Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali inaendelea na mikakati mbalimbali ya kutatua changamoto za tembo katika Wilaya ya Meatu mkoani Simiyu huku akimtaka Mbunge wa Kisesa, Mhe. Luhaga Mpina kuwasiliana na Wizara ya Maliasili na Utalii endapo changamoto hiyo itazidi kuwa kubwa.
Mhe. Rais Samia ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na wananchi wa Meatu mkoani humo katika viwanja vya Stendi ya mabasi leo Juni 17,2025.
"Kuhusu uvamizi wa tembo, mambo haya yanafanyika hatua kwa hatua kama tumeweza kujenga vituo vitatu vya askari uhifadhi, bila shaka tutaendelea kuchukua hatua zaidi na kama tatizo ni kubwa umuone Waziri wa Maliasili na Utalii" amesisitiza Rais Samia.
Awali, Mhe. Mpina aliiomba Serikali kuweka nguvu kubwa ya fedha kwa ajili ya mikakati ya kupambana na wanyamapori wakali hususan tembo.
Kuhusu Sekta ya Utalii, Rais Samia amesema kuwa kukamilika kwa daraja la Itembe mkoani humo, kutarahisisha watalii kupitia Wilaya ya Meatu kuelekea katika hifadhi za Maswa, Ngorongoro na Serengeti hivyo wananchi wajipange kutumia fursa hiyo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema serikali yake ipo kwaajili ya kustawisha maisha ya wananchi wake, akiahidi kuendelea kuharakisha maendeleo kwenye sekta mbalimbali nchini hasa zenye kugusa maisha ya wananchi walio wengi.
Kauli ya Rais Samia ameitoa leo Jumanne Jioni Juni 17, 2025, wakati wa Mkutano wake wa hadhara Wilayani Itilima Mkoani Simiyu mara baada ya kuzindua Hospitali ya Wilaya ya Itilima, akiwataka kuachana na siasa za zao la Pamba, kwani serikali haitochukua hatua yoyote ya kumdhuru Mkulima.
"Katika kilimo na uzalishaji wa pamba kuna siasa kubwaz niwaombe sana tusikilizeni serikali tunavyowaambia. Serikali hata siku moja haitachukua hatua ya kumdhuru mkulima au mwananchi wake, tutachukua hatua za kunyanyua kilimo na kumfanya Mkulima anufaike na Kilimo chake." Amesema Rais Samia.
Rais Samia katika hotuba yake pia amesema serikali itaendelea na jitihada za kuvutia viwanda Wilayani Itilima na Simiyu kwa Ujumla, akionesha kutoridhika na takwimu za uwepo wa Kiwanda Kimoja kikubwa Itilima, vidogo 9 na vidogo kabusa 92 vilivyoajiri Watanzania 414 peke yake.
"Mwenye uwezo wa kuweka viwanda vya kuchakata pamba, kukamua mafuta au viwanda vingine nawahamasisha mfanye kazi hiyo. Nawapongeza Halmashauri kwa kutenga maeneo ya viwanda na biashara, hiyo ni fursa nzuri maeneo yatumike na yatarahisisha adhma yetu ya utekelezaji wa kuwavutia wawekezaji ndani ya Wilaya hii." Amekaririwa akisema Rais Samia.
Rais Samia pia amebainisha kuwa serikali ya awamu ya sita inajenga kiwanda kikubwa cha Vifaatiba wilayani humo kitakachohudumia Tanzania nzima, zikitengwa pia Ekari 1,000 kwaajili ya ujenzi wa viwanda vya kuchakata zao la Pamba Wilayani hapo.
Rais Samia pia amemuelekeza Waziri wa Ujenzi Mhe. Abdallah Ulega kwenda Wilayani Itilima Mkoani Simiyu kufuatilia ombi la Mbunge wa Jimbo hilo, aliyemuomba Mhe. Rais ujenzi wa barabara ndani ya Wilaya hiyo, akimtaka Waziri Ulega pia kufunga taa kwenye barabara zilizopo wilayani humo.
Na John Mapepele - OR TAMISEMI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt, Samia Suluhu Hassan leo amezindua Hospitali ya Wilaya ya Itilima iliyogharimu shilingi bilioni 4.7 iliyojumuisha ujenzi wa miundombinu na ununuzi wa vifaatiba huku wananchi wakimpongeza.
Mhe. Rais amezindua Hospitali hiyo leo akiwa kwenye siku ya tatu ya ziara yake ya kikazi katika mkoa wa Simiyu ambapo tangu aanze ziara hiyo amekagua na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo iliyogharimu mabilioni ya fedha huku akifanya mikutano na wananchi.
Akizungumza mara baada ya kuzindua hospitali hiyo, amefafanua kuwa dhamira ya Serikali yake ni kusogeza huduma bora kwa wananchi.
" Nimeridhishwa na miundombinu ya hospitali hii ilivyo ya kisasa na fedha iliyotumika, kimsingi hospitali hii ina kila kitu ambacho kinatakiwa kuwepo kwenye hospitali". Ameongeza Mhe. Rais huku akishangiliwa na wananchi waliofurika kumlaki
Aidha, ameeleza kuwa Serikali imejenga hospitali kama hiyo katika maeneo tofauti ya nchi lengo likiwa ni kuwapunguzia wananchi kwenda umbali mkubwa kupata huduma za afya.
Amewaahidi wananchi kuwa Serikali yake itaendelea kuwaletea maendeleo wananchi wake na kuwa kuwaboreshea maisha.
Akimkaribisha Mhe. Rais Samia ili aongee na maelfu ya wananchi katika mkutano wa kuhitimisha ziara kwa siku ya leo Waziri wa Ardhi, nyumba na maendeleo ya Makazi Mhe. Deogratius Ndejembi kwaniaba ya Waziri wa Nchi, TAMISEMI, Mhe Mohamed Mchengerwa amesema TAMISEMI kupitia Idara ya afya ilipewa shilingi trilioni 1.34 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za wilaya na zahanati nchini nzima kwenye Halmashauri zote 184 zikihusisha pia ununuzi wa Vifaa tiba.
Aidha aliongeza kuwa Rais Samia ameongeza bajeti ya ujenzi wa barabara za mijini na vijijini katika Halmashauri ya Wilaya ya Itilima kutoka Shilingi Milioni 800 mwaka 2021 hadi kufikia Bilioni 2.5, suala ambalo limewezesha barabara zote za wilaya hiyo kupitika kwa msimu wote wa mwaka.
Anna Masanja, Mkazi wa Itilima amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia imefanya maboresho makubwa kwenye kila sekta katika kipindi kifupi cha uongozi wake.
"Kwa kusema ukweli Mama Samia ametuheshimisha wananchi kwa kufanya makubwa kwenye elimu, miundombinu, afya, umeme hata maji" ameongeza Buliga Amos Mkazi wa Meatu
▪️Aelekeza mabadiliko ya Kanuni ili kuruhusu uhaulishwaji teknolojia kwa Kampuni za Kigeni
▪️Ataka Watanzania kuchangamkia Trilioni 5.3 za usambazaji bidhaa na utoaji huduma
▪️Rais Samia apongezwa kwa uongozi wa maono
▪️Watanzania 19,371 wanufaika na ajira rasmi
▪️Kamati ya Bunge yaipongeza Wizara kwa ukuaji wa sekta
MWANZA
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde ameitaka Tume ya Madini kuwapa kipaumbele watanzania kwenye usambazaji wa huduma na bidhaa kwenye migodi ya madini ili kujipatia kipato, kuongeza mzunguko wa fedha nchini hivyo Sekta ya Madini kuendelea kuwa na mchango mkubwa kwenye Pato la Taifa.
Mhe. Waziri Mavunde ameyasema hayo mapema leo Juni 17, 2025 jijini Mwanza kwenye ufunguzi wa Jukwaa la Nne la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini linalokutanisha wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na Wizara ya Madini na Taasisi zake, Taasisi za Serikali, Taasisi Binafsi, Taasisi za Fedha, Kampuni za Uchimbaji wa Madini na Watoa Huduma kwenye Migodi ya Madini.
Amesema kuwa katika kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini na kuhakikisha watanzania wananufaika na rasilimali madini, Serikali imeendelea kusimamia ipasavyo Sheria ya Madini, Sura 123 Kifungu Na. 102 na Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania za Mwaka 2018 ili kuweka usimamizi thabiti katika utekelezaji wa masuala ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini nchini.
Amesisitiza kuwa lengo la uwepo wa Kanuni za Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini ni kuhakikisha watanzania wanashiriki ipasavyo kupitia usambazaji wa bidhaa na huduma kwenye migodi ya madini badala ya kampuni kuagiza bidhaa kutoka nje ya nchi.
Aidha Mhe. Mavunde ameitaka Tume ya Madini kufanya mabadiliko ya Kanuni ili kuruhusu uhaulishwaji teknolojia kwa Kampuni za Kigeni ambapo itatoa fursa kwa kampuni za kitanzania kushirikiana na kampuni za kigeni kwenye utoaji wa huduma migodini na kujifunza teknolojia mpya kutoka kampuni za kigeni.
Katika hatua nyingine, Mhe. Mavunde amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake makubwa ya kuendeleza Sekta ya Madini hali iliyopelekea mabadiliko makubwa ambapo mpaka sasa mafanikio makubwa yamepatikana.
“Mpaka sasa mafanikio makubwa yamepatikana hasa kwa wachimbaji wadogo ambapo wameanza kukopesheka kutoka kwenye Taasisi za Fedha, ushiriki wa watanzania kwenye shughuli za uchimbaji, uchenjuaji, biashara ya madini na utoaji wa bidhaa na huduma kwenye migodi ya madini umeongezeka na mchango wa wachimbaji wadogo kwenye makusanyo ya maduhuli umeendelea kuimarika,” amesisitiza Mhe. Mavunde.
Akielezea mafanikio ya utekelezaji wa kanuni za ushirikishwaji wa watanzania katika Sekta ya Madini, Waziri Mavunde amesema katika kipindi cha mwaka 2023/2024 jumla ya ajira rasmi 19,874 zilizalishwa katika migodi ya madini ambapo ajira 19,371 sawa na asilimia 97 zilitolewa kwa Watanzania na ajira 503 sawa na asilimia 3 zilitolewa kwa wageni.
![]() |
Aidha, amewataka watanzania kuchangamkia fursa za uwekezaji katika Sekta ya Madini hasa kwenye usambazaji wa bidhaa na huduma kwenye migodi ya madini kama vile usambazaji wa vifaa, vyakula na huduma na kuzitaka Taasisi za Kifedha kuendelea kuwakopesha mitaji.
Amesema kuwa kampuni za madini zinatumia kiasi cha shilingi Trilioni 5.3 kila mwaka kwa ajili ya manunuzi ya bidhaa na huduma zinazotumika migodini na kuwataka watanzania kuchangamkia fursa hizo.
Naye Mkuu wa Wilaya Ilemela, Mhe. Hassan Masala akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Said Mtanda amempongeza Waziri Mavunde kwa usimamizi mzuri wa Sekta ya Madini hali iliyopelekea mafanikio makubwa ikiwa ni pamoja na ongezeko la wawekezaji nchini.
Ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji kuwekeza katika mkoa wa Mwanza hasa katika eneo la uchimbaji wa madini na utoaji wa huduma mbalimbali kwenye migodi ya madini.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Msafiri Mbibo amesisitiza kuwa Wizara ya Madini itaendelea kufungamanisha Sekta ya Madini na sekta nyingine muhimu za kiuchumi ili kuongeza ushiriki wa watanzania kwenye shughuli za madini nchini.
Wakati huohuo akizungumza kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Dkt David Mathayo, Mbunge wa Ilemela, Dkt. Angeline Mabula amepongeza kazi kubwa inayofanywa na Waziri Mavunde hali iliyochangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa.
“Kupitia uongozi wa Mhe. Mavunde tumeshuhudia mapinduzi makubwa kwenye Sekta ya Madini ambapo Tanzania imepiga hatua kubwa ya kihistoria kwa kufikia mchango wa asilimia 10.1 katika Pato la Taifa kwa Mwaka 2024, ikiwa ni Mwaka mmoja (1) kabla ya lengo la asilimia 10 lililowekwa kwenye Sera ya Madini ya Mwaka 2009 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026),” amesisitiza Dkt. Mabula
Naye Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Dkt. Janet Lekashingo amesema kuwa Tume imeanza kukusanya takwimu za bidhaa zinazoingizwa nchini ili kushauri Serikali kuhusu uanzishwaji wa viwanda vinavyotoa bidhaa husika na kuongeza mzunguko wa fedha nchini huku wananchi wakijipatia ajira.
Katika hatua nyingine, Kamishna wa Tume ya Madini ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini, Dkt. Theresia Numbi ameeleza mikakati iliyowekwa na Tume ya Madini ya kuongeza ushiriki wa watanzania katika Sekta ya Madini kuwa ni pamoja na mikutano, majukwaa na vyombo vya habari.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Kenani Laban Kihongosi ameahidi kuendelea kutekeleza maelekezo na maagizo ya Rais Samia Suluhu Hassan, akimshukuru kwa kuridhi na kutoa zaidi ya Shilingi Bilioni 60, kutekeleza miradi na huduma mbalimbali za Maendeleo kwenye Wilaya ya Meatu Mkoani humo.
Mhe. Kenani amebainisha hayo leo Jumanne Juni 17, 2025 wakati akitoa salamu za Mkoa kwa Rais Samia Suluhu Hassan wakati wa ziara yake Wilayani Meatu Mkoani Simiyu akieleza kuwa fedha hizo zimetekeleza miradi ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo ujenzi wa Daraja la Itembe lililogharimu Bilioni 8.4 pamoja na ruzuku ambazo zimekuwa zikitolewa kwenye mbolea, mbegu na viuatilifu kwenye zao la Pamba
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Meatu Mhe. Leah Komanya amemshukuru Rais Samia kwa utekelezaji mkubwa wa maboresho katika huduma za afya Meatu pamoja na utekelezaji wa mradi mkubwa wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi (Simiyu Climate Resilience Project) katika wilaya tano za Mkoa wa Simiyu, akisema mradi huo utaondoa changamoto kubwa ya uhitaji wa maji iliyotokana na ukame Wilayani Meatu.
Aidha Mbunge wa Kisesa Mhe. Luaga Mpina, amempongeza Rais Samia kwa kwa maboresho makubwa kwenye mifumo ya kodi nchini, akimuomba Rais Samia kuharakisha ujenzi wa Treni ya kisasa ya SGR ili kuongeza thamani na faida kwa wakulima na wafugaji wa Kanda ya Ziwa ikiwemo Mkoani Simiyu.Luaga ameeleza kuwa wananchi wa Kisesa na Meatu kwaujumla wameahidi kumpa kura za kishindo Rais Samia katika uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Na. James K. Mwanamyoto OR-TAMISEMI
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema kwa kuzingatia mamlaka aliyopewa kwa mujibu wa sheria, tayari amekwisha saini notisi za kuvunjwa kwa Mabaraza ya Madiwani katika Mamlaka za Wilaya na Mamlaka za Miji, kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Waziri Mchengerwa amesema hayo leo, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Rais-TAMISEMI jijini Dodoma.
Mhe. Mchengerwa amesema kuwa, notisi hizo za Kuvunjwa kwa Mabaraza ya Madiwani katika Mamlaka za Wilaya, na Mamlaka za Miji, 2025 zitatangazwa kwenye Gazeti la Serikali hivi karibuni.
Mhe. Mchengerwa amefafanua kuwa, notisi hizo zinaelekeza kwamba vikao vya Halmashauri na Kamati zake zinapaswa ziwe zimekoma siku saba kabla ya kuvunjwa kwa Bunge hapo tarehe 27 Juni, 2025.
“Vikao vya Halmashauri na Kamati zake zinapaswa kuwa zimekoma ifikapo tarehe 20 Juni, 2025 hivyo Mkurugenzi wa Halmashauri atawajibika kwa kufanya kikao chochote cha Halmashauri au Kamati yake baada ya tarehe hiyo,” Waziri Mchengerwa amesisitiza.
Baada ya mabaraza ya madiwani kufikia ukomo tarehe 20 Juni 2025, Mhe. Mchengerwa ameelekeza masuala yote ya kiutendaji katika Halmashauri kusimamiwa na Mkurugenzi wa Halmashauri, ambaye atakuwa Mwenyekiti wa Halmashauri kwa kipindi cha mpito, akisaidiana na Wakuu wa Idara watakaokuwa kama wajumbe wa kamati.
Sanjari na hilo, Waziri Mchengerwa ameelekeza kuwa Mkurugenzi wa Halmashauri hataruhusiwa kuanzisha miradi au uwekezaji mpya ikiwa ni pamoja na kubadilisha au kurekebisha mradi, uwekezaji au uamuzi wowote uliopitishwa na Halmashauri kabla ya kuvunjwa.
“Matumizi mabaya ya mamlaka au kutotekeleza kwa ufanisi majukumu ya kiutawala kwa mujibu wa notisi hizi, kutamfanya Mkurugenzi kuwajibika binafsi kwa mujibu wa Sheria,” Mhe. Mchengerwa amehimiza.
Pia, Waziri Mchengerwa ameelekeza kwamba katika kikao cha kwanza cha Baraza jipya la Madiwani baada ya uchaguzi kufanyika, Mkurugenzi wa Halmashauri atapaswa kuwasilisha taarifa ya maamuzi na mwenendo wa vikao vya menejimenti vilivyofanyika wakati wa kipindi champito.
Aidha, Waziri Mchengerwa amewashukuru na kuwapongeza Madiwani wote waliomaliza muda wao wa uongozi kwa kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Jumanne Juni 17, 2025 anatarajiwa kuendelea na ziara yake ya Kikazi Mkoani Simiyu, akipangiwa kufungua kiwanda cha Kuchakata Pamba cha Biosustain Meatu pamoja na miradi mingine ya maendeleo Mkoani humo.
Rais Samia atafungua pia Hospitali ya Wilaya ya Itilima pamoja na kufanya mikutano kadhaa ya hadhara na kuzungumza na wananchi kwenye Kiwanja cha Stendi ya Mabasi Meatu pamoja na Mkutano mwingine utakaofanyika kwenye Kiwanja cha stendi ya Mabasi Itilima mkoani humo.
Jana Rais Samia alizindua kampeni ya Kitaifa ya chanjo na utambuzi wa mifugo, Jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Jengo la Halmashauri ya Bariadi Mji, Uzinduzi wa Ofisi za Mamlaka ya mapato Tanzania Mkoa wa Simiyu pamoja na kiwanda cha uzalishaji mabomba na cha uchakataji wa Pamba Mkoani Simiyu. Ziara ya Rais Samia Kanda ya ziwa itampeleka mpaka Jijini Mwanza, alipopangiwa kuzindua miradi mbalimbali ikiwemo daraja la Kigongo- Busisi Jijini Mwanza.
Benki ya Tanzania(BOT) leo imesaini mikataba na Kampuni za Uchimbaji Madini za Geita Gold Mine(GGM),Buckreef Gold Ltd na Shanta Ltd juu kampuni hizo kuiuzia BOT kiasi kisichopungua asilimia 20 ya dhahabu inayozalishwa kama ambayo imeelezwa kwenye kifungu cha 59 cha Sheria ya Madini,Sura ya 123.
Hafla hiyo ya utiaji saini mikataba ya uuzwaji wa dhahabu imefanyika leo tarehe 16.06.2025 Jijini Dodoma na kushuhudiwa na Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu L. Nchemba na Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde.
Akizungumza katika hafla hiyo Mh.Mwigulu Nchemba amempongeza Mh. Rais Dkt. SamiaS. Hassan kwa uongozi wenye maono na ambao umechochea kukua kwa hifadhi ya dhahabu ya BOT hali ambayo itasaidia kuimarisha uchumi wa Tanzania.
“Serikali kupitia Wizara ya Fedha itaendelea kuhakikisha inaiwezesha Benki kuu katika manunuzi ya dhahabu ili kuongeza akiba ya nchi ya 𝙢𝙤𝙣𝙚𝙩𝙖𝙧𝙮 𝙜𝙤𝙡𝙙.
Nampongeza Waziri Mavunde kwa usimamizi mzuri wa sekta ya madini mpaka kufikia hatua hii,naamini kwa miaka michache ijayo nchi yetu itakuwa miongoni mwa nchi zenye akiba kubwa ya hifadhi ya dhahabu kupitia Benki Kuu.”Alisema Mwigulu
Naye Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde amezipongeza Kampuni zote za uchimbaji na usafishaji madini kwa kusaini mikataba hiyo ambayo ina matokeo makubwa katika kukuza uchumi wa Tanzania na kuchochea uongezaji thamani madini nchini.
Mavunde aliongeza kuwa hatua ya ununuzi wa dhahabu wa BOT kupitia wachimbaji wadogo na wakubwa utaiweka Tanzania kwenye ramani ya Afrika kuwa miongoni mwa nchi 10 zenye hifadhi kubwa ya dhahabu kupitia Benki Kuu.
Akitoa taarifa ya awali Gavana wa Benki Kuu Ndg. Emmanuel Tutuba amesema hatua hii ya ununuzi wa dhahabu kupitia BOT utasaidia kuimarisha Uchumi na Shilingi ya Tanzania na kwamba imejipanga kuikuza hifadhi hii ya dhahabu kwa kuendelea na ununuzi kila mwaka ili kufanikisha azma ya Serikali ya kuwa na hifadhi ya dhahabu itakayoihakikishia Tanzania uchumi imara.
Gavana Tutuba ameongeza kwamba mpaka sasa BOT imeshanunua Tani 5.02 huku lengo likiwa kununua Tani 6 za dhahabu kwa mwaka wa fedha 2024/2025 ambapo malipo yote yamefanyika ndani ya masaa 24.
*Na Mwandishi Wetu – Addis Ababa, Ethiopia*
Tanzania imeshiriki Maadhimisho ya Miaka 25 ya Jumuiya ya Tathmini Afrika (AfrEA) yanayofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 16 hadi 18 Juni, 2025, katika Kituo cha Mikutano cha Umoja wa Mataifa (UNECA), jijini Addis Ababa, Ethiopia.
![]() |
Ujumbe wa Tanzania umeongozwa na Mkurugenzi wa Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Bi. Sakina Mwinyimkuu.
Washiriki wengine kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu ni Mkurugenzi wa Mipango na Bajeti Bw. Eleuter Kihwele na Mkaguzi Mkuu wa Ndani katika Ofisi hiyo Bw. Exavery Salira.
Maadhimisho hayo ya siku tatu yameandaliwa kwa lengo la kuenzi mchango wa tathmini katika maendeleo barani Afrika, na kuimarisha uwajibikaji wa sera kwa kutumia ushahidi (Evidence Based) katika kufanya maamuzi.
Aidha Washiriki kutoka nchi mbalimbali ndani na nje ya bara la Afrika wanajadili mbinu bunifu na jumuishi za tathmini kwa maendeleo endelevu yenye muktadha wa Kiafrika.
"Ndugu zangu nimejulishwa kuwa jumla ya wataalamu wa mifugo takribani 3800 watashiriki moja kwa moja kwenye kampeni hii katika maeneo mbalimbali nchini. Kutokana na uhaba wa maafisa wa ugani wa mifugo katika Mamlaka za serikali za mitaa, mpango uliopo unaenda kutoa pia fursa za ajira za muda mfupi 7500 kwa vijana wetu, wataalamu wa mifugo hususani Vijana waliopo nje ya mfumo wa ajira au ajira rasmi.
Sasa ninawasihi watambue kwamba wamekabidhiwa jukumu kubwa hilo wakahudumie mifugo yetu hiyo kwa weledi na kwa uzalendo ili kupata matokeo yanayotarajiwa. Tukifanya vinginevyo tutakuja kulaumu wazalishaji wa chanjo kumbe uchanjwaji umekosewa, kwahiyo niwaombe sana wale wote watakaoshiriki kwenye zoezi hili wafanye kadri watakavyoelekezwa na wataalamu.
Hatutarajii kujitokeza kwa uzembe katika kuhudumia maisha ya mifugo yetu aidha kwa mara nyingine tena niwatake wafugaji kujitokeza kwa wingi kupeleka mifugo katika maeneo ya chanjo na utambuzi."- Rais Samia Suluhu Hassan wakati akizungumza na wananchi wa Bariadi Mkoani Simiyu, mara baada ya kuzindua Kampeni ya Kitaifa ya Chanjo na utambuzi wa mifugo leo Juni 16, 2025.
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga amesema gharama ya kujaza gesi kwenye mitungi (LPG) ni himilivu ikiwa ni jitihada zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ili kuwezesha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.
Mhe. Kapinga ameyasema hayo leo Juni 16, 2025 katika ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan mkoani Simiyu wakati wa kuzindua Shule Maalum ya Sayansi ya Wasichana ya Simiyu ambayo imefungwa miundombinu ya nishati safi ya kupikia.
“Mheshimiwa Rais ulituelekeza Taasisi ambazo zinahudumia watu zaidi ya mia moja tuzifungie miundombinu ya nishati safi ya kupikia, Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na TAMISEMI tunatekeleza agizo hilo kwa kuzifungia mifumo ya nishati safi shule mpya ambazo zinajengwa." Amesema Kapinga
Ameeleza kuwa, uwezo wa shule hiyo ni wanafunzi 800 na mifumo ya Nishati Safi ya Kupikia iliyofungwa ina uwezo wa kuhudumia wanafunzi 800.
Ameongeza kuwa, kwa idadi hiyo ya wanafunzi 800 mtungi wa gesi katika Shule ya Wasichana Simiyu utakuwa ukijazwa kila baada ya miezi miwili.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Juni 16, 2025 akiwa ziarani Mkoani Simiyu amezindua shule ya Sekondari ya wasichana Simiyu, miongoni mwa shule 26 zilizojengwa kwenye Mikoa yote ya Tanzania bara ikiwa ni sehemu ya mpango wa Rais Samia wa kuboresha kiwango cha taaluma ya Sayansi kwa wasichana nchini.
Kulingana na Waziri wa nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na serikali za Mitaa Mhe. Mohammed Mchengerwa, amebainisha kuwa katika kutekeleza dhamira ya Rais Samia, serikali ya awamu ya sita ilitoa takribani Bilioni 115.48 kwaajili ya ujenzi wa shule hizo 26, shule ambazo zimekamilika na zina wanafunzi takribani 9,810 kwasasa.
Kwa Mkoa wa Simiyu takribani Bilioni 4.45 zilitolewa na kutumika kwenye ujenzi wa shule hiyo ikihusisha Mabweni ya wanafunzi, viwanja vitatu vya michezo, nyumba tano za waalimu, Madarasa 22, maabara nne za Fizikia, Kemia, Baiolojia na Geografia, Jengo la utawala pamoja na Bwalo na Jiko lake lenye kutumia nishati safi ya kupikia.
Awali wakati akisoma taarifa hiyo kwaniaba ya Mkurugenzi Mtendajiwa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi,Mkuu wa Shule hiyo Mwalimu Huruma Mtindya amebainisha kuwa shule hiyo inatarajiwa kukamilika ujenzi wake mwishoni mwa mwezi huu, akieleza pia changamoto ya ukosefu wa samani kwenye bwalo la Chakula, Genereta na Gari ya shule, kama miongoni mwa changamoto zilizopo shuleni hapo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ameeleza kuwa serikali yake imeanza rasmi kutoa ruzuku kwa wafugaji wa Tanzania, ikianza na ruzuku ya Chanjo kwa kuku Takribani Milioni 40, Mbuzi na Kondoo Milioni 17 pamoja na hereni za utambuzi kwa mifugo aina ya Ng'ombe.
Rais Samia amebainisha hayo wakati akizungumza na wananchi wa Bariadi Mkoani Simiyu, mara baada ya kuzindua Kampeni ya Kitaifa ya chanjo na utambuzi kwa mifugo akitoa wito kwa wafugaji nchini kushiriki kikamilifu kwenye zoezi hilo lenye kaulimbiu isemayo "Mifugo ni utajiri, chanja na kuitambua ili kuongeza thamani."
'Sababu mojawapo ya sekta ya mifugo kuwa na mchango mdogo kwanza ni kutotambulika na kutotumika vyema kwa rasilimali ya mifugo tuliyonayo, tulikuwa tunafuga kienyeji, tunafuga kama ni mila na desturi kwamba kufuga ni kazi yetu, lakini tulikuwa tunafuga kama fahari yetu kuwa na ng'ombe wengi lakini hao ng'ombe hawakuzalishii, tuna ng'ombe tunaishi nao miaka 15, 20 lakini wenyewe hawatuzalishii kitu." amesema Rais Samia.
Rais Samia amebainisha kuwa serikali imewekeza zaidi ya shilingi Bilioni 216 kwaajili ya Kampeni hiyo, magonjwa yanayolengwa yakiwa ni Homa ya mapafu ya Ng'ombe, Sotoka ya Mbuzi na Kondoo pamoja na chanjo ya Mdondo ambayo imekuwepo kwa Kuku.
Kulingana na Rais Samia, gharama za chanjo kwa kuku zote zimebebwa na serikali sambamba na hereni za utambuzi, huku chanjo nyingine serikali na wafugaji wakichangia nusu kwa nusu, lengo likiwa ni kuiwezesha nchi kwa pamoja kuwa na kanzidata ya mifugo na kuongeza tija kwa wafugaji na thamani ya mifugo.
Akisitiza Kampeni hiyo kuwa endelevu, Rais Samia ameeleza kuwa kwasasa mauzo ya mifugo na bidhaa za mifugo nje ya nchi yameongezeja kutoka tani 692 mwaka 2021 hadi tani 14, 701 mwaka 2024, ikiwa na thamani ya Dola Milioni 61.4, akieleza kuwa matarajio yake ni kuongeza zaidi kwa mauzo hayo mara baada ya zoezi la Chanjo kukamilika kwani kutaongeza sifa ya Tanzania katika ithibati zinazokubalika kwenye soko la mifugo na bidhaa zake.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Jumatatu Juni 16, 2025 amesisitiza umuhimu wa Watanzania kuwekeza ndani ya nchi yao ili kukuza uchumi na kuiwezesha nchi kuondokana na utegemezi wa mikopo na misaada kutoka nje ya Tanzania.
Rais Samia amebainisha hayo muda mfupi baada ya kuzindua kiwanda cha kuchakata Pamba na kiwanda cha Mabomba (Moli Oils Mills company), vinavyomilikiwa na kampuni ya NGS vilivyopo Bariadi Mjinj Mkoani Simiyu na vikimilikiwa na Mtanzania kwa zaidi ya asilimia 90 na vikitarajiwa kutoa ajira zaidi ya mia nane kwa watanzania.
Akizungumzia tija ya uwepo wa viwanda hivyo, mbali ya kutoa ajira, Rais Samia amebainisha kuwa Viwanda hivyo vitapunguza matumizi ya fedha za kigeni zilizokuwa zinatumika kuagiza bidhaa nje ya nchi sambamba na kuwezesha utekelezaji wa sera ya serikali ya kuongeza thamani bidhaa mbalimbali ndani ya nchi kabla ya kuziuza nje.
"Nimshukuru mwekezaji hapa wa ndani amewaza kuongeza thamani zao la Pamba kwa hatua ya kwanza lakini kwa hatua ya pili, tutanunua kwake kuweka kwenye kiwanda ambacho tayari tunaanza kukijenga cha kutengeneza nyuzi za pamba, tunataka kusitisha kupeleka pamba yetu kama ilivyo kwenye marobota kwa wenzetu wakatengeneze nguo na watu wao wapate kazi. Tunataka pamba yetu tuitengeneze hapa hapa ili watu wetu wa Simiyu waweze kupata ajira."Amesema Rais Samia.
Katika hatua nyingine Rais Samia amesisitiza dhamira ya kuinua mazao mbalimbali ya biashara nchini ikiwemo zao la Pamba, akiwaomba wananchi wa mkoa wa Simiyu kukubaliana na hatua zinazochukuliwa kwenye sekta ya Kilimo kwani hakuna dhamira yeyote ya kuweza kuwakandamiza na kuwaumiza wakulima wa Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Jumatatu Juni 16, 2025 akiwa Mkoani Simiyu kwenye ziara yake ya kikazi, amezindua jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo pamoja na jengo la Halmashauri ya ya Mji wa Bariadi.
Kulingana na Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za mikoa na serikali za mitaa TAMISEMI, ujenzi na uzinduzi wa majengo hayo ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Samia, ambaye alipoingia madarakanj aliagiza kuboreshwa kwa miundombinu kwenye Mikoa yote 26 ya Tanzania bara ambapo Jumla ya Shilingi Bilioni 91.17 zilitengwa kukarabati na kujenga Ofisi za Mikoa.
Aidha shilingi Bilioni 94.74 zilitengwa kwa Mamlaka za serikali za Mitaa kwaajili ya kujenga na kukarabati majengo ya Wakurugenzi watendaji wa Halmashauri za Miji, Majiji na Wilaya kote Tanzania bara ambapo Mkoa wa Simiyu ulipokea Bilioni 14.10, ambazo zimejenga Majengo manne ya Wakurugenzi, Matano ya wakuu wa Idara pa.oha na jengo la Halmashauri ya Bariadi Mji ambalo limegharimu shilingi Bilioni 3.9
Katika ziara yake Mkoani Simiyu itakayompeleka baadae Mkoani Mwanza, leo pia Rais Samia amepangiwa kufungua shule ya Wasichana Simiyu pamoja na kufungua kampeni ya Kitaifa ya Chanjo na utambuzi wa mifugo na baadae jioni kuhutubia wananchi katika Mkutano wa hadhara.
MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu Taifa(CCM)Namelock Sokoine amesema tunapokwenda kwenye uchaguzi mjue mnaenda kugombea na si kugombana
Aidha alisema baada ya siasa kuisha kunamaisha mengine hivyo msiumizane katika chaguzi
Namelock aliyasema hayo jana Jijini Arusha wakati wa mapokezi ya kumpokea mjumbe huyo aliyeteuliwa naa Rais Samia Hassan Suluhu kwenye nafasi hiyo ya wajumbe 28 wa Kamati Kuu ukumbi wa CCM Mkoa.
"Tusiumizane katika chaguzi tupo viongozi hapa ambao tutashiriki katika nafasi za ndani katika michujo tusitumie nafasi zetu kukanyaga wenzetu ambao hawapo katika vikao hivyo, namshukuru Rais Samia kwa kuniteua katika nafasi hii"
Alisisitiza kutoumizana katika uchaguzi huu mkuu wa mwaka 2025 badala yake viongozi wanaoshiriki kuamua katika maamuzi watende haki
Alisema Rais Samia Hassan Suluhu amebeba maono ya haki na usawa hivyo tuwe na hofu ya mungu na tusiumize wenzetu
Alihoji kwanini vijana na watu mbalimbali wanakubali Rais Samia Hassan Suluhu kutukwanwa kwenye mitandao ya kijamii hivyo tusiendekeze matusi na dhihaka kwa Rais wetu tuheshimiane
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Arusha, Thomas ole Sabaya alimpongeza Namelock kwa kuteuliwa katika nafasi hiyo ya kuamua maamuzi ngazi za juu na kuongeza kuwa Rais Samia anatoa fedha nyingi mkoani Arusha kwaajili ya miradi ya maendeleo
Wakati huo huo, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda alisisitiza amani katika kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 na kuongeza kuwa uchaguzi si kabila wala dini ya mtu bali ni uwezo wa kuchagua mtu mwenye kutatua changamoto