Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mh. Paul Christian Makonda amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Arusha kutenga barabara maalumu katikati ya jiji, itumike kwaajili ya Maonesho ya kibiashara kwa wajasiriamali wa mavazi ya asili, Picha, Vinyago na bidhaa nyingine za Urembo kuelekea kwenye kilele cha siku ya wafanyakazi duniani.

Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa amemuagiza Mkuu wa Wilaya Mh. Felician Gasper Mtahengerwa kuwa barabara hiyo iwe pembezoni mwa Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, uwanja uliotengwa kwaajili ya kutumika kwenye sherehe za Mei Mosi, akitaka ianze kutumika Jumatatu ya wiki ijayo.

Mkuu wa Mkoa Ametoa kauli hiyo leo Aprili 27,2024 wakati kikao kazi na viongozi wa Chama cha Wafanyakazi na kamati mbalimbali za maandalizi ya sherehe za wafanyakazi ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mh. Makonda amesema wananchi wa Mkoa wa Arusha wanapaswa kunufaika na shughuli mbalimbali za kitaifa zinazofanyika Mkoani hapa na hivyo kuwataka wananchi kujiandaa kutumia fursa zinazotokana na ugeni ambao tayari umeshaanza kuwasili Jijini Arusha kujiandaa na sherehe hizo.

Katika hatua nyingine Mh. Mkuu wa mkoa amewahakikishia usalama wa kutosha wakazi wa Arusha na wageni wote wanaofika mkoani Arusha kwenye shamra shamra za kuelekea kwenye Kilele cha siku ya wafanyakazi duniani.

Mheshimiwa Mkuu wa mkoa ametumia fursa hiyo pia kuwaomba wananchi wa Arusha na mikoa jirani kujitokeza kwa wingi katika sherehe hizo za Mei Mosi kama sehemu ya kuwaenzi na kuenzi kazi nzuri zinazofanywa na watumishi na wafanyakazi mbalimbali.

Katika Kikao hicho Mkuu wa mkoa pia ametangaza kuanza kwa shamra shamra za kuelekea siku ya wafanyakazi ikiwemo michezo ya sarakasi na vikundi mbalimbali vya sanaa ambavyo vitakuwa vikizunguka maeneo mbalimbali ya Jiji la Arusha.

Kwa Upande wake Rais wa Vyama vya wafanyakazi TUCTA Bw.Tumaini Nyamhokya amemshukuru Mkuu wa Mkoa kwa ubunifu wake kwenye kukoleza shamra shamra za Mei Mosi mwaka huu akiutaja ujana wake kama silaha muhimu iliyoongeza mambo mengi mapya kwenye sherehe za mwaka huu jijini Arusha.

Nyamhokya ametumia fursa hiyo pia kutangaza kuhusu mbio za marathoni zitakazozinduliwa kesho jumapili Aprili 28, 2024 na kuwaalika wananchi kushiriki kama sehemu ya shamrashamra za kuelekea kilele cha Mei Mosi.

Share To:

Post A Comment: