Mkuu wa mkoa wa Arusha Paul Makonda ametoa wito kwa wakazi wa mkoa huo na viunga vyake kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye kilele cha siku ya wafanyakazi Duniani (Mei mosi) inayotarajiwa kufanyika kitaifa Mei 01.2024 kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha

Makonda ametoa wito huo leo, Jumamosi Aprili 27.2024 alipokuwa kwenye kikao kazi cha maandalizi kuelekea siku ya wafanyakazi Duniani kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Arusha ambapo amesema uwepo wa shughuli hiyo ya kitaifa mkoani humo ni fursa kubwa kwa wakazi wake, na kwamba  katika kuchangamkia fursa hiyo uongozi wa mkoa huo umeandaa eneo maalumu (Barabara) kando ya uwanja wa Sheikh Amri Abeid kwa ajili ya kutumiwa na wajasiriamali mbalimbali kufanya biashara zao

Amesema uwepo wa siku hiyo (Mei mosi) unaashiria uhuru na haki za wafanyakazi mahala pa kazi hivyo ni vyema wananchi wakatambua kuwa ushiriki wao utawaongezea morali watumishi katika kuihudumia jamii, ambapo katika hilo amewapongeza viongozi wa shirikisho la wafanyakazi nchini (TUCTA) kwa kazi kubwa wanayoifanya kuhakikisha siku hiyo inafana

Kwa upande wake Rais wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi Tanzania (TUCTA) Tumaini Nyamhokya amemshukuru Mkuu wa mkoa huyo kwa kuitisha kikao kazi hicho ambacho amedai kuwa kimeongeza msukumo na kasi kwa watumishi na wananchi kushiriki kikamilifu kwenye shughuli mbalimbali zinazofanyika mkoani humo kama sehemu ya shamrashamra za kuelekea siku ya wafanyakazi Duniani 

Ametaja baadhi ya shughuli zinazofanyika kuwa ni pamoja na mashindano ya michezo ya aina mbalimbali yanayoendelea kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, maandalizi ya riadha maalumu ya Mei mosi, pamoja na maonesho yanayoendelea kwenye viwanja vya General Tyre yaliyoandaliwa na Wakala wa usalama na afya mahala pa kazi (OSHA - Occupational Safety and Healthy Authority) ambayo yanatarajiwa kufungwa na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko Aprili 28.2024

Naye, Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha ACP Justine Masejo amewaeleza wanahabari kuwa Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama mkoani humo linaendelea kuimarisha usalama kwenye kila kona ya mkoa huo hivyo wananchi hawapaswi kuwa na mashaka yoyote ya kiusalama wakati huu ambao idadi ya watu imeongezeka maradufu kwenye jiji la Arusha na mkoa wote kwa ujumla wake.

Share To:

Post A Comment: