma kuwa tukio hilo halikuwa na madhara yoyote. 

Mheshimiwa Spika, GST ilifanya uchunguzi wa chanzo cha joto kali kutoka chini ya ardhi lililokuwa likisadikiwa kuwa ni dalili za mlipuko wa volkano ambalo lilisababisha tabaka la juu la udongo kuwaka moto katika Kijiji cha Momwe, Wilaya ya Rombo, Mkoa wa Kilimanjaro. Matokeo ya uchunguzi huo yalionesha kwamba tukio hilo halina uhusiano na mlipuko wa volkano bali ni peat fire iliyosababishwa na mabaki ya mimea (biomass) yenye uozo hafifu (partial decomposition) yaliyojikusanya kwa muda mrefu na kutengeneza tabaka la udongo lenye kiwango kikubwa cha oksijeni, na hivyo kuhifadhi joto linaloweza kusababisha moto kuwaka. Baada ya uchunguzi huo, GST ilitoa taarifa kwa umma juu ya tukio hilo na kushauri wananchi waendelee na shughuli zao kwa kuwa tukio hilo halikuwa na uhusiano na mlipuko wa volkano.

Mheshimiwa Spika, uchunguzi mwingine ulihusu tukio la kububujika kwa tope lililokuwa likitoka ardhini katika Kijiji cha Mpinga, Wilaya ya Bahi, Mkoa wa Dodoma. Matokeo ya uchunguzi huo yalibainisha kuwa tukio hilo lilikuwa ni mabadiliko 65 ya jiolojia ambalo kitaalamu linajulikana kama liquefaction. Tukio hilo husababishwa na mabadiliko ya jiolojia ambayo husababisha kuwepo kwa msukumo au mgandamizo kwenye tabaka la udongo unaoweza kutokea kutokana na nguvu za asili kama vile matetemeko ya ardhi na kusababisha kuvurugika kwa uwiano uliopo kati ya chembechembe za udongo na maji yaliyopo kwenye nafasi wazi katikati ya udongo na hatimaye kutengenezwa kwa tope ambalo hububujika juu ya ardhi na siyo volkano kama ilivyodhaniwa kabla ya uchunguzi. (iv) Kuimarisha uwezo wa Taasisi na Kusogeza Huduma kwa Wananchi 

Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha utekelezaji wa majukumu yake, GST imefungua ofisi ndogo katika mkoa wa Geita kwa lengo la kusogeza huduma za taasisi karibu na wadau. Hatua hii ni ya kihistoria kwa kuwa GST haikuwahi kuwa na ofisi nje ya Dodoma tangu kuanzishwa kwake mwaka 1925. Ofisi zitaendelea kufunguliwa katika maeneo mengine kulingana na upatikanaji wa rasilimaliwatu na fedha. 66 Picha Na. 13: Mhe. Dkt. Doto M. Biteko (Mb.) Waziri wa Madini akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi na wadau mbalimbali katika uzinduzi wa ofisi za GST – Geita. 1

Mheshimiwa Spika, ili kuimarisha utekelezaji wa majukumu yake, GST imenunua mashine na vifaa vya maabara ikiwemo mashine kubwa ya kisasa ya kuzalisha vyungu vya kuyeyushia sampuli za dhahabu (crucibles). Mashine hiyo itaiwezesha GST kuwa mzalishaji mkubwa pekee wa vyungu hivyo Afrika Mashariki na Kati. Uzalishaji huo utakapoanza, GST itaongeza mapato yake kwa kuuza vyungu hivyo ndani na nje ya nchi. Picha Na. 14 inaonesha mashine ya kisasa ya utengenezaji wa vyungu hivyo. 67 Picha Na. 14: Mashine ya kisasa ya kutengeneza vyungu (crucibles) vya kuyeyushia sampuli za miamba na udongo. 

 Mheshimiwa Spika, GST imenunua tanuru kubwa la kisasa la uchunguzi wa sampuli za dhahabu lenye uwezo wa kuchunguza sampuli 50 kwa mkupuo mmoja na hivyo kuhudumia wateja wengi zaidi kwa muda mfupi. Picha Na. 15 ni tanuru lilionunuliwa kwa ajili ya kuyeyushia sampuli. Aidha, GST imenunua mashine mbalimbali za uchunguzi ikiwemo XRD kwa ajili ya uchunguzi wa sampuli za udongo, madini na madawa; na mashine aina ya magnetometer zinazotumika katika tafiti za madini ambazo zitaongeza uwezo wa taasisi kuwahudumia wadau wengi zaidi hasa wachimbaji 68 wadogo wa madini na kutatua changamoto za uchimbaji madini wa kubahatisha. Aidha, GST imenunua magari manne (4) mapya kwa ajili ya kuimarisha kazi za ugani. 

Mheshimiwa Spika, GST imetoa ushauri elekezi kwa kampuni ya uchimbaji wa kati wa madini ya dhahabu ya MMG iliyopo Mkoa wa Mara. Utafiti huo ulibaini uwepo wa mkondo unaobeba dhahabu. Pia, ushauri elekezi ulitolewa kwa wachimbaji wadogo wa eneo la Pemba Wilaya ya Mvomero. Matokeo ya utafiti huo yalibaini uwepo wa madini ya dhahabu. Picha Na. 15: Tanuru la kisasa la kufanyia uchunguzi wa sampuli za miamba na udongo. 69 (d) Taasisi ya Uhamasishaji Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali Madini, Mafuta na Gesi Asilia (TEITI) 

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza jukumu lake la msingi la kuhamasisha uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali madini, mafuta na gesi asilia, TEITI imeendelea kutoa kwa umma taarifa zake kwa kila mwaka. Tarehe 30 Juni, 2021, Kamati ya TEITI ilikamilisha na kuweka wazi kwa umma Ripoti ya 11 ya TEITI kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019. Pamoja na mambo mengine ripoti hii iliainisha mapato yaliyopokelewa na Serikali kiasi cha shilingi bilioni 623.2 na malipo ya kampuni kwa Serikali kiasi cha shilingi bilioni 626.1. Mapato hayo ni kutoka kwenye kampuni 41 zilizofanyiwa ulinganishi ambapo kampuni 22 zilikuwa za madini; kampuni 7 za gesi asilia na mafuta; na kampuni 12 ni zilizotoa huduma katika Sekta ya Madini, Mafuta na Gesi Asilia. 

 Mheshimiwa Spika, kati ya shilingi bilioni 623.2 ambazo Serikali ilikiri kupokea, asilimia 42.75 zilipokelewa na Tume ya Madini, asilimia 38.97 na Mamlaka ya Mapato Tanzania na asilimia 15.41 zilipokelewa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania. Kiasi kilichobaki sawa na asilimia 2.88 kilipokelewa na Mamlaka nyingine ambazo ni 70 Mamlaka za Serikali za Mitaa (asilimia 2.26), Msajili wa Hazina (asilimia 0.56) na Wakala wa Misitu (asilimia 0.06). 

Mheshimiwa Spika, tofauti kati ya malipo na mapato ni shilingi bilioni 2.97pungufu ya kiasi ambacho Serikali ilikiri kupokea kutoka kwa kampuni hizo. Tofauti hiyo ni asilimia 0.48 ikiwa ni chini ya asilimia 1 ya mapato hayo ambayo kwa mujibu wa Sheria ya TEITA, 2015 kiwango cha tofauti hiyo siyo lazima kufanyiwa ukaguzi na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). Hata hivyo, Kamati ya TEITI ina uwezo wa kisheria wa kufanya uamuzi kuwa ukaguzi wa tofauti hiyo ufanyike. 

Mheshimiwa Spika, ripoti hiyo pia iliweka wazi taarifa mbalimbali zikiwemo za uzalishaji na usafirishaji wa rasilimali madini, mafuta na gesi asilia; umiliki wa hisa; na taarifa za ushirikishwaji wa watanzania (Local Content). Taarifa hiyo ilibainisha kuwa Sekta ya Madini ilichangia asilimia 67.54, Sekta ya Mafuta na Gesi Asilia asilimia 28.43 na kampuni zilizotoa huduma kwenye Sekta ya Uziduaji asilimia 4.03 ya mapato ya Serikali kwa kampuni 41 zilizofanyiwa ulinganisho. Aidha, taarifa iliainisha thamani ya madini yaliyozalishwa katika 71 Mwaka wa Fedha 2018/2019 kuwa ni shilingi trilioni 4.7. Thamani hiyo ilikuwa ni ongezeko la asilimia 27 ikilinganishwa na shilingi trilioni 3.7 za Mwaka wa Fedha 2017/2018. Sehemu kubwa ya uzalishaji huo ilitokana na madini ya dhahabu ambayo yalikuwa ni asilimia 71.9 ya thamani ya madini yote yaliyozalishwa. 125. Mheshimiwa Spika, TEITI imebuni na kuanzisha njia mbadala ya kuhakikisha takwimu na taarifa zinawafikia wadau kiurahisi kupitia mfumo wa kieletroniki. Takwimu hizo huwekwa kupitia kwenye dashboard iliyopo katika tovuti ya TEITI kwa kutumia vielelezo mbalimbali ikiwemo chati na grafu. Hadi Julai, 2021, takwimu na taarifa zilizopo katika Ripoti ya 11 ya TEITI zimeingizwa katika mfumo huo ambao unapatikana kupitia https://www.teiti.go.tz/dashboard/. 126. Mheshimiwa Spika, TEITI imeendelea kuhamasisha na kuelimisha umma kuhusu matumizi ya takwimu zinazopatikana katika ripoti zake kwa njia mbalimbali ikiwemo maonesho, makongamano, warsha, mafunzo, semina, vyombo vya habari na mitandao ya kijamii. Uelimishaji huo umejenga uwezo wa taasisi na wananchi kwa ujumla kuhoji na kuhamasisha mijadala kuhusu manufaa 72 ya uchimbaji wa rasilimali madini, mafuta na gesi asilia. (e) Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) 

Mheshimiwa Spika, TGC hutoa mafunzo ya utambuzi, usanifu, ukataji na ung’arishaji wa madini ya vito. Mafunzo hayo ni ya muda mrefu katika fani za teknolojia ya madini na usonara (gem and jewellery technology) kwa ngazi ya Astashahada na Stashahada; na mafunzo ya muda mfupi katika fani za gemology, gem identification, synthetic and treated gem identification, coloured gem grading and pricing, diamond grading and pricing, lapidary, gem and rock carving and jewellery design and manufacturing. 128. Mheshimiwa Spika, TGC hutoa huduma za usanifu madini ya vito na miamba, huduma za maabara kwa madini ya vito na bidhaa za usonara na kutoa vyeti vya uthibitisho (Certificate of Authenticity). Aidha, TGC hutengeneza bidhaa za mapambo na urembo. Pia, TGC hutoa ushauri elekezi kwenye tafiti za uongezaji thamani madini na kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini nchini na matumizi ya bidhaa zinazotokana na madini ya vito. 73 

Mheshimiwa Spika, kuanzia Julai, 2021 hadi Machi, 2022, TGC imedahili wanafunzi 95 kwa mafunzo ya muda mrefu katika ngazi ya stashahada (NTA Level 4, NTA Level 5 na NTA Level 6) katika fani ya teknolojia ya madini na usonara. Aidha, wanafunzi 43 walidahiliwa kujiunga na mafunzo ya muda mfupi (miezi sita na mitatu) katika ngazi ya astashahada kwa fani za utambuzi wa madini, ukataji na usanifu madini ya vito. 130. Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha wanafunzi wanaosoma TGC wanapata elimu stahiki, TGC iliratibu mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi 73 katika fani ya teknolojia ya madini na usonara ambayo yalifanyika Arusha Gemological Laboratory na katika ofisi za madini za Mikoa ya Arusha, Dar es salaam, Shinyanga, Mirerani-Manyara. Aidha, wanafunzi wa fani ya ukataji na ung'arishaji wa madini ya vito walipatiwa mafunzo kwa vitendo katika kampuni zinazojishughulisha na uongezaji thamani madini ya vito kwenye miji ya Arusha, Dar es Salaam na Mirerani. 

Mheshimiwa Spika, pamoja na kutoa elimu na huduma za ushauri, TGC inazalisha na kuuza bidhaa mbalimbali zikiwemo vinyago, bidhaa za usonara kama vile vidani, key holders, mikufu, 74 bangili, pete, na vito vilivyokatwa. Bidhaa hizi zinapatikana kwenye ofisi za TGC zilizoko Arusha na kwenye mabanda ya TGC yanayokuwa kwenye maonesho mbalimbali. Aidha, TGC inatengeneza bidhaa hizo kwa mujibu wa mahitaji ya mteja. Ni wito wangu kwa watanzania wenzangu na taasisi za umma pale tunapohitaji bidhaa za zawadi au kumbukumbu (souvenir) kununua bidhaa zinazozalishwa na TGC. Baadhi ya bidhaa zinazozalishwa na TGC ni kama zinavyoonekana katika Picha Na. 16. Picha Na. 16: Baadhi ya bidhaa zinazozalishwa na kuuzwa na TGC. 

Mheshimiwa Spika, TGC imeendelea kujitangaza na kuhamasisha shughuli za uongezaji 75 thamani madini kwa kushiriki katika Maonesho ya Kitaifa na Kimataifa ya Sabasaba ya mwaka 2021 na SADC yaliyofanyika jijini Dar es Salaam, maonesho ya kuelekea kilele cha Sherehe za Uhuru wa Tanzania Bara yaliyofanyika Zanzibar na Mkutano wa Nne wa Uwekezaji katika Sekta ya Madini uliofanyika Dar es Salaam. Ushiriki huu umeongeza uelewa wa wadau kuhusu Kituo na shughuli za uongezaji thamani madini. Picha Na. 17: Mhe Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko alipotembelea banda la TGC wakati wa Maonesho ya Sabasaba - Dar es Salaam 2021. 76 D. 

MPANGO NA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2022/2023 

Mheshimiwa Spika, katika kuandaa Mpango na Bajeti wa Mwaka wa Fedha 2022/23, Wizara imezingatia miongozo mbalimbali ya kitaifa. Miongozo iliyozingatiwa ni pamoja na: Mwongozo wa Kitaifa wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti wa Mwaka 2022/2023; Ilani ya CCM kwa Ajili ya Uchaguzi wa Mwaka 2020; Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2021/22 – 2025/26; Sera ya Madini ya Mwaka 2009; Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025; Maelekezo ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na viongozi wengine wa kitaifa waliyoyatoa kwa nyakati tofauti; na Maelekezo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini yaliyotolewa kwa nyakati tofauti. I. Vipaumbele vya Wizara ya Madini kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Madini kwa mwaka 2022/2023 itatekeleza majukumu yake kwa kuzingatia vipaumbele vifuatavyo: kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli na kuongeza mchango wa 77 Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa; kuwaendeleza wachimbaji wadogo na kuwawezesha wananchi kushiriki katika uchumi wa madini; kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini; kuhamasisha biashara na uwekezaji katika Sekta ya Madini; kusimamia mfumo wa ukaguzi wa shughuli za migodi; kuzijengea uwezo taasisi zilizo chini ya Wizara ili ziweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi; na kuendeleza rasilimaliwatu na kuboresha mazingira ya kufanyia kazi. a) Kuimarisha Ukusanyaji wa Maduhuli na Kuongeza Mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa 

Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli ya Serikali, Wizara imepanga kutekeleza mikakati ifuatayo: kuimarisha udhibiti na usimamizi wa uchimbaji mkubwa na wa kati wa madini ili uweze kufaidisha Taifa na wawekezaji kwa usawa; kutekeleza mikakati itakayowezesha kudhibiti vitendo vya utoroshaji wa madini kwenda nje ya nchi na biashara haramu ya madini nchini; kuimarisha masoko ya madini nchini; na kuanzisha na kuimarisha soko la dhahabu la Kalema, Mkoa wa Katavi. 78 1

Mheshimiwa Spika, mikakati mingine itakayotekelezwa ni: kufungua na kusimamia migodi ya uchimbaji mkubwa na kuweka msisitizo katika uchimbaji wa madini ya kinywe (graphite) na madini mengine; kuendeleza na kuimarisha usimamizi wa madini ya ujenzi, soko la Tanzanite na vito vingine hapa nchini ili kuongeza mapato yatokanayo na madini hayo na madini mengine ya vito; kuhakikisha migodi yote mikubwa inaajiri watanzania na kununua huduma na bidhaa kutoka hapa nchini kwa kiwango cha kuridhisha kwa kadiri ya upatikanaji wake; na kutoa huduma za kijamii katika maeneo husika. 

Mheshimiwa Spika, kufuatia mikakati hiyo, Wizara, katika mwaka 2022/2023, inapanga kukusanya jumla ya shilingi bilioni 894.3. Kiasi hiki ni ongezeko la asilimia 22.12 ikilinganishwa na shilingi bilioni 696.4 zilizopangwa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022. Kati ya fedha zitakazokusanywa, shilingi bilioni 822.0, sawa na asilimia 91.9 zitakusanywa na kuwasilishwa Hazina na shilingi bilioni 72.3, sawa na asilimia 8.1 zitakusanywa na kutumika na Taasisi zilizo chini ya Wizara. 79 b) Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo na Kuwawezesha Wananchi Kushiriki katika Uchumi wa Madini 

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hiki, Wizara itafanya yafuatayo: kubuni na kuimarisha utekelezaji wa mipango ya kuwawezesha wachimbaji wadogo ili waweze kufanya shughuli zao kwa tija kwa kuwatengea maeneo au kuwapatia leseni kwenye maeneo ambayo yana taarifa za msingi za kijiolojia; kutoa huduma za utafiti kwa gharama nafuu; kuwaendeleza wachimbaji wadogo kuwa wa kati na hatimaye kuwa wachimbaji wakubwa; kuwapa mafunzo yanayohitajika kuhusu uchimbaji, uchenjuaji na biashara ya madini; kuzifuta leseni ambazo hazijaendelezwa kwa mujibu wa sheria na maeneo ya leseni hizo kutolewa kwa wachimbaji wengine, hususan wachimbaji wadogo; na kusimamia utekelezaji wa sheria inayoitaka migodi yote mikubwa kuajiri, kununua huduma na bidhaa kutoka hapa nchini na kuwasilisha mpango wa ushirikishwaji wa watanzania katika mnyororo wa uchumi wa Madini (Local Content). 80 c) Kuhamasisha Shughuli za Uongezaji Thamani Madini 139. Mheshimiwa Spika, katika kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani, Wizara itaendelea kuhamasisha ujenzi wa viwanda vya uchenjuaji, uyeyushaji, usafishaji na utengenezaji wa bidhaa za madini; na kusimamia na kuhamasisha uwekezaji katika shughuli za uongezaji thamani madini. d) Kuhamasisha Biashara na Uwekezaji katika Sekta ya Madini 

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hiki, Wizara itafanya yafuatayo: kuweka mazingira yatakayohamasisha uwekezaji katika Sekta ya Madini bila ya kuathiri ustawi na matarajio ya nchi kutokana na uwekezaji huo; kubuni na kutekeleza mikakati ya kuhamasisha uwekezaji katika Sekta ya Madini kwa kufanya tafiti za madini ya kimkakati, madini ya viwandani na madini ya metali; kujenga imani kwa biashara ya madini nchini kwenye uwanja wa kimataifa kwa kutekeleza wajibu wa nchi yetu kama mwanachama wa Extractive Industries Transparency Initiative (EITI); na kushiriki mikutano, maonesho ya madini na makongamano mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa lengo la 81 kutangaza fursa za uwekezaji zilizopo katika Sekta ya Madini. e) Kusimamia Mfumo wa Ukaguzi wa Shughuli za Migodi 

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hiki, Wizara itaimarisha kaguzi katika masuala ya afya, usalama na utunzaji wa mazingira kwa lengo la kudhibiti athari za kiafya, kiusalama na kimazingira zinazoweza kujitokeza katika shughuli za utafiti, uchimbaji na uchenjuaji wa madini. Aidha, Wizara itaendelea kuimarisha ukaguzi wa uzalishaji wa madini, hesabu za uwekezaji ikiwa ni kiasi cha mitaji na gharama za uendeshaji (Capex and Opex) pamoja na ulinganifu wa malipo ya kodi na tozo kwenye shughuli za madini ili kuhakikisha nchi inapata mapato stahiki. f) Kuzijengea uwezo Taasisi Zilizo Chini ya Wizara ili Ziweze Kutekeleza Majukumu yake kwa Ufanisi 

Mheshimiwa Spika, Wizara itatekeleza kipaumbele hiki kwa kufanya yafuatayo: kuendelea kuimarisha Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ili lishiriki kikamilifu kwenye shughuli za madini; 82 kuiimarisha Tume ya Madini ili iendelee kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi ikiwa ni pamoja na kukusanya maduhuli na takwimu za madini kwa lengo la kuongeza mapato ya Serikali; kuimarisha GST ili iendelee kufanya utafiti mkubwa wa shughuli za madini na kuendana na mabadiliko ya teknolojia; kuimarisha TGC ili iendelee kutoa mafunzo ya uongezaji thamani madini na kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini nchini; na kuiimarisha TEITI kwa lengo la kuendeleza uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji.

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hiki, Wizara itafanya yafuatayo: kuajiri watumishi wenye sifa na ujuzi unaostahili; kuboresha mazingira ya kufanyia kazi; kuwawezesha watumishi kupata mafunzo ya muda mrefu na mfupi; kuboresha maslahi na stahili za watumishi; kutoa elimu na vifaa kinga kwa ajili ya kuzuia maambukizi mapya ya VVU na kuwahudumia watumishi waliothibitika wanaishi na VVU waliojitokeza; kuendelea kutoa elimu, ushauri na huduma dhidi ya Magonjwa Sugu Yasiyoambukiza (MSY); kuendelea kukabiliana na janga la UVIKO 19; na kuendelea kutekeleza Mpango Mkakati wa Wizara dhidi ya Rushwa wa Mwaka 2017 - 2022. 83 II. Kazi Zitakazotekelezwa na Taasisi Zilizo Chini ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 (a) Tume ya Madini Kuimarisha Usimamizi wa Sekta ya Madini na Ukusanyaji wa Maduhuli ya Serikali 

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2022/2023, Tume itaendelea kuboresha ukusanyaji wa maduhuli yatokanayo na rasilimali madini nchini kwa kufanya yafuatayo: kusimamia uzalishaji wa madini ujenzi kwa kuhakikisha Mfumo wa Ukusanyaji wa Maduhuli yatokanayo na Madini (MiMS) unafanya kazi kikamilifu nchi nzima; kuongeza kasi ya utoaji wa leseni kwa kuimarisha mfumo wa utoaji na usimamizi wa leseni; kugawa maeneo yaliyotengwa kwa wachimbaji wadogo ili wafanye uzalishaji; kuendelea kufuta leseni zote zisizoendelezwa na zilizoisha muda wake ili maeneo hayo yatolewe kwa wachimbaji wengine; kuendelea kutatua migogoro katika maeneo mbalimbali; kuboresha huduma katika masoko ya madini nchini; kudhibiti mianya ya utoroshaji wa madini kwa kushirikiana na mamlaka nyingine za Serikali; na kuendelea kusajili mialo ya wachimbaji wadogo wa dhahabu nchini. 84 Kuimarisha Ufuatiliaji na Ukaguzi wa Usalama, Afya, Mazingira na Uzalishaji wa Madini kwa Wamiliki wa Leseni 

Mheshimiwa Spika, ili kuwa na uchimbaji madini salama, endelevu na unaozingatia utunzaji wa mazingira, Tume ya Madini itaendelea kufanya kaguzi za kimazingira ikiwa ni pamoja na ukaguzi wa miundombinu ya migodi kama vile mabwawa ya kuhifadhia topesumu, mashimo ya uchimbaji, maeneo ya kutunzia miambataka; maghala na stoo za kuhifadhia baruti, shughuli za ukarabati wa mazingira migodini, uchimbaji salama hususan kwa wachimbaji wadogo pamoja na ukaguzi wa mitambo ya uchenjuaji madini. Aidha, Tume itaendelea kusimamia utekelezaji wa mipango ya uendelezaji migodi na ufungaji migodi kwa wamiliki wa leseni kubwa na za kati; na kubuni miradi ya mfano ya uchimbaji madini salama na utunzaji wa mazingira kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Kuendelea Kuboresha Mazingira ya Kuwawezesha Wananchi Kufaidika na Rasilimali Madini 

Mheshimiwa Spika, Tume ya Madini itaendelea kutenga na kugawa maeneo kwa wachimbaji wadogo nchini, kusimamia 85 ushirikishwaji wa wananchi (Local Content) kwenye shughuli za madini kwa mujibu wa Sheria, kuhakikisha kampuni za uwekezaji katika Sekta ya Madini zinatumia malighafi zinazozalishwa nchini pamoja na huduma zinazotolewa na watanzania, na kusimamia utekelezaji wa miradi ya CSR. Kuelimisha Umma na Kuboresha Upatikanaji wa Taarifa Mbalimbali kwa Wadau wa Sekta ya Madini 

Mheshimiwa Spika, Tume ya Madini itaendelea kutoa taarifa na elimu kwa umma kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu Sekta ya Madini ikiwa ni pamoja na Sheria na Kanuni mbalimbali za usimamizi wa shughuli za utafutaji, uchimbaji, biashara ya madini, utunzaji wa mazingira na ulipaji wa kodi na tozo. Utoaji wa elimu husika na uhamasishaji utafanyika kupitia vyombo vya habari, semina, tovuti ya Tume ya Madini (www.tumemadini.go.tz), maonesho, makongamano pamoja na midahalo mbalimbali ndani na nje ya nchi. 86 Kuboresha Ushirikiano Kati ya Tume ya Madini na Wadau Mbalimbali katika Uendelezaji wa Sekta ya Madini 

Mheshimiwa Spika, ili kuimarisha ushirikiano na wadau wengine, Tume ya Madini itaendelea kuzihusisha mamlaka nyingine za Serikali zinazofungamana na sekta katika utekelezaji wa majukumu ikiwa ni pamoja na Baraza la Taifa la Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira (NEMC), Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Mamlaka za Serikali za Mitaa, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), Taasisi za Fedha, pamoja na wadau wengine wa ndani na nje ya nchi ili kuhakikisha changamoto mbalimbali zikiwemo za kisheria, mitaji, upatikanaji wa vibali, tozo na kodi ambazo zimekuwa zikiwakabili wachimbaji nchini zinatatuliwa kwa wakati na kwa maridhiano. Kuendeleza Rasilimaliwatu na Kuboresha Mazingira ya Kufanyia Kazi 

Mheshimiwa Spika, Tume ya Madini itaendelea kuimarisha utendaji kazi wake kwa lengo la kuisimamia ipasavyo Sekta ya Madini nchini kwa kuboresha mazingira na vitendea kazi na 87 kuwaongezea ujuzi na weledi watumishi kwa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na mrefu ili kuimarisha utendaji kazi wa Tume. (b) Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2022/2023, Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) inatarajia kutekeleza shughuli zifuatazo: Kufanya Tafiti za Jiosayansi na Kuboresha Kanzidata ya Taifa ya Taarifa za Miamba na Madini. 151. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hicho GST itafanya yafuatayo: utafiti wa jiolojia na jiokemia katika QDS mbili (2) mpya (203 na 204) zilizopo mikoa ya Pwani na Dar es Salaam; kuhuisha ramani katika QDS 175 (Njombe) na 176 (Ruvuma) katika skeli ya 1:100,000; kufanya tafiti maalum tano (5) za jiosayansi; tafiti tano (5) za kina kwenye madini ya viwandani, helium, vito, dhahabu na madini ya kimkakati kama vile nikeli (nickel) na kinywe (graphite); kutoa ushauri elekezi; kuhamisha mfumo wa utunzaji taarifa kutoka mfumo wa nakala mango kwenda tepe (digitization); kukusanya na 88 kufanya uchambuzi wa taarifa za utafutaji na uchimbaji madini nchini; kuhuisha kanzidata ya rasilimali madini zinazopatikana nchini na kitabu cha Madini Yapatikanayo Tanzania. Kuwaendeleza Wachimbaji Wadogo kwa Kufanya Tafiti za Jiosayansi 

Mheshimiwa Spika, katika kuwaendeleza wachimbaji wadogo na wa kati wa madini, GST itafanya utafiti wa jiosayansi na kutoa mafunzo kwa lengo la kutambua tabia za mbale katika maeneo mawili (2) ya wachimbaji wadogo yaliyopo Mikoa ya Morogoro na Iringa. Aidha, GST kwa kushirikiana na STAMICO, itafanya utafiti wa jiosayansi kwa lengo la kubaini uwepo wa madini katika eneo moja (1) lililotengwa kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Kuboresha Huduma za Maabara 

Mheshimiwa Spika, katika kuboresha huduma za maabara, GST itafanya yafuatayo: kufanya uchunguzi kwa kuzingatia matakwa ya ithibati (accreditation); kuboresha maabara ya Geita na kuanzisha maabara Chunya kwa lengo la kusogeza huduma karibu na wachimbaji na watafutaji wa madini; kutengeneza vyungu vya 89 kuyeyushia sampuli (crucibles) 300,000 na cupels 50,000 kwa ajili ya kuyeyusha dhahabu; kufanya uchunguzi wa sampuli za udongo, miamba au madini 17,000; kuandaa sampuli rejea (reference materials) za dhahabu, shaba, silver, zinki, chuma na cobalt; na kufanya ukarabati wa mashine ya kupimia sampuli (Induced Coupled Plasma - ICP). Kuratibu Taarifa za Majanga ya Asili ya Jiolojia na Kuelimisha Wananchi Namna Bora ya Kujikinga nayo 

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na majanga ya asili ya jiolojia kama vile matetemeko ya ardhi, maporomoko ya ardhi, na milipuko ya volkano, GST inakusudia kufanya mambo yafuatayo: kukusanya takwimu kutoka vituo vitano (5) vya kudumu vya kupimia matetemeko ya ardhi vilivyoko Arusha, Dodoma, Geita, Mtwara na Mbeya ili kujua matukio mbalimbali ya mitetemo; kuchakata takwimu zilizokusanywa kutoka katika vituo hivyo na kuhuisha ramani inayoonesha vitovu vya matetemeko ya ardhi nchini; kuunganisha vituo viwili (2) vya kupimia mitetemo vilivyopo Dodoma na Arusha katika mfumo mubashara (real time); kutoa elimu kwa Umma juu ya namna bora ya kujikinga au kupunguza athari za majanga ya asili ya jiolojia; na 90 kusimika kituo kimoja kipya mkoani Kigoma cha kuratibu ukanda wa Bonde la Ufa Mkondo wa Magharibi. Kuimarisha Uwezo wa Taasisi katika Kutoa Huduma 

Mheshimiwa Spika, ili kuimarisha uwezo wa Taasisi katika kutoa huduma, GST inakusudia kufanya yafuatayo: kuboresha mifumo ya uchakataji, uhifadhi na usambazaji wa taarifa za jiosayansi kuhusu upatikanaji wa madini; kuwawezesha watumishi kupata mafunzo ya muda mfupi na mrefu; kuboresha mazingira ya utendaji kazi na maslahi ya watumishi; kutangaza (marketing) bidhaa na huduma zitolewazo na GST; na kukamilisha kufanya mapitio na maboresho ya Muundo wa Taasisi ili kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu ya GST. (c) Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2022/2023, STAMICO inatarajia kutekeleza vipaumbele vifuatavyo: 91 Kuongeza Ukusanyaji wa Mapato ya Ndani ya Shirika hadi Kufikia Shilingi Bilioni 70 

Mheshimiwa Spika, ili kufikia lengo hilo shirika litatekeleza kazi zifuatazo: kuendelea kutangaza huduma za uchorongaji zinazofaywa na shirika; kuanza uzalishaji wa kibiashara katika mradi wa makaa ya mawe ya kupikia (coal briquettes); kuendelea na mradi wa kuuza vilipuzi na kemikali za madini; na kusimamia miradi ya uwekezaji. Kuendelea na Uzalishaji Mkubwa katika Eneo la Kabulo-Kiwira 158. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hicho, shirika litafanya kazi zifuatazo: kukamilisha ukarabati wa miundombinu ya migodi ikiwemo reli na barabara; kununua vifaa vya uchimbaji ili kuongeza ufanisi wa mradi; kufanya utafiti ili kuongeza mashapo yanayotarajiwa kuchimbwa; pamoja na kutafuta masoko makubwa ndani na nje ya nchi. 92 Kuendeleza na Kuongeza Uzalishaji wa Makaa ya Kupikia (Coal briquettes) 

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hicho, shirika litafanya kazi zifuatazo: kuanza uzalishaji kwa kutumia mitambo miwili mikubwa yenye uwezo wa kuzalisha tani 20 kwa saa itakayosimikwa Pwani na Kabulo; na kununua mitambo miwili mingine mikubwa yenye uwezo wa kuzalisha tani 20 kwa saa kwa kila mtambo ambapo mmoja utasimikwa Dodoma kwa ajili ya kanda ya kati na mwingine utasimikwa katika eneo litakaloonekana lina uhitaji wa nishati hiyo; na kufanya kampeni ya uhamasishaji wa matumizi ya nishati hiyo. Kuimarisha Shughuli za Uchorongaji 

 Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hicho, shirika litafanya kazi zifuatazo: kuendelea kuzitangaza shughuli za uchorongaji zinazofanywa na shirika; kutafuta kandarasi nyingine mpya; na kununua mitambo ya uchorongaji (rigs), magari saidizi (supporting vehicle), low bed vehicle, magari manne (4) na water bowser. 93 Kuratibu Shughuli za Uchimbaji Mdogo na Kuimarisha Vituo vya Mfano 

 Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hicho, shirika litafanya kazi zifuatazo: kuendelea kutekeleza mkakati wa kuendeleza uchimbaji mdogo nchini pamoja na mpango wa mafunzo kwa wachimbaji wadogo nchi nzima; kununua mitambo mitano (5) ya uchorongaji maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo (Shallow Holes Drilling Rigs – DD/RC 0-100 Meters); kuongeza uwezo wa vituo vya mfano vilivyopo Lwamgasa, Katente na Itumbi kwa kuimarisha miundombinu iliyopo; kuanza ujenzi wa vituo viwili vipya vya mfano katika Mkoa wa Tanga (chokaa) na Lindi (chumvi); na kuwasaida wachimbaji wadogo kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha. Kuendeleza Mali na Leseni za Shirika 

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hicho, shirika litafanya kazi zifuatazo: kuendeleza leseni za madini mbalimbali zinazomilikiwa na shirika; na kuanzisha mgodi wa kuchimba dhahabu wa Kigosi kwa kuanza uchorongaji na utafiti kwa ajili ya kuhakiki mashapo yaliyopo. 94 Kuendelea Kutoa Elimu Juu ya Afya na Utawala Bora 

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hicho, shirika litafanya kazi zifuatazo: Kutoa mafunzo mbalimbali kwa watumishi juu ya maambukizi ya VVU, UVIKO - 19 pamoja na Magonjwa Sugu Yasiyoambikiza; kutoa huduma za lishe kwa wafanyakazi wenye maambukizi ya VVU; kutoa elimu katika masuala ya rushwa, maadili na utawala bora kwa watumishi; na kuandaa michezo mbalimbali ili kuhamasisha wafanyakazi kujijengea afya bora. Kuboresha Mazingira ya Kazi kwa Watumishi 164. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kipaumbele hicho, shirika litafanya kazi zifuatazo: kulipa madeni ya wafanyakazi; kutoa mafunzo ya muda mrefu na mfupi; kuwapatia watumishi vitendea kazi; na kujenga jengo la ofisi ya shirika Dodoma. 95 (d) Taasisi ya Uhamasishaji Uwazi na Uwajibikaji katika Rasilimali Madini, Mafuta na Gesi Asilia (TEITI) 

Mheshimiwa Spika, kazi zitakazotekelezwa na TEITI katika mwaka 2022/2023 ni kama ifuatavyo: kukamilisha na kutoa kwa umma ripoti ya malipo ya kodi na tozo yaliyofanywa na Kampuni za Madini, Mafuta na Gesi Asilia kwa Serikali kwa kipindi cha Mwaka wa Fedha 2020/2021; kuendelea kuelimisha umma juu ya matumizi ya takwimu zinazotolewa kwenye ripoti za TEITI ili kuhoji uwajibikaji wa Serikali; kuendelea kuelimisha kampuni za madini, mafuta na gesi asilia juu ya majukumu yao ya kuweka wazi majina ya wamiliki wa hisa kwa ajili ya kuanzisha Rejista ya Taarifa; kujumuisha taarifa za wachimbaji wadogo na fidia zilizolipwa kutokana na athari za mazingira katika ripoti za TEITI; na kuendelea kutekeleza vigezo vya EITI vya kuweka wazi mikataba (Contract Disclosure) na kuandaa Rejista ya uwekaji wazi wa majina ya wamiliki wa hisa katika kampuni za madini, mafuta na gesi asilia (beneficial ownership disclosure). 96 (e) Kituo cha Jemolojia Tanzania (TGC) 

Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2022/2023, Kituo cha Jemolojia Tanzania kinatarajia kutekeleza kazi zifuatazo: (i) Kuendelea kutoa mafunzo 

Mheshimiwa Spika, TGC katika kutekeleza kipaumbele hicho itafanya yafuatayo: kuendelea kutoa mafunzo ya ngazi ya stashahada katika teknolojia ya vito na usonara (Gem and Jewellery Technology); kuanzisha mafunzo ya astashada ngazi ya VETA katika fani za ukataji, ung’arishaji madini ya vito na uchongaji vinyago; kutoa mafunzo ya muda mfupi (mwezi 1 hadi 6) katika fani za utambuzi wa madini ya vito, usonara, utengenezaji wa vinyago vya miamba na vito na usanifu madini ya vito; itahamasisha kuhusu uongezaji thamani madini ya vito katika shule za msingi na sekondari; kuanzisha karakana za uchakataji madini; kutoa semina elekezi mbalimbali ikiwemo kujikinga na maambukizi ya VVU na magonjwa Yasiyoambukizwa kwa watumishi na wanafunzi na kuzuia vitendo vya rushwa na ufisadi kwa watumishi na wanafunzi. 97 (ii)Uzalishaji wa bidhaa 

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Mwaka wa Fedha 2022/2023, Kituo kimepanga kuongeza uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zitokanazo na madini ya vito na miamba zikiwemo vinyago, mikufu, hereni na bidhaa nyingine za urembo na mapambo zitokanazo na rasilimali madini. (iii) Kuimarisha Shughuli za TGC 

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2022/2023, TGC imetengewa fedha za maendeleo kwa ajili ya mradi wa upanuzi wa miundombinu mbalimbali ya kutolea mafunzo ikiwemo karakana za mafunzo na uchakataji madini, madarasa, maabara za madini ya vito na bidhaa za usonara, maktaba, mabweni na kantini. Kituo pia, kimepanga kufanya ununuzi wa magari manne (4), mitambo ya kuchakata madini na vifaa mbalimbali kwa ajili ya mafunzo. Aidha, Kituo kimepanga kuendelea kuwajengea uwezo watumishi kwa kuwapeleka kwenye mafunzo ya muda mrefu na mfupi ndani na nje ya nchi hususan katika nchi zilizobobea kwenye teknolojia za uongezaji thamani madini zikiwemo Thailand, India, Sri Lanka, Marekani na China. 

Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa nipende kukiri kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imeonesha juhudi kubwa katika kuhakikisha kuwa uchumi wa nchi yetu unaimarika. Ni imani yangu kuwa kwa kasi kubwa ya utendaji kazi anayoendelea nayo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, nchi yetu itaendelea kupiga hatua katika kuimarisha ustawi wa kila mtanzania na taifa kwa ujumla. 

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kumshukuru Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, kwa maelekezo na miongozo mbalimbali katika kusimamia utendaji wa shughuli mbalimbali kwa manufaa ya watanzania wote. Aidha, nimshukuru Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb.) kwa hotuba yake nzuri ya bajeti ambayo imetoa mwelekeo wa shughuli za Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023. 

Mheshimiwa Spika, kipekee nitumie fursa hii kumshukuru Naibu Waziri wa Madini, Mheshimiwa Dkt. Steven Lemomo Kiruswa (Mb.) kwa namna 99 anavyonipa ushirikiano katika kusimamia Sekta ya Madini. Amekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kuwa Sekta ya Madini inakuwa na tija. 

Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa niwashukuru Bw. Adolf Hyasinth Ndunguru, Katibu Mkuu, na Bw. Msafiri Lameck Mbibo, Naibu Katibu Mkuu kwa namna wanavyosimamia vyema utekelezaji wa majukumu ya Wizara. Aidha, niwashukuru Dkt. Abdulrahman Shabani Mwanga, Kamishna wa Madini, Profesa Idris Suleiman Kikula, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Justinian Rwezaula Ikingura, Mwenyekiti wa Bodi ya GST, Meja Jenerali (Mstaafu) Michael Wambura Isamuhyo, Mwenyekiti wa Bodi ya STAMICO, Dkt. George Mofulu, Mwenyekiti wa Bodi ya TGC, Makamishna wa Tume ya Madini na wajumbe wa Bodi zote kwa kusimamia kwa umakini na weledi uendeshaji wa Sekta ya Madini. 

Mheshimiwa Spika, vilevile, niwashukuru Wakuu wa Taasisi, Wakurugenzi wa Idara, Wakuu wa Vitengo, pamoja na Wafanyakazi wote wa Wizara na Taasisi zake kwa ushirikiano mkubwa wanaonipa na kwa kujituma bila kusukumwa katika kutekeleza majukumu ya Wizara ya Madini jambo linaloifanya Sekta ya Madini izidi kuimarika na kustawi. 100 

Mheshimiwa Spika, niwashukuru pia wadau wa Sekta ya Madini wakiwemo watafutaji, wachimbaji, wenye mitambo ya uchenjuaji pamoja na wafanyabiashara wa madini kwa kuendelea kutekeleza shughuli zao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi. Utekelezaji wa shughuli zao kwa mujibu wa sheria unarahisisha usimamizi wa shughuli hizo. Aidha, nizishukuru Taasisi za Fedha hususan mabenki kwa kuendelea kuwapa mikopo wachimbaji, vyombo vya ulinzi na usalama kwa kutuhakikishia usalama kwenye maeneo yenye shughuli za madini bila kusahau vyombo vyote vya habari kwa ushirikiano waliotupatia katika kuitangaza Sekta ya Madini. 

Mheshimiwa Spika, shukrani zangu za pekee na za dhati naomba nizitoe kwa mara nyingine tena kwa wananchi wema wa Bukombe ambao kwa muda wote wameendelea kunivumilia na kunitia moyo katika kutekeleza majukumu yangu ya kitaifa kama Waziri. Aidha, niwashukuru kwa ushirikiano wanaonipatia katika kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo ya Jimbo. Naomba niwahakikishie kuwa nitazidi kuwatumikia kwa uaminifu na kasi zaidi kwa kadri Mwenyezi Mungu atakavyonijalia. 101 

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nichukue fursa hii kumshukuru kwa dhati mke wangu mpendwa Benadetha Clement Mathayo pamoja na watoto wangu wapendwa Elshadai, Elvin, Elis, Abigael, Amon, Abishai na Moses kwa kunivumilia, kuniombea kwa dhati kwa Mwenyezi Mungu, na kuniunga mkono katika utekelezaji wa majukumu yangu ya ubunge na uwaziri katika kujenga na kutetea maslahi ya Taifa letu. 

                                                     HITIMISHO 

Mheshimiwa Spika, ili Wizara iweze kutekeleza majukumu na malengo yaliyopangwa, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu liridhie na kupitisha makadirio ya shilingi 83,445,260,000.0 kwa ajili ya matumizi ya Wizara na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 kwa mchanganuo ufuatao:- (i) Shilingi 22,000,000,000.0 ikiwa ni fedha za maendeleo; na (ii) Shilingi 61,445,260,000.0 kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida. Kati ya fedha hizo, shilingi 20,609,600,000.0 ni kwa ajili ya Mishahara na shilingi 40,835,660,000.0 ni Matumizi Mengineyo. 

 Mheshimiwa Spika, kwa mara nyingine naomba nitoe shukrani zangu za dhati kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwa kunisikiliza. Majedwali na vielelezo mbalimbali kwa ajili ya kutoa ufafanuzi wa masuala na takwimu muhimu kuhusu Sekta ya Madini vimeambatishwa pamoja na hotuba hii. Aidha, hotuba hii inapatikana katika tovuti ya Wizara ya Madini kwa anuani ya www.madini.go.tz. 180. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

Share To:

Post A Comment: