Jane Edward, Arusha


Waziri wa maliasili na utalii Dkt Damas Ndumbaro ametoa wito kwa vijana na watanzania kwa ujumla kujitokeza katika zoezi la kupanda mlima Kilimanjaro katika kusherehekea miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania.


Waziri Ndumbaro ameyasema hayo jijini Arusha wakati Akizungumza na waandishi wa habari juu ya maandalizi ya kupanda mlima huo.


Amebainisha kuwa katika kusherehekea miaka 60  ya uhuru wa Tanzania, njia itakayotumika ni kupanda mlima Kilimanjaro ambapo zaidi ya watu mia tatu wanatarajiwa kupanda mlima huo.


"Mpaka sasa watu waliothibitisha ni zaidi ya watu mia moja na hivyo idadi ya watu mia tatu ikikamilika zoezi litaanza mara moja" Alisema


Aidha ameendelea kusisitiza kuwa wananchi wanatakiwa kujipanga kushiriki zoezi hilo kwa kuendelea kujinoa kwakuwa matarajio ni wote kufika kilele cha mlima Kilimanjaro ili kuweza kufikia lengo.


Amefafanua kuwa katika kupanda mlima huo hakutahusisha wageni kutoka nje ya nchi kwakuwa lengo ni kusherehekea miaka 60 ya uhuru wa nchi ya Tanzania kwa kufanya zoezi hilo.


"Nawakumbusha wageni kutoka nje ya nchi ya kuwa Mlima huu upo hapa Tanzania pekee na sio sehemu nyingine ingawa wapo wapotoshaji wanaodai mlima huu haupo Tanzania,mimi nawatoa hofu Mlima Kilimanjaro upo Tanzania pekee Duniani" Alisema Dkt Ndumbaro


Kwa upande wake msanii wa vichekesho maarufu kama Mzee Shayo amesema kupitia zoezi hilo la upandaji Mlima Kilimanjaro watanzania wazawa watumie fursa hiyo ya kupanda mlima Kilimanjaro ili kuweza kujivunia rasilimali zilizopo hapa nchini.


Hata hivyo sherehe hizo za miaka 60 ya uhuru zitafanyika kuanzia tar 5 disemba mpaka tarehe 9 disemba 2021 na kuwataka wananchi kuwasiliana na kampuni ya Zara tours ya Utalii ili kuweza kufanya usajili wa kushiriki zoezi hilo.


Share To:

Post A Comment: