Klabu ya waandishi wa habari mkoa wa Manyara imefanikiwa kutoa elimu ya Afya ya Uzazi kwa Wanawake na Wasichana zaidi ya 122 katika mradi walioutekeleza kwa muda wa miezi sita.

Hayo yamesemwa na Mratibu wa mradi wa Haki ya afya ya uzazi unaofadhiliwa na shirika lisilo la kiserikali la Women Fund Tanzania (WFT) Jaliwason Jasson wakati akizungumza na waandishi wa Habari  Mjini Babati ambapo amesema Katika mradi huo wamekuwa wakitoa elimu kwa wanawake na wasichana kwa kushirikiana na wataalamu katika wilaya mbili za Hanang katika kata ya Endasaki na Hamashauri za wilaya ya Babati katika Kata ya Riroda na Halmashauri ya mji wa Babati kata ya Sigino.

Amesema Wanawake na Wasichana wanapitia changamoto nyingi za afya ya uzazi lakini pia vitendo vya ukatili ambavyo wamekuwa wakikutana navyo, ndio maana walichagua kipengele cha haki ya afya ya uzazi ili kuweza kukutana na makundi hayo ambapo tangu wameanza mradi huo wa miezi sita tangu mwezi Julai na kufikia tamati Desemba 2021 wamebaini kuwa changamoto kubwa iliyoko ni katika kupanga uzazi.

"Wengine hawaelewi wafanyaje, wengine wamekuwa wakichukua elimu ya mitaani ambapo wamekuwa wakienda kwenye maduka ya madawa na kupewa dawa za kupanga uzazi wa mpango bila kufuata wataalamu"alisema Jasson

Mpaka Desemba mwaka 2021 jumla ya wanawake 122 wamefikiwa na kupatiwa elimu ya afya ya uzazi na mpango wa Klabu ya waandishi wa Habari mkoa wa Manyara kwa ufadhili wa Women Fund Tanzania.

Jasson amesema katika wanawake hao kila mmoja amefundishwa kuwa balozi kwenda kutoa elimu kwa wanawake wengine watatu ambapo watafikiwa zaidi ya wanawake 360.

Kwa upande mwingine ameishukuru Women Fund Tanzania kwa ufadhili  ambao umedumu kwa kipindi cha miezi sita huku akiomba wawasaidie tena kwa awamu nyingine ili kupanua wigo zaidi katika kata nyingine na kuisaidia jamii.

Baadhi ya Wanawake na wasichana waliopatiwa elimu hiyo katika kijiji cha Singu kata ya Sigino wamesema imewagusa na kwamba watakwenda kuwaelimisha wengine.

Share To:

Post A Comment: