Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza uchaguzi kwenye kata mbili mpya na kuahirisha uchaguzi wa kata nyingine nne. Mabadiliko hayo yanafanya jumla ya kata zenye uchaguzi kuwa 77 badala ya 79 zilizotangazwa awali.

Akizungumza  jana Julai 10, Jijini Dar es Salaam  Mwenyekiti wa NEC, Jaji  Semistocles Kaijage amezitaja kata hizo mpya kuwa ni Kelamfua  ya Halmashauri ya Wilaya ya Rombo na Kata ya Kitaya,  Halmashauri ya Wilaya ya Nanyamba.

“Kwa mujibu wa Kifungu cha 13 (1) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa aliitaarifu Tume uwepo wa nafasi wazi za Madiwani katika Kata ya Kelamfua iliyoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Rombo na Kata ya Kitaya iliyoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Nanyamba,” alisema Jaji Kaijage.

Jaji Kaijage alisema kwamba nafasi zote mbili za Udiwani zimetokana na kujiuzulu kwa madiwani waliokuwa wamechaguliwa awali.

Alisema uteuzi wa wagombea udiwani utafanyika Julai 16 na  kampeni zitaanza  Julai 17 mpaka 11 Agosti na siku ya kupiga kura ni  Agosti 12.

Jaji Kaijage amevialika vyama vya siasa, wadau wote wa uchaguzi na wananchi kwa ujumla kushiriki uchaguzi huo.

Katika hatua nyingine Jaji Kaijage ametangaza kuahirishwa kwa uteuzi wa wagombea kwenye kata tatu za Tindabuligi, Kisesa, Katumba na Mlimba.

Tume itatangaza hapo baadae tarehe nyingine za uteuzi na uchaguzi katika kata hizo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: