Kilimo kimekuwa uti wa mgogo wa uchumi wa Tanzania tangu uhuru, ambapo kinaajiri na kutoa mchango mkubwa kwa Pato Ghafi la Taifa. Kwa kuzingatia suala hili, KILIFAIR Promotion, taasisi inayoongoza katika kuandaa maonesho ya biashara ya kimataifa nchini, inazindua maonesho ya Kimataifa ya Kilimo yatakayojulikana kama “TANZFOOD Expo”, yatakayofanyika katika Viwanja vya Magereza, Arusha kuanzia Ijumaa ya tarehe 11 Machi hadi Jumapili ya tarehe 13, ambapo maonesho yatakuwa wazi kuanzia saa 4 asubuhi hadi saa 11 kila siku.


Hafla ya ufunguzi wa TANZFOOD itazinduliwa rasmi na Waziri wa Kilimo, Mh. Hussein Bashe pamoja na Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania, Bi. Regine Hess saa 5 asubuhi siku ya Ijumaa ya tarehe 11 Machi. Wageni wengine maalumu katika maonesho hayo ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Dkt. John Mongella. 

Maonesho hayo yatawaleta pamoja zaidi ya makampuni 120 kutoka Tanzania na nchi jirani za Afrika Mashariki. Maonesho hayo yatashirikiana na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), GIZ, TAHA na wadau wengine muhimu wenye dhamira ya kuendeleza sekta ya Kilimo nchini Tanzania.

“Tunaelewa kwamba sekta hii si tu kwa ajili ya Taifa letu la Tanzania bali inalisha nchi nyingine nyingi za Kusini mwa Jangwa la Sahara. Hii ndiyo sababu tuliamua kuwekeza katika maonesho yenye viwango vya kimataifa ili kwamba tujivunie vya kutosha na kuonesha “Ladha ya Tanzania” kama kibwagiz cha maonesho huyo kinavyosema,” alisema Dominic Shoo, mmoja wa Wakurugenzi wa KILIFAIR Promotion. 

“Na sisi tunafurahi kuona mwitikio wa waoneshaji kutoka ndani ya Tanzania na masoko mengine. Maonesho haya si tu yataonesha bidhaa, bali itawaleta wataalamu mbalimbali wa Sekta ya Kilimo ili kutoa ujuzi wao kamilifu kwa makampuni yanayoshiriki na wakulima watakaofika katika maonesho haya,” alisema Mkurugenzi wa KILIFAIR Tom Kunkler, akiongeza: “Tumeanzisha Semina na Warsha ili kuwaelimisha wakulima kuhusu kuongeza ubora na maendeleo katika sekta hii.”

Tukio hili la siku tatu litagawanyika katika siku za wanafanya biashara (B2B) ambayo itakuwa Ijumaa na kwa kiasi fulani Jumamosi na siku za watumiaji/familia katika siku za Jumamosi na Jumapili. Katika kipindi chote hiki, wageni watatumia kujenga mtandao wa kibiashara katika mazingira rafiki ya kitaalamu, kufurahia burudani kutoka kwa wasanii wa hapa nchini na aina anuwai za vyakula vya kitanzania.

Bw. Antony Chamanga, Meneja Mkuu wa Maendeleo wa TAHA alieleza furaha yao kuwa sehemu ya maonesho kama hayo yanayoonesha hali ya ubora na ladha ya vyakula vya Kitanzania. “Sisi tuna wakulima 19,700 ambao ni wanachama wa TAHA na wanazalisha bidhaa za mbogamboga zenye ubora wa juu zinazokidhi viwango vya masoko ya kimataifa. Kwa hiyo, tunafurahi kwamba wanachama wetu watakaohudhudia maonesho haya, watoana fursa tele zilizopo katika sekta ya kilimo na jinsi gani ushiriki wao katika setka hii unavyoweza kusaidia kupeperusha bendera ya Taifa katika masoko ya kimataifa,” alisema Antony.

Miongoni mwa washirika na wadhamini wengine wa maonesho haya ni Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na GIZ ambao wamewekeza kiasi kikubwa sana katika kuwajengea uwezo wakulima wa hapa nchini na wadau wengine wa kilimo kwa kuwapatia fursa rahisi katika sekta hiyo kupitia upatikanaji wa fedha zinazohitajika ili kuwawezesha kunufaika na fursa mbalimbali za kilimo. 

Mdhamini mwingine wa kimkakati ni Benki ya CRDB, ambayo imekuwa na dhamira ya dhati kuhakikisha wakulima wadogo wanapata msaada wa kifedha na kujumuishwa, ambavyo wanahitaji vyote hivi ili kuchangia katika kuleta usalama wa chakula na kuimarisha ubora wa maisha ya Watanzania. Wadhamini wengine ni pamoja na Bakhresa Group (AZAM), Coca Cola, Pepsi Cola, BLINK WIFI na kundi la HARSHO miongoni mwa makampuni mengi maarufu.

Maonesho haya ya kila mwaka yatawaleta pamoja wadau wa kilimo wanaotoka katika sekta mbalimbali zinazohusiana na kilimo na kuangazia maeneo mbalimbal kwa ubunifu katika kilimo, ufungashaji na usindikaji, mbegu bora, pembejeo za kilimo, viuatilifu na kemikali. Vilevile kutakuwa na maeneo maalumu kwa ajili ya semina & warsha ili kutoa elimu na kuongeza ujuzi kwa wakulima katika siku hizo zote tatu za maonesho. Na tukio hilo pia litarushwa moja kwa moja kupitia vyombo mbalimbali vya habari, vituo vya runinga, redio na kurasa rasmi za kijamii za TANZFOOD Expo. 


Share To:

Post A Comment: