Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amemtaka mkandarasi anayejenga barabara ya Kikombo – Chololo - Mapinduzi inayokwenda kwenye Makao Makuu mapya ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kukamilisha kazi hiyo ifikapo Desemba mwaka huu.
Ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 16.4 kwa kiwango cha lami umekuwa ukisuasua kutokana kwa kile kinachoelezwa kuwa ni upungufu wa wafanyakazi na mitambo ya ujenzi.
Ulega ametoa maelekezo hayo jijini Dodoma wakati wa ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa barabara hiyo akiwa amefuatana na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Stergomena Tax pamoja na Mnadhimu Mkuu wa JWTZ, Luteni Jenerali Salum Haji Othman na watendaji wengine wa wizara yake.
“Tumekagua barabara hii na sijaridhishwa na kasi ya utekelezaji wake. Natoa maelekezo mahususi kwa barabara hii, mkandarasi afanye kazi usiku na mchana, aongeze vifaa na mitambo ya ujenzi lakini pia azalishe ajira kwa wakazi wa maeneo haya ili barabara hii ikamilike kwa viwango na muda tuliompa kimkataba”, amesema Ulega.
Waziri Ulega amemuagiza mkandarasi ambaye ni kampuni ya CHICO kuhakikisha anaboresha mpango kazi wake ili aweze kukamilisha kazi zilizobakia zikiwemo ujenzi wa makalvati pamoja na madaraja katika barabara hiyo.
Aidha, Waziri Ulega amebainisha kuwa Serikali hivi sasa ipo katika hatua za mwisho za manunuzi za kumpata mkandarasi wa kujenga barabara ya njia nne na sita kuanzia Chamwino Ikulu hadi katikati ya jiji la Dodoma.
Kwa upande wake, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dkt. Stergomena Tax ameeleza kuwa ni matumaini yake ujenzi wa barabara hiyo utakamilika kwa muda uliopangwa na ikiwa na ubora na viwango vinavyotakiwa.
Naye, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Alhaj. Jabir Shekimweri amewashukuru Mawaziri hao kwa kufika na kukagua hatua za barabara hiyo kwani lengo la barabara hiyo ni kuleta muunganiko na ukaribu kati ya Wilaya za Dodoma Mjini na Chamwino hivyo utachochea maendeleo katika maeneo husika.
Akitoa taarifa ya mradi huo, Mkurugenzi wa miradi kutoka TANROADS, Mhandisi Japherson Nnko amewahakikishia mawaziri hao kuusimamia kwa karibu utekelezaji wa ujenzi wa barabara hiyo ili ikamilike kwa muda uliopangwa ambapo hadi sasa umefikia asilimia 51.
Post A Comment: