Waziri wa  Kilimo Hussein Bashe amesema Serikali kupitia Wizara ya Kilimo ina Mpango wa kuendeleza Kilimo cha umwagiliaji Cha Chai kwa kuwasaidia wakulima wadogo wadogo kuweka miundombinu ya umwagiliaji.

Kuhusu Bei ya chai Waziri Bashe amesema itabaki ile ile ya mwaka jana ya Sh 366.

Kauli hiyo ameitoa leo Jijini Dodoma wakati akizungumza kwenye mkutano Mkuu wa mwaka wa wadau zao la Chai.

Mkutano huo ulihudhuriwa wakulima wa zao la Chai,wakubwa,wadogo na wa kati, wazalishaji, wachakataji, wachanganyaji, wafungashaji, wafanyabiashara wa ndani na nje.

Washiriki wengine ni Wakuu wa Wilaya na Halmashauri zenye wakulima wa Chai nchini (Rungwe, Busokelo, Njombe, Ludewa, Mufindi, Kilolo, Muheza, Korogwe, Lushoto, Muleba, Bukoba na Tarime).

Waziri wa Kilimo,Hussein Bashe amesema Serikali imeweka mikakati ya kuliendeleza zao la Chai ambapo ina mpango wa kuajiri maafisa ugani 200 ambao watashughulika na wakulima wadogo wadogo wa zao hilo.

Waziri Bashe amesema Wizara ya kilimo inazifahamu changamoto zote za zao la Chai hivyo amezungumza na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo kuona namna bora ya kuajiri maafisa Ugani ambao watashughulikia zao hilo tu.

"Hawa maafisa ugani maalumu 200 watashughulikia wakulima wadogo wadogo wa zao la chai,"amesema Waziri Bashe.

Pia amesema amezielewa na kuzipokea changamoto zote hivyo waombe Mungu Wizara ya Fedha waweze kuwaelewa watakapoomba fedha.

Aidha amesema Serikali kupitia Wizara ya Kilimo ina Mpango wa kuendeleza Kilimo cha umwagiliaji Cha Chai kwa kuwasaidia wakulima wadogo wadogo kuweka miundombinu ya umwagiliaji.

"Changamoto zote tunazipitia tunataka sekta ya chai izidi kusonga mbele na niwaambie tutaendeleza majadiliano na Mohammed Enterprises kuhusu yale mashamba," amesema Waziri Bashe.


Naye,Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Gerald Mweli amesema bado Kuna changamoto za uzalishaji na bei ambapo Wizara inaendelea kuzitafutia ufumbuzi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Bodi ya Chai Tanzania Mary Kipeja amesema wana Mpango wa kujenga viwanda vitano vya Chai nchini.

Pia amesema wana Mpango wa kujenga mifumo ya umwagiliaji na wataanza Wilayani Njombe.

Kipeja amesema Mkutano huo hufanyika mara moja kila mwaka kwa lengo la kuwakutanisha wadau wote wa ndani na nje ya Tanzania kwa ajili ya kujadiliana kuhusu mafanikio, changamoto na fursa ili kubuni, kujadili na kuweka mikakati ya kuendeleza tasnia ya chai. 

Amesema katika mkutano wa jukwaa la wadau wa mwaka 2024, mada Kuu zitakazojadiliwa ni pamoja na,Kupitia muhtasari na taarifa ya utekelezaji wa maazimio ya mkutano mkuu wa wadau wa zao la Chai uliofanyika Januari 18, 2023 Mkoani Iringa.

Pia,Kuwasilisha taarifa ya mwenendo wa Tasnia ya Chai nchini ikiwa ni Pamoja na usajili wakulima wa zao la Chai,Uhamasishaji maendeleo ya Tasnia ya Chai.

Vilevile Uendelezaji wa zao la Chai katika Wilaya ya Kilolo Mkoani Iringa,Maendeleo ya mnada wa Chai wa kimtandao Dar Es Salaam, Hali ya ulipaji wa madeni sugu ya wakulima wa Chai nchini.

Pia,Hali ya uendeshaji wa viwanda vya uchakataji wa chai,Upatikanaji na usambazaji wa pembejeo za Chai (Miche bora, mbolea na viuagugu).

Kwa upande wake,Mwenyekiti wa kamati ya Kilimo,Viwanda na Mifugo,Deo Mwanyika amesema iko haja ya kuangalia wawekezaji wengine kutokana na baadhi ya waliopo kutokufanya vizuri.

Share To:

Post A Comment: