Na. Chrispin Kalinga – Njombe

Katibu Tawala wa Mkoa wa Njombe, Bi. Judica Omari leo tarehe 31 Januari, 2024 ameongoza kikao cha tathimini ya Utekelezaji wa Afua za Usafi wa Mazingira Mkoa wa Njombe ambapo hapo zimewasilishwa Taarifa mbalimbali kutoka halmashauri 6 za Mkoa wa Njombe ikiwa ni pamoja na Taarifa ya Utekelezaji wa Kampeni ya Usafi wa Mazingira, Taarifa ya Utekelezaji wa Udhibiti wa taka ngumu, Mfumo wa mnyororo wa utupaji wa kinyesi pamoja na Taarifa ya Mwelekeo wa Kampeni ya Usafi wa Mazingira Mkoa wa Njombe.

Kikao hicho kimefanyika katika Ukumbi wa Milimani Hotel uliopo Njombe mjini.

“Leo tupo hapa kwa ajili ya kufanya kikao cha tathimini ya Utekelezaji wa Afua za Usafi na Mazingira, mkoani kwetu hapa bado hatujakubwa na magojwa ya kuambukiza kama Kipindupindu, kwa ujumla hali ipo vizuri sana, lakini jambo moja muhimu sana la kuzingatia ni kuwekea mkazo siku ya usafi wa mazingira ambapo kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi wananchi washirikishwe kufanya usafi kwa dhati kabisa na wawe wanakumbushwa kila mnapokutana kwenye mikutano na kwenye nyumba za ibada,” amesema Bi. Judica Omari.

Ikumbukwe kwamba Mkoa wa Njombe ni Miongoni mwa mikoa inayofanya vizuri katika utekelezaji wa kampeni ya Usafi wa Mazingira, hadi kufikia Mwezi Desemba, 2023 hali ya matumizi ya Vyoo bora katika ngazi ya jamii (Kaya) ilifikia asilimia 86.9 na uwepo wa vifaa vya kunawia mikono kwa maji tiririka na sabuni ilikuwa ni asilimia 77.98 na Hivi karibuni Vijiji 133 kati ya 2013 vinatarajiwa kupata vyeti vya uthibitisho wa hali ya Usafi uliotakiwa na Wizara ya Afya.

Katika hatua nyingine Bi. Judica Omari amesema kuwa, anatambua mchango mkubwa unaofanywa na wadau wa maendeleo wakiwemo UNICEF kwa kusaidia uboreshaji wa maisha ya Watoto kwa kuhakikisha wanaishi na kusoma katika mazingira bora.

Na mwisho akamaliza kwa kuwaomba Wakurugenzi Watendaji wote wa Halmashauri za Mkoa wa Njombe wakiwakilishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa Ndg. Sunday Deogratias ambaye aliwakiliwa na Bw. Mathan Chalamila pamoja na Wataalumu mbalimbali kuandaa mikakati ya Utekelezaji ambayo itapelekea kupata matokeo chanya na yenye kulinda afya kwa jamii.

Share To:

Post A Comment: