Ujenzi wa jengo la ghorofa tatu (03) la Makao Makuu ya Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) unaoendelea jijini Arusha, ni hatua muhimu inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita katika kuimarisha miundombinu ya utafiti, uhifadhi na usimamizi endelevu wa rasilimali za wanyamapori nchini ambapo hadi sasa imetoa shilingi bilioni 2.5.
Jengo hilo linakuja wakati ambapo Tanzania inazidi kuimarisha nafasi yake kama moja ya mataifa yenye utajiri mkubwa wa wanyamapori na vivutio vya utalii barani Afrika ambapo imetwaa tuzo mbalimbali za kimataifa za utalii. Ujenzi huu ni juhudi za kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza uwezo wa TAWIRI kutekeleza jukumu kuu la Kufanya, Kuratibu na Kusimamia tafiti za wanyamapori nchini.
Mkurugenzi Mkuu TAWIRI, Dkt. Eblate Mjingo ameishukuru Serikali kwa kuwezesha ujenzi wa jengo la makao Makuu ya Taasisi hiyo unaoendelea ambapo ndani ya jengo hilo kutakuwa na ofisi za watumishi, maabara za wanyamapori pamoja na kumbi za mikutano
“ Miundombinu hii itatoa mazingira bora zaidi kwa watafiti na watumishi wote kufanya kazi na kuendelea kutoa taarifa za kisayansi ambazo ni tija katika uhifadhi wa wanyamapori hapa nchini kwa utalii endelevu” amebainisha Dkt. Mjingo
Aidha, Ujenzi wa jengo hilo ulioanza Januari 5,2026 na unatarajiwa kukamilika 05/01/2028 utagharimu Bilioni 8.9 za Kitanzania na utachangia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambapo Sayansi na Teknolojia ni miongoni mwa vichocheo vitakavyo saidia hatua madhubuti za kuweka mazingira wezeshi kwa maendeleo ya sayansi na teknolojia katika kukidhi mahitaji ya jamii na uchumi endelevu.
Ikumbukwe kuwa TAWIRI ni Injini katika Maendeleo ya sekta ya Uhifadhi na Utalii.




Post A Comment: