Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi amesema Serikali imejipanga kuhakikisha wanawake wajasiriamali wanashiriki kikamilifu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050, hususan katika nguzo za uchumi imara, jumuishi na shindani pamoja na maendeleo ya jamii.

Ameyasema hayo tarehe 02 Februari 2026 Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Janeth Elias Mahawanga, ambalo liliuliza kuwa “Je Serikali imejipangaje kuhakikisha wanawake wajasiliamali wanashiriki moja kwa moja kwenye utekelezaji wa dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050”?

Akijibu swali hilo Mhe. Mahundi amesema Serikali imeweka mikakati mbalimbali itakayowawezesha wanawake wajasiriamali kushiriki moja kwa moja katika maendeleo ya taifa kupitia shughuli za kiuchumi.

Mhe. Mahundi amesema mikakati hiyo inalenga kupunguza vikwazo vinavyowakabili wanawake katika upatikanaji wa mitaji na masoko ili kuongeza uzalishaji na ushindani wa bidhaa na huduma zao.

Mhe. Mahundi ameongeza kuwa Serikali inaendelea kubuni na kutekeleza jitihada mahsusi za kuwawezesha wanawake na wanaume kunufaika na fursa za kiuchumi, ikiwemo utekelezaji wa majukwaa ya uwezeshaji wanawake kiuchumi pamoja na kuwapatia mafunzo ya ujasiriamali, matumizi ya teknolojia na viwanda vidogo na vya kati.

"Hatua hizo zitasaidia biashara za wanawake kukua, kuongeza ajira na kuchangia kikamilifu katika uchumi wa taifa kuelekea kufikiwa kwa malengo ya Dira ya Maendeleo 2050." amesema Mhe. Mahundi 

Share To:

Post A Comment: