Articles by "WABUNGEMAJIMBONI"
Showing posts with label WABUNGEMAJIMBONI. Show all posts

 

MBUNGE Viti Maalum Mkoa wa Pwani Mariam Ibrahim, amechangia Sh. milioni tano kwa ajili ya ujenzi wa Shule Mpya ya Msingi Kisutu iliyopo Jimbo la Bagamoyo mkoani humo. 

Ametoa mchango huo wakati aliposhiriki katika  tukio la upandaji wa miti 300 lililofanyika katika eneo la shule hiyo.
Akizungumza na wananchi, Mbunge Mariam amesema mchango huo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi kubwa zinazofanywa na wananchi pamoja na wadau mbalimbali katika kuhakikisha shule hiyo inakamilika. 

Pia amempongeza Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo CPA Subira  Mgalu, kwa juhudi zake za kusimamia maendeleo ya elimu na kuendelea kushirikiana na wananchi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Aidha, amempongeza  Diwani wa Kata ya Kisutu Awesu Muhidini, kwa uongozi wake na namna anavyoshirikiana na wananchi kuipambania shule hiyo hadi kufikia hatua ya sasa.

Mbunge Mariam pia amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuwezesha upatikanaji wa eneo lililojengwa shule hiyo, hatua ambayo imefungua fursa ya kuboresha huduma za elimu kwa watoto wa Kata ya Kisutu.

Katika hafla hiyo,amekabidhi sh. milioni 3 papo hapo, huku akiahidi kuwa Sh. milioni mbili zilizobaki atazikabidhi kupitia Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo CPA Mgalu, ili kukamilisha ahadi yake ya mchango wa Sh.Milioni 5.



Na Mwandishi Wetu

IRINGA – Mbunge wa Jimbo la Ismani, Mhe. Emmanuela Mtatifikolo, amezindua rasmi maonesho na sherehe za Sabasaba zinazofanyika katika Kata ya Ilolo Mpya, Tarafa ya Pawaga, wilayani Ismani, huku akiwataka wananchi kutumia maonesho hayo kujifunza, kufanya biashara na kuimarisha mshikamano wa kijamii.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Mtatifikolo alisema maonesho ya Sabasaba ni fursa muhimu kwa wananchi kukutana, kubadilishana uzoefu, kuuza na kununua bidhaa mbalimbali pamoja na kujifunza fursa za maendeleo kutoka kwa washiriki na wageni wanaotoka maeneo mbalimbali nchini.

Aliwahamasisha wananchi wa Kata ya Ilolo Mpya na Jimbo la Ismani kwa ujumla kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo, akieleza kuwa mbali na burudani, maonesho hayo yana mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa wananchi na kuimarisha mahusiano ya kijamii.

"Mnatakiwa kutumia maonesho haya kama jukwaa la kujifunza, kufanya biashara na kujenga mahusiano yatakayochochea maendeleo ya Ismani na wananchi wake," alisema Mtatifikolo.

Mbunge huyo pia aliwataka vijana kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuhatarisha amani na utulivu wa nchi, akisisitiza kuwa maendeleo hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mazingira ya amani.
Aidha, aliwahimiza wazazi na walezi kuendelea kuwalea watoto katika misingi ya maadili, uzalendo na uwajibikaji ili kujenga kizazi kitakachochangia maendeleo ya taifa.

"Malezi bora ndiyo msingi wa kujenga taifa lenye vijana wenye nidhamu, uzalendo na uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi," alisisitiza.

Maonesho hayo ya Sabasaba yanajumuisha shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, zikiwemo maonesho ya bidhaa, michezo ya mpira wa miguu, ngoma za asili pamoja na burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali.
Waandaaji wa maonesho hayo wamesema lengo ni kutoa fursa kwa wananchi kuonesha bidhaa na huduma zao, kuhamasisha biashara ndogondogo na kukuza vipaji vya vijana kupitia michezo na sanaa.

Sherehe hizo hufanyika kila mwaka baada ya wananchi kumaliza shughuli za uvunaji, zikiwa sehemu ya kuimarisha mshikamano wa jamii, kuchochea biashara na kutoa burudani kwa wakazi wa Ismani na maeneo jirani.

Wananchi waliohudhuria uzinduzi huo walieleza kufurahishwa na maandalizi ya maonesho hayo, wakisema yameendelea kuwa kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Jimbo la Ismani.

 


 Mbunge wa Jimbo la Hanang Mkoani Manyara ambaye pia ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Mhe. Asia Halamga, amekabidhi mifuko ya mbegu za dengu kwa viongozi na wananchi mbalimbali wilayani Hanang  ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha sekta ya kilimo na kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza katika hafla ya ugawaji wa mbegu hizo Mbunge huyo amesema kuwa lengo la kutoa mbegu hizo ni kuongeza tija kwa wakulima na kuinua kipato chao kupitia kilimo cha kisasa hususani baada ya mvua nyingi za mwaka huu kuharibu mazao ya maharage shambani

Asia ameendelea kueleza kuwa  kuwa utoaji wa mbegu hizo utasaidia kurejesha uzalishaji na kuimarisha usalama wa chakula kwa wakazi wa Hanang kwani mbegu za dengu ni mkakati wa kuongeza uzalishaji wa mazao ya biashara yenye soko la uhakika ndani na nje ya nchi.

Kwa upande Mkuu wa Wilaya ya Hanang Almishi Issa Hazali amemshukuru Mbunge Asia Halamga kwa kuwakumbuka wananchi wa Jimbo hilo na kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuwaletea maendeleo wananchi

“Hatua hii ni ya kupongezwa kwani inaenda moja kwa moja kugusa maisha ya wananchi wetu na sisi kama Serikali tutaendelea kushirikiana na Mbunge sambamba na viongozi wengine wote wenye nia njema ya kuleta maendeleo katika Jimbo letu hili,” Amesema Almishi

Hata hivyo wananchi hao wamemshukuru sana Mbunge huyo kwa msaada huo ambao utaleta mapinduzi makubwa katika sekta ya kilimo.




 


Umoja wa Wanawake Machinga Dodoma(UWAMADO) wamempongeza Mh. Rais Dkt. Samia S. Hassan kwa ujenzi wa soko la kisasa la Machinga Complex na miundombinu ya kisasa ya soko hilo ambalo ni la kipekee nchini.

Hayo yamesemwa jana wakati wa uzinduzi wa chama cha UWAMADO uliofanyika kwenye eneo la soko la Machinga Complex kwa kuzinduliwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mh. Rosemary Senyamule

Akisoma Risala Katibu wa UWAMADO Bi. Mariam Kajembe amesema umoja huo umelenga kuwaleta wanawake Machinga pamoja ili kujijenga na kujiimarisha uchumi.

Aidha pia UWAMADO umempongeza Mh. Rais Dkt. Samia S. Hassan kwa ujenzi wa Soko la Machinga Complex ambalo limesaidia kuwaleta pamoja wafanyabiashara wengi wadogo pamoja ambao awali hawakuwa katika maeneo rasmi na hivyo kuwafanya kutokuwa rasmi.

Akitoa hotuba yake,Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mh. Rosemary Senyamule amewapongeza UWAMADO kwa kuamua kuanzisha umoja wao ambao utawasaidia kujiendeleza zaidi na kujiimarisha kiuchumi.

“Jambo hili la kuanzisha umoja ni jambo jema,hakikisheni umoja unafikia malengo mliyokusudia.

Mh. Rais kawajengea soko kubwa na zuri,soko hili liwe kichocheo cha ukuaji wenu kimtaji na kibiashara.

Niwatake Uongozi wa Jiji la Dodoma kuendelea kubuni na kuanzisha maeneo mapya ya kuwapanga vizuri wafanyabiashara wadogo wa Dodoma”Alisema Senyamule

Akitoa salamu zake Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini Mh. Anthony Mavunde amewapongeza UWAMADO kwa kuona umuhimu wa kukaa pamoja kujiinua kiuchumi na kuwataka kuchangamkia fursa ya mikopo ya asilimia 10% ya mapato ya ndani ya Jiji ambayo kiasi cha Shilingi Bilioni 7 kimetengwa kwa ajili ya kuwawezesha wakina mama,vijana na watu wenye ulemavu.











 


Mbunge wa Jimbo la Msalala mkoani Shinyanga, Mhe. Iddi Kassim, ametoa baiskeli 92 kwa wenyeviti wa vijiji vyote vya Halmashauri ya Msalala kwa lengo la kuwawezesha kufuatilia kwa ukaribu utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao.

Baiskeli hizo zenye thamani ya shilingi milioni 23 zimekabidhiwa rasmi katika hafla iliyofanyika leo katika kata ya Bugarama zikiwa ni kwa ajili ya wenyeviti wa vijiji katika jimbo zima la Msalala kwa lengo la kurahisisha usafiri wa viongozi hao kuzungukia miradi ya maendeleo katika maeneo yao.

Zoezi hilo la ugawaji wa baiskeli limefanyika leo Mei 4,2025 likiongozwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Taifa, Mohammed Ali Kawaida, ambaye pia amehutubia wananchi na kuwahimiza kuhakikisha miradi ya maendeleo inalindwa na kutunzwa kwa manufaa ya wote.


“Ni jambo la kuigwa. Mbunge amewawezesha viongozi wa msingi kufanikisha usimamizi wa maendeleo ya wananchi. Nawasihi wenyeviti kutumia baiskeli hizi kwa shughuli zilizokusudiwa,” amesema Kawaida na kupongeza hatua hiyo aliyoitaja kuwa ya kipekee katika ziara yake ya siku 10 nchini.


"Naomba mkazitunze hizi baiskeli ili ziwasaidie katika kuzungukia miradi ya maendeleo inayotekelezwa na ilani ya Chama cha mapinduzi (CCM)", amesema.


Akizungumza katika mkutano huo, Mbunge Iddi amesema kuwa wenyeviti wa vitongoji na vijiji wanafanya kazi kubwa bila kuwa na mshahara na kwamba jimbo la msalala lina utajiri mkubwa unaoweza kuwapa posho wenyeviti hao kupitia mapato ya ndani.

Ameeleza kuwa kila baiskeli imegharimu shilingi 250,000, na kwamba hatua hiyo inalenga kuwawezesha wenyeviti kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi mbalimbali ili kuhakikisha changamoto zinagunduliwa mapema na kutafutiwa ufumbuzi.


Aidha Mheshimiwa Iddi amewataka viongozi kuwatumikia wananchi kwa kusimamia kwa uaminifu miradi ya maendeleo ili kuinua Uchumi wa taifa na Uchumi wa mtu mmoja mmoja.


“Katika vijiji vyetu, kuna miradi mingi inayoendelea na inahitaji usimamizi wa karibu. Nitashirikiana na viongozi hawa kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na maendeleo ya kweli,” ameongeza.


Wakizungumza mara baada ya kupokea baiskeli hizo baadhi ya wenyeviti wamemshukuru Mbunge Iddi na kwamba baiskeli hizo zitawasaidia katika majukumu yao.


Katika tukio hilo, wanachama tisa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutoka Wilaya ya Kahama, wakiongozwa na aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Tendaji ya wilaya hiyo, Samson Thomas, wamehamia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kupokelewa rasmi na Mwenyekiti wa UVCCM Taifa.


Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Thomas amesema wameamua kuunga mkono juhudi za serikali ya CCM katika kusukuma mbele maendeleo ya wananchi, na kuahidi kushiriki kikamilifu katika shughuli za chama na uongozi, huku akiahidi kuwa mtiifu kwa chama hicho.


















 



Akisisitiza umuhimu wa kuwa na Shukrani kama ambavyo imehubiriwa hii leo kwenye Ibada ya Pasaka kwenye Kanisa la KKKT Sinoni Jijini Arusha, Mbunge wa Arusha Mjini Mhe. Mrisho Gambo amemtaja Rais Samia kama Kiongozi aliyeweka alama nyingi za vielelezo vya miradi ya maendeleo Arusha Mjini, akimshukuru kwa kutenga fedha nyingi za kutekeleza miradi ya Maendeleo Arusha.


Mhe. Gambo aliyeshiriki Ibada ya Pasaka kwenye Kanisa hilo na kuchangia shughuli mbalimbali za maendeleo zinazoendelea kanisani hapo, ameeleza kwamba kuwa na Mwanamke Kiongozi kuanzia ngazi ya familia ni baraka na chanzo cha Maendeleo, akisema kwa Arusha pekee Rais Samia amefanikiwa kukuza uchumi wa wananchi kwa asilimia kubwa kwa kipindi kifupi ambacho amekuwa Rais wa Tanzania.


Mhe. Mrisho Gambo amewaambia waumini wa kanisa hilo kuwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa muda mfupi aliokuwa madarakani, ametoa Bilioni 286 kwaajili ya ujenzi wa Uwanja wa michezo Mirongoine kata ya Olmot, lakini pia amesisimua sekta ya utalii Mkoani humo kupitia filamu ya The Royal Tour, suala ambalo limekuza uchumi na kutoa ajira kwa Vijana na wajasiriamali wengi wa Mkoa wa Arusha, akieleza kuwa mambo hayo kwa Arusha yanafanikiwa kutokana na ushirikiano uliopo kati ya Ofisi yake na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Madiwani wa Arusha Mjini.


Gambo pia amezungumzia mradi wa Uendelezaji Miji Tanzania (TACTICS)ambapo ameeleza kuwa kutokana na jitihada za Rais Samia, fedha zimetolewa na Tenda imeshatangazwa ambapo kutafanyika Ujenzi wa Masoko makubwa mawili ya Kilombero na Morombo, yatakayokwenda sambamba na ujenzi wa Kituo kikuu cha Mabasi Arusha itakayojengwa eneo la Bondeni City.


Akizungumzia alama zilizowekwa na Rais Samia kwa Kata ya Sinoni, Mhe. Gambo ameeleza kuwa Rais Samia atatoa Milioni 250 za awali kwaajili ya ujenzi wa Kituo cha afya Sinoni, akitoa pia fedha katika Bajeti ijayo ya serikali kwa ajili ya Ujenzi wa shule ya Sekondari Sinoni ili kupunguza masafa marefu ya wanafunzi kufuata huduma ya elimu kwenye shule za nje ya Sinoni.


Mhe. Gambo amemshukuru Rais Samia pia kwa kuirejesha Arusha kwenye uenyeji wa mikutano ya Kitaifa na Kimataifa, akieleza kuwa mikutano hiyo imekuwa sehemu ya kukuza uchumi wa wananchi wa Arusha Mjini kupitia biashara na Ujasiriamali ambao wamekuwa wakiufanya na kuleta tija kutokana na mwingiliano na ugeni mkubwa wa watu mbalimbali wanaofika Arusha kuhudhuria Mikutano na warsha za ndani na nje ya Tanzania.