Mratibu wa mahusiano ya jamii EACOP Mkoa wa Shinyanga Bi. Cecilia Nzeganije akieleza hatua mbalimbali za maendeleo katika mradi wa bomba la mafuta ghafi katika Wilaya ya Kahama.

Na Mapuli Kitina Misalaba

Afisa mahusiano wa mradi wa bomba la mafuta ghafi Tanzania (EACOP) leo wametoa semina ya siku moja kwa waandishi wa habari Mkoa wa Shinyanga kuhusu hatua mbalimbali za maendeleo ya mradi huo.

Semina hiyo imefanyika katika ukumbi wa Empire mjini Shinyanga ambapo mkuu wa kitengo cha mawasiliano kwenye mradi huo Bi. Catherine Mbatia amesema mpaka sasa mradi huo umefikia takribani asilimia 29 na kwamba shughuli zinaendelea  katika maeneo mbalimbali Nchini.

Amesema mradi huo umefikia takribani asilimia 99 katika hatua za ulipaji fidia kwa wananchi huku akieleza kuwa suala la ajira linazingatiwa zaidi akwa kupewa  kipaumbela wazawa wa eneo husika kama sehemu ya kuwainua kiuchumi.

“Mpaka sasa hivi mradi umeshafikia takribani asilimia 29 na shughuli zinaendelea katika maeneo mbalimbali lakini katika ulipaji wa fidia tumeshafikia zaidi ya asilimia 99 hamna mtu ambaye mradi wake utapotea katika mradi mafanikio ya wazi ambayo kila mtanzania ni rahisi kuyaona ni ajira kuna kitu tunaita local content ambacho kinawashirikisha wazawa kwahiyo kama kuna kazi hapa Shinyanga inayohusiana na mradi mtu wa kwanza atakayefikiriwa kupata kazi hiyo ni mzawa wa hapa Shinyanga hiyo ni faida moja wapo kubwa sana lakini pia patachamgamsha maendeleo ya hapa Shinyanga kwa sababu kutakuwa na mzunguka wa fedha”.

“Mradi huu unatoa fursa mbalimbali za kiuchumi na kibiashara katika hatua za awali za mradi (early works), wakati wa ujenzi (Construction) na wakati wa uendeshaji wa mradi (operations), Mradi pia unatoa fursa kwa watanzania kupitia makampuni ya watoa huduma kujiandikisha katika kanzi data ya EWURA ambaye ni mdhibiti wa mkondo wa chini na kati katika sekta ya uziduaji na vilevile kwa watanzania kujiandikisha kupitia kanzidata ya nguvukazi iliyopo Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu kupitia kitengo cha TaESA”. amesema Bi. Catherine

Afisa mawasiliano wa nje EACOP nchini Tanzania Bwana Abbas Nassoro Abraham amesema mradi wa bomba la mafuta nchini Tanzania utapita katika  Mikoa nane ambayo ni  Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora, Singida, Dodoma, Manyara pamoja na Tanga.

Bwana Abraham ametumia naafsi hiyo kuwakumbusha wananchi kuendelea kuunga mkono jitihada zinazofanyika katika utekelezaji wa mradi wa bomba la mafuta ghafi ikiwa ni pamoja na kulinda miundombinu katika maeneo ambayo  bomba hilo linapita.

Kwa upande wake mratibu wa mahusiano ya jamii EACOP Mkoa wa Shinyanga Bi. Cecilia Nzeganije amesema mradi wa bomba la mafuta kwa Mkoa wa Shinyanga umepita katika Wilaya ya Kahama na kwamba zaidi ya watu mia sita wamenufaika na mradi huo.

“Urefu wa bomba ni kilomita 54.72 kilomita hizo zinapita kwenye kata nane (8) pamoja na vijiji na mitaa 16 ambapo kwa eneo hili la kilomita 54. 72  tunaidadi ya waguswa 619 katika hawa wote waguswa 619 utwaaji wa ardhi umekamilika kwa silimia 99 kwa sababu waguswa 609 tayari wamekwisha pokea malipo yao ya fidia  kwa mujibu wa sheria  na wengine kumi ni wale wenyechangamoto na wengina wamesafiri ama kuna kesi kwenye mabaraza la ardhi ambapo hawa mchakato wao utakamilika mara tu baada ya kukamilisha au kutatua changamoto zilizopo”.

“Lakini pia kwenye Wilaya ya Kahama tunawaguswa 12 ambao walipoteza makazi yao lakini katika hao 12, kumi walichagua kujengewa nyumba wakati wawili walichagua kulipwa fedha ili waende wakajenge wenyewe, wale ambao walichagua kujengewa nyumba ambao ni 10  tayari wamejengewa nyumba lakini zimejengwa nyumba 12 kwa Wilaya ya Kahama  ambapo yatari waguswa hawa walikabidhiwa nyumba zao mwaka jana Mwezi wa nane walikabidhiwa nyumba zao na mkuu wa Wilaya ya Kahama na kupewa muda wa matazamia ya Mwaka mmoja kwamba wakipata changamoto yoyote basi mradi unawatumia wakandarasi wake kurekebisha changamoto bure”.

“Pia Wilaya ya Kahama tulikuwa na makaburi 25 na yote yamehamishwa na uhamishwaji huo wa makaburi ulihusisha mila na desturi za familia zinazomiliki makaburi hayo hakukuwa na changamoto yoyote maana yote yaliweza kuhamishwa salama, sambaba na hayo pia tunazoezi la kuendelea kuwapatia chakula wakuswa zoezi hilo lilianza Mwaka jana Mwezi wa kumi lakini tunawataalam mbalimbali kutoka Manispaa ya Kahama ambao ni watumishi wa serikali ambao tunafanya nao kikao kila robo ya Mwaka  tunajadili kwa pamoja kwamba tufanye nini lakini pia tunamfumo wa kupokea, kusikiliza na kutatua malalamiko ya watu”.amesema Bi. Cecilia

Nao baadhi ya waandishi wa habari kutoka Klabu ya waandishi wa habari ( SPC) Mkoa wa Shinyanga wamepongeza na kushukuru kwa semina hiyo ambapo wameahidi kutumia kalamu zao kuelimisha jamii juu ya  hatua mbalimbali zitakazokuwa zinafikiwa katika mradi huo.

Bomba la Mafuta la Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), Huu ni mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) kutoka Kabaale – Hoima nchini Uganda kwenda kwenye peninsula ya Chongoleani mkoani Tanga nchini Tanzania.

Mradi huu una urefu wa jumla ya kilomita 1443 kati ya hizo kilomita 296 zipo nchini Uganda na kilomita 1147 zipo Tanzania na kwamba Bomba hilo vilevele linapita katika Mikoa 8 lakini pia wilaya 24, kata 134 na vijiji zaidi ya 180.

Lengo la mradi huu ni kuwezesha mafuta yatakayozalishwa nchini Uganda kusambazwa katika soko la ndani na sehemu inayobaki kuuzwa nje kwenye soko la kimataifa kupitia bomba la mafuta.

 Mkuu wa kitengo cha mawasiliano kwenye mradi wa EACOP, Bi. Catherine Mbatia akizungumza kwenye semina na waandishi wa habari wa Mkoa wa Shinyanga leo Juni 7, 2024.

Afisa mawasiliano wa nje EACOP nchini Tanzania Bwana Abbas Nassoro Abraham akiwasilisha mada yake kwa waandishi wa habari wa Mkoa wa Shinyanga katika ya semina ya leo Juni 7,2024.

Mratibu wa mahusiano ya jamii EACOP Mkoa wa Shinyanga Bi. Cecilia Nzeganije akieleza hatua mbalimbali za maendeleo katika mradi wa bomba la mafuta ghafi katika Wilaya ya Kahama.



Share To:

Misalaba

Post A Comment: