Waziri wa Madini Anthony Mavunde  amezindua mradi wa uchimbaji Madini ya dhahabu kwa vijana, wanawake na wenye ulemavu kwa kutoa leseni za uchimbaji mdogo wa madini ikiwa ni utekelezaji wa Programu ya Mining For a Brighter Tomorrow (MBT).

Amezindua mradi huo leo Mei 03, 2025 katika viwanja vya shule ya sekondari Ingwe vilivyopo katika eneo la Nyamongo wilayani Tarime  Mkoa wa Mara ambapo ametoa leseni 48 za uchimbaji mdogo wa madini kwa wanufaika zaidi ya 2000 vijana, wanawake na wenye nahitaji maalumu.

Akizungumza katika hafla hiyo amesema, Wizara ya Madini imekamilisha maandalizi ya Programu ya MBT ambayo itatekelezwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2025 hadi 2030 ambapo Programu hiyo ni ya kimageuzi katika Sekta ya Madini ambayo imeanzishwa kwa ajili ya kushughulikia changamoto na kuboresha fursa kwa wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum ili kuongeza ushiriki wa makundi hayo katika mnyororo wa thamani wa madini.

"Naomba nichukue fursa hii kumpongeza Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye yeye alitupa maelekezo kuhakikisha vijana, wanawake na wenye mahitaji maalumu wanashiriki kikamilifu katika shughuli za madini.

Naupongeza Mgodi wa Barrick North Mara kwa kutoa Leseni kwa Vijiji 13 ambazo zitaendana na msaada wa kiufundi kwa Vijana zaidi ya 2000 watakanaonufaika na mradi huu.

 Tukio hili litasaidia kuondoa mahusiano hasi kati ya mgodi wa North Mara na wananchi wanaozunguka mgodi huo ambao walionekana mara kadhaa kuvamia mgodi huo.

Mradi huu wa kihistoria na wa kwanza kufanyika nchini baina ya serikali,Mgodi na wananchi wanaozunguka mgodi,umevutia ushiriki mkubwa wa wadau kama Benki ya Dunia(WB) na Baraza la Dhahabu Duniani(WGC) ambao wameonesha dhamira ya kusaidia utekelezaji wake.”Alisema Mavunde

Meneja Mkuu wa Mgodi wa North Mara Mhandisi Apolinary Lyambiko amesema utoaji wa Leseni hizo una lengo la kuimarisha uhusiano mwema na jamii inayozunguka  mgodi.

Akitoa salamu zake,Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini Mh. Mwita Waitara ameipongeza serikali pamoja mgodi kwa mradi huu ambao utatoa ajira nyingi kwa vijana wa Tarime na kuiomba serikali isaidie upatikanaji wa mitaji wa kuendesha shughuli za madini.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mara, Kanali Evance Mtambi amempongeza Waziri Mavunde kwa namna anavyo  wasaidia wananchi wa Mara hususan katika eneo la Sekta ya Madini ambapo amesema juhudi za Waziri huyo zinaonekana kwa vitendo na kuomba vijana hao wajengewe uwezo ili waweze kuchimba kwa tija.

Sambamba na hayo, Kanali Mtambi amemuomba Waziri Mavunde kutoishia kwenye utoaji wa leseni pekee bali pia kuliangalia suala la msaada wa kiufundi pamoja na mitaji ili kuwawezesha wachimbaji hao kufanya kazi kwa tija.

Naye, Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo Tanzania (FEMATA), John Bina amempongeza Waziri Mavunde kwa kuzindua mradi huo na kuwataka vijana, wanawake na wenye mahitaji maalumu kufanya kazi kwa kushirikiana na kuepuka migogoro isiyo ya lazima.











NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

 SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS), limebaini mafuta ya kupikia yaliyosababisha athari kwa  wakazi wa eneo la Yombo Dovya, Jijini Dar es salaam, yalikuwa yameharibika na ndani yake kubeba aina mbili za kemikali ambazo kitaalamu ni (E,E)2,4-Decadienal na decena. Kemikali hii hutokana na mafuta hayo kupikwa katika joto kali.

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI,  Mhe. Mohamed Mchengerwa ni miongoni mwa viongozi waliohudhuria  jukwaa la uchumi Arusha linalofanyika katika Ukumbi wa IACC Arusha.

Kongamano hili limejumuisha zaidi ya wadau 1000 kutoka maeneo mbalimbali duniani na kushirikisha mawaziri kadhaa wa sekta za tofauti.

Mwanamajumui wa Afrika Profesa Patrick Lumumba  pia amealikwa kuwa miongoni mwa watoa mada.

Jukwaa hilo limeandaliwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Paul Makonda ili kutoa fursa kwa wafanyabiashara wa Mkoa huo kupata ujuzi wa namna ya kutumia fursa za uchumi zilizopo mkoani Arusha.







Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Balozi Dkt.Pindi Chana (Mb) ameshiriki katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru katika uwanja wa Shule ya Msingi Idofi kwenye Kijiji cha Idofi, Halmashauri ya Mji wa Makambako, Mkoani Njombe leo Mei 3,2025.

Akizungumza katika mapokezi hayo, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Anthony Mtaka amesema Mwenge huo utakimbizwa  jumla ya kilomita 869.7 kwa muda wa siku sita katika Wilaya nne za Mkoa wa Njombe ambapo utazindua, kukagua, kufungua, kugawa na kutembelea jumla ya miradi 62 yenye thamani ya shilingi bilioni 17.6 Mkoani humo.

Mwenge huo uliongozwa na Kiongozi wa  mbio za Mwenge wa Uhuru 2025 Bw. Ismail Ali Ussi kutoka Unguja Kaskazini.










 


OR-TAMISEMI

Mkurugenzi wa Idara ya Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii, Ofisi ya Rais TAMISEMI Dkt. Rashid Mfaume amewataka watumishi wa afya katika ngazi ya msingi kuzingatia viwango (SOP) na ubora wa huduma za afya katika utekelezaji wa majukumu yao.

Dkt. Mfaume amesema hayo alipokuwa akikagua hospitali ya halmashauri ya manispaa ya ubungo katika ziara yake ya kikazi inayoendelea mkoani Dar es Salaam yenye lengo la kuangalia upatikanaji wa huduma za Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii.

“Wakati tunatoa hamasa kwa wananchi wanapokuja katika maeneo yetu kupata huduma lazima na sisi kama watendaji tuwe mfano kwa kuishi viwango vya ubora katika kutoa huduma bora na Salama” amesema Dkt.Mfaume

Amesema kwa kuzingatia viwango vya utoaji huduma katika maeneo ya kutendea kazi itasidia kumlimda mtoa huduma za afya na kumlimda mteja anayepokea huduma.

Aidha, Dkt. Mfaume amesema watumishi wanaofanyakazi kwa kukiuka misingi na viwango vya utoaji wa huduma za afya anafanya kosa kisheria kwani viwango hivyo vimekubalika kitaifa na kimataifa kupitia vyama vya taaluma na bodi taaluma zinazowasimamia watumishi hao.

Kamati ya Siasa ya halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi mkoa wa Njombe imetoa maelekezo kwa kamati za siasa wilaya zote mkoani humo kuwachukulia hatua wanachama na viongozi wote wa chama hicho wanaoandika maneno yenye kukejeli na kutukana viongizi mitandaoni.

Akitoa taarifa ya kikao cha kawaida cha kamati ya Siasa kilichofanyika mkoani humo,katibu wa Siasa na Uenezi mkoa wa Njombe Josaya Luoga amesema kikao hicho kilichokuwa na lengo la kujadili mambo mbalimbali ya Chama lakini pia kimetoa maelekezo hayo ili kudhibiti sintofahamu zinazotengenezwa na kuharibu kazi za Chama.

"Kamati ya Siasa ya halmashauri kuu ya mkoa imetoa maelekezo kwa kamati za Siasa  za wilaya na kamati za maadili kuhakikisha zinafanya kazi ya kuwaita watu wote wanaochapisha mitandaoni maneno yanayo ashiria kutengeneza sintofahamu kwenye makundi sogozi na kuwachukulia hatua"amesema Luoga

Amesema "Wale wote ambao wataonekana kweli wameandika na kuthibitika watachukuliwa hatua kali kuhakikisha chama kinakuwa tulivu kuelekea uchaguzi 2025 tuwapate viongozi ambao watakwenda kufanya kazi za wananchi kwa utulivu"

Luoga amewataka wanachama na viongozi wa Chama hicho kuchukua tahadhari na mandishi yanayochapishwa mitandaoni ambapo ametoa rai kwa wanachama kuandika maneno yanayolenga umoja na mshikamano wa Chama cha Mapinduzi.

 


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Innocent Bashungwa amelaani vikali tukio la kushambuliwa kwa Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padre Dkt. Charles Kitima na kuliagiza Jeshi la Polisi kumtafuta na kumhoji mtu aliyeandika kwenye mitandao ya kijamii kuwa "siku za Kitima zinahesabika",pamoja na watu wote waliohusika na uhalifu huo ili hatua kali za kisheria zichukuliwe.

“Naliagiza Jeshi la Polisi kumtafuta kwa haraka, yule mtu aliye-tweet kwenye mitandao ya kijamii kwamba, ‘siku za Kitima zinahesabika’. Mtu huyu atafutwe haraka, ahojiwe ametumwa na nani, na hatua kali za kisheria zichukuliwe haraka iwezekanavyo, kwa watu wote watakaobainika kuhusika katika tukio hili.” amesema Bashungwa.

Bashungwa amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa viongozi wa dini nchini katika kudumisha amani, mshikamano wa kijamii, na maadili ya Taifa.

“Tunalaani vikali shambulio hilo la kinyama dhidi ya kiongozi wa Dini na tunamuombea Padre, Dkt. Charles Kitima uponaji wa haraka na urejeaji salama katika majukumu yake muhimu kwa taifa” amesema Bashungwa.

Aidha, Bashungwa ameagiza Jeshi la Polisi kuwatafuta waliotengeneza na kusambaza waraka feki uliodaiwa kutolewa na Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), waraka ambao ulilenga kuchochea mgongano kati ya Kanisa na Serikali.

“Kumekuwepo na ‘Waraka feki’ uliosambazwa kwenye mitandao ya kijamii ukidaiwa ni waraka wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Baraza la Maaskofu Tanzania kupitia taarifa yake kwa umma imekanusha kuwa waraka huo haukutolewa na TEC, na kuwataka wananchi, waumini na watu wote wenye mapenzi mema kupuuza kabisa waraka huo” amesema Bashungwa

Ameeleza hayo, Mei 02, 2025  jijini Dodoma wakati wa hafla ya kuwaaga Watumishi wa umma waliostaafu kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani, ambapo alikumbusha kuwa Wizara hiyo ndiyo yenye dhamana ya kuhakikisha usalama wa raia na mali zao kupitia Vyombo vyake vya Usalama.

Bashungwa amewaelekeza Watendaji wote wa Wizara na vyombo vya usalama kutekeleza wajibu wao kwa weledi, kwa kuzingatia sheria, ili kulinda amani na usalama wa nchi.

“Naliagiza Jeshi la Polisi kuhakikisha uchunguzi wa kina unafanyika na kuchukua hatua zinazositahili dhidi ya wahalifu wanaotaka kuvuruga amani ya nchi yetu” amesisitiza Bashungwa.

Vilevile, Bashungwa amekemea vikali vitendo vyote vinavyochafua taswira ya taifa, vikiwemo vya kudhuru watu au kusambaza taarifa zenye kuchochea uhasama wa madhehebu ya  kidini.

“Ni wakati muafaka sasa, Jeshi la Polisi kuongeza kasi ya kusimamia sheria zinazohusu mitandao ya kijamii ili kuhakikisha watu wote wanatii sheria bila shuruti na hivyo kuendelea kuwa na jamii yenye ustaarabu na kuheshimu utu wa kila mtanzania na hata mgeni” amesisitiza.

Amewahakikishia Watanzania kuwa nchi iko salama na kuwasihi kuendelea kutii sheria bila kushurutishwa, ili kudumisha hali ya amani, utulivu na usalama nchini.


 


Wanawake kikundi cha UMOJA kilichopo Wilaya ya  Mtama Mkoani Lindi wamejengewa uwezo na Mtaalam kutoka Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) juu ya ufugaji bora wa nyuki na uongezaji  thamani mazao ya nyuki ambapo wameweza kutengeneza bidhaa mbalimbali kama vile Sabuni, Mafuta ya kujipaka , mishumaa ambazo zinatokana mazao ya nyuki (asali na nta)

Bi Amina  Nandilika ambaye ni Mwenyekiti wa kikundi hicho amesema  mafunzo hayo Yana tija katika kuongeza kipato chao kwani awali walikua wakinufaika na asali pekee “ mafunzo haya yatatuwezesha kuandaa bidhaa nyingi zaidi kwa ubora wa juu” amefafanua Nandilika

Mtafiti kutoka TAWIRI  Bw. Jackson Vicent Kizeze amesema tafiti za nyuki zinazofanywa na TAWIRI kupitia Kituo cha utafiti wa wanyamapori Njiro zinalenga kupata taarifa za kisayansi zinazosaidia kuleta tija katika Sekta ya nyuki ambapo amewakaribisha wadau na jamii kuja TAWIRI ili kujifunza juu ya ufugaji bora wa nyuki na uongezaji thamani mazao ya nyuki.







 



MKUU wa Mkoa wa Simiyu Kenani Kihongosi amewataka viongozi na watumishi wa umma katika Mkoa huo kuhakikisha wanawatendea haki wanaowaongoza huku akieleza wazi hakuna sababu ya kutengenenezeaja ajali na kuumiza wengine.

Kihongosi ameyasema hayo alipokuwa Mgeni rasmi katika Maadhimisho ya Mei Mosi wilayani Maswa Mkoani Simiyu ambapo tukio hilo limefanyika Kimkoa

“Niombe viongozi tuwatendee haki wenzetu pindi tunapopewa fursa ya kuongoza wengine ,asitokee mtu yeyote akamuumiza mtu na usiruhusu mtu akaharibikiwa ndani ya mikono yako .Usiruhusu kalamu yako ikamuonea mtu kumharibia maisha yake ya kazi.

“Viongozi tunawajibu mmoja kulea,kuelimisha,kuonya na kufundisha lakini kuwasaidia wale ambao wanachangamoto ili kuwa bora zaidi .Kwahiyo nitoe mwito ndani ya taasisi za umma ,halmashauri na maeneo mengine tuwatendee watu haki kama Rais Dk.Samia Suluhu Hassan anavyosisitiza.

“Itakuwa kosa kubwa sana endapo umepewa fursa ya kuongoza uoamuonea mtu tambua unaeneza laana kwako na kizazi chako,”amesema alipokuwa akitoa hotuba yake kwa wafanyakazi wa Mkoa huo.

Pia amesema wafanyakazi wanawajibu wa kuisadia nchi yetu pamoja na serikali yetu kwa kufanya Kazi kwa bidii lakini wakumbuke Taifa linawategemea na kufafanua wote ni mashahidi kuna watu maelfu kwa maelfu wanatamani kupata nafasi ambazo wamezipata wao lakini hawajapata hiyo fursa hiyo.

“Leo Mungu amekupa fursa hii itumie vizuri kwa ajili ya watu, fanya kazi bila kuchoka pale kwenye changamoto tuwasiliane ,viongozi wapo ili wananchi wanufaike na matunda ya Serikali yao.Kama wewe mganga mkuu wa Wilaya na kwenye hospital yako kukawa na malalamiko mengi maana yake unaigombanisha Serikali na wananchi.

“Kama ni Mkuu wa idara , mkuu wa kitengo au taasisi kukawa na malalamiko maana yake utendaji kazi utashuka na utendaji ukishuka wananchi wataishutumu Serikali lakini Serikali imekupa fursa ya kuwatumikia wananchi.

“Niombe sana kwa dhati ya moyo wangu kila aliyepewa kipande cha kwenda kufanya kazi akaifanye hiyo kazi bila kumpendelea mtu, bila kumuonea mtu na tujue kazi tulizonazo ni za muda utaondoka atakuja mwingine.

“Hivyo tuifanye kazi kwa uadilifu, mimi leo ni Mkuu wa mkoa na kabla sijaja alikuwepo mkuu wa mkoa maana yake nitaondoka na atakuja mwingine na hivyo hivyo kwa nafasi nyingine .Nafasi hiyo hutakuwa nayo milele,muombe Mungu akupe hekima,tumikia watu ili upate baraka kwa midomo itakavyokuwa inataja jina lako.”

Kihongosi amesema wakizingatia hayo watakuwa na Mkoa bora ,watakuwa watumishi bora zaidi na kwamba maeneo mengi ya kazi kumekuwepo na vitu haviko sawa. Kuna baadhi ya watu wanatabia ya kutengeneza chuki ndani ya viongozi na watumishi.

“Tabia ya kutengeneza majungu, uchonganishi ,uongo na kuwatengenezea wenzao ajali waonekane bora na wenzao waharibikiwe ,hatuna sababu ya kuumizana,matamanio yetu wote tuwe bora.

Ndio maana wakati nimekuja nilisema sitaki mtu yoyote aniletee habari ya Mtu mwingine bali nitazijua mwenyewe kwa kufanya naye kazi.

"Kwanini nasema hivi nimeshuhudia watu wengi wakiumizwa kwasababu ya midomo ya watu,watu wengi wanaonewa kwasababu hawana sauti ya kujitetea ,watu wengi wanaimiza kwa kutengeneza fitna hapa kati kati .Niombe viongozi na watumishi tutendeane haki , tupeane nafasi ya kusikilizana, tuangalie Utu ni jambo la msingi sana.”

 


Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kauli moja wamepitisha kwa kishindo Bajeti ya Ofisi ya Wizara kwa Mwaka wa Fedha 2025/26 yenye takribani Shilingi bilioni 224.98 kwa ajili ya wizara na taasisi zilizo chini yake kutekeleza majukumu yake.

Bajeti hiyo iliyopitishwa kwa uungwaji mkono mkubwa kutoka kwa wabunge, inalenga kuendeleza utekelezaji wa miradi ya kimkakati katika Sekta ya Madini pamoja na kuimarisha utoaji wa huduma na utendaji kazi wa wizara na taasisi zake.

Awali, Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde akiwasilisha Hotuba ya Mpango wa Mapato na Matumizi ya Wizara ya Madini kwa Mwaka wa Fedha wa Serikali wa 2025/2026 leo Mei 02, 2025 Bungeni Jijini Dodoma, ameeleza Bunge kuwa kiasi hicho ni kwa ajili ya kuwezesha Wizara ya Madini na taasisi zake kutimiza majukumu na wajibu wao.

“Mheshimiwa Spika, ili Wizara iweze kutekeleza majukumu na malengo yaliyopangwa ikiwemo ukusanyaji wa maduhuli ya shilingi 1,405,537,268,755.00 (Trilioni 1.4) naomba Bunge lako Tukufu liridhie na kupitisha makadirio ya shilingi 224,984,150,000.00 kwa ajili ya matumizi ya Wizara na Taasisi zake kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026” ameeleza Mavunde.

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, mchanganuo wa bajeti hiyo, Shilingi 124,604,788,000.00 (Bilioni 124.6) sawa na asilimia 55.38 ya bajeti yote imetengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ambayo inalenga kuleta tija na kuchochea ukuaji wa sekta ya madini hapa nchini.

Ameeleza kuwa, Shilingi 100,379,362,000.00 (bilioni 100.3) sawa na asilimia 44.62 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida, ambapo kati ya hizo, Shilingi 24,268,585,000.00 zimetengwa kwa ajili ya mishahara ya watumishi (PE) huku Shilingi 76,110,777,000.00 ikitengwa kwa ajili ya matumizi mengineyo (OC) ya Wizara pamoja na taasisi zilizo chini yake.

Kupitishwa kwa bajeti hiyo kwa kauli moja kunatoa ishara ya dhamira ya Serikali kuendelea kuwekeza kwa nguvu katika sekta ya madini ili kuhakikisha inachangia kikamilifu katika uchumi wa taifa na ustawi wa wananchi.

Katika hotuba yake, Waziri Mavunde ameeleza Wizara kuja na Programu maalum ya “Mining for a Brighter Tomorrow (MBT)” inayolenga kuhamasisha ushiriki wa makundi ya wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum kwenye mnyororo mzima wa shughuli za madini.

Aidha, kupitia, maono ya Vision 2030; Madini ni Maisha na Utajiri, Wizara inalenga kuifanya sekta ya madini kuwa kichocheo cha maisha ya Watanzania kwa kufanya utafiti kina wa jiosayansi kwa kutumia teknolojia ya kisasa (airborne geophysical survey) ili kuongeza kanzidata ya jiololia ya nchi sambamba na kuunganisha sekta ya madini na sekta nyingine kama za maji, ardhi, afya, kilimo, kiuchumi n.k.

Katika eneo la Utafiti wa Kina na Teknolojia ya Kisasa, Waziri Mavunde amesema, Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST) itaongeza utafiti wa jiofizikia kwa njia ya ndege hadi kufikia 34% ya eneo la nchi ifikapo 2026, sambamba na Ujenzi wa maabara mpya ya kisasa (State-of-the-Art Geoscientific Laboratory) Dodoma utaongeza uchunguzi wa madini ya kisasa kama lithium, nickel, cobalt lakini pia ununuzi wa Helicopter itakayofungwa vifaa maalum vya kisasa kwa ajili ya utafiti na vifaa vya kisasa vinanunuliwa kuharakisha ukusanyaji wa taarifa.

Vilevile, Waziri Mavunde ameeleza mpango wa Serikali kuendelea kuboresha mazingira kwa wachimbaji wadogo kwa kuwaunganisha na taasisi za kifedha na mabenki ili waweze kupata mikopo na kukuza mitaji yao, kuwapatia teknolojia za kisasa za uchimbaji na uchakataji madini, elimu na maeneo ya uchimbaji na hivyo kuendesha shughuli zao kwa tija Zaidi.

Pia, Wizara ya Madini itaendelea na mkakati wake wa kujenga mfumo wa kidijitali kwa ajili ya kusimamia Sekta ya Madini kwa ufanisi na tija na kwa manufaa ya kiuchumi na taifa kwa ujumla.



 


Na WAF - Handeni, Tanga

Waziri wa Afya Mhe. Jenista Mhagama amewataka wamiliki  wa vyuo vya afya nchini kudahili idadi ya wanafunzi kulingana na uwezo wa chuo ikiwemo miundombinu ya darasani pamoja na kwenye maabara za mafunzo kwa vitendo ili kuwa na ubora wa elimu kwa vyuo hivyo. 

Waziri Mhagama amesema hayo leo Mei 2, 2025 akimwakilisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Isdor Mpango kwenye hafla ya mapokezi ya Chuo Cha Afya cha Mafunzo ya Taaluma ya Uuguzi na Ukunga kilichofadhiliwa na Shirika la Hisani la Sheikh Abadallah Alnouri kutoka nchini Kuwait kilichojengwa  wilaya ya Handeni Mkoani Tanga.

"Tunaendelea kutoa angalizo kwa vyuo vyote vya afya nchini, pale vyuo vyetu vinapoanza kutoa mafunzo ni lazima vihakikishe vinakuwa na maabara za kujifunzia kwa vitendo kabla mwananfunzi hajaenda kumhudumia mgonjwa ili kujiimarisha kwenye mafunzo," amesema Waziri Mhagama.

Aidha, Waziri Mhagama amevitaka vyuo hivyo kupata hospitali kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo inayotosheleza mahitaji ikiwa ni pamoja na Chuo cha Afya cha Mafunzo ya Taaluma ya Uuguzi na Ukunga walichokipokea leo ambacho kipo karibu na Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Handeni ili wanafunzi waweze kufika katika hospitali hizo ambazo wanaweza kujijengea uwezo. 

Vilevile, Waziri Mhagama amewataka wamiliki, wakufunzi na wanafunzi kuendelea kusimamia maadili na miiko inayotakiwa kuzingatiwa wakati wa mafunzo ya Sekta ya Afya pamoja na wakati wa utendaji kazi kama watumishi wa afya ili kuifamya Sekta ya Afya kuendelea kutoa mchango unaohitajika katika ujenzi na uimara wa Taifa. 

"Leo kwa heshima kubwa tunakubaliana kuwa, tuna kila sababu ya kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma bora za afya karibu na maeneo yao, hivyo Serikali itaendelea kufanya kila liwezekanalo kuboresha upatikanaji wa huduma bora za afya nchini," amesema Waziri Mhagama.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Buriani amesema mkoa huo umepokea jumla ya Shilingi Bilioni 72 za kuboresha huduma za afya ikiwemo ujenzi wa Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali pamoja na ununuzi wa vifaa tiba na dawa. 

"Lakini pia katika mkoa wetu Mhe. Waziri tumefanikiwa kupunguza vifo vya kina mama wajawazito kutoka vifo 55 katika kila vizazi hai 100,000 kwa mwaka 2021 hadi kufikia vifo 30 katika kila vizazi hali 100,000 kwa mwaka 2024," amesema Dkt. Batilda.

Naye, Mwenyekiti wa Sheikh Alnouri Charity Organization Bw. Jamal Alnouri amesema kwa kushirikiana na Serikali ya Kuwait wataendelea kutoa msaada kwa Serikali ya Tanzania hasa katika  Sekta ya Afya kwakuwa afya ni suala la msingi katika maendeleo.