Ujumbe wa Wizara ya Madini wa Serikali ya Jamhuri ya Zimbabwe ukiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa Uendeshaji kutoka Wizara hiyo, Charles Simbalache kwa niaba ya Katibu Mkuu pamoja na  Wataalam upo nchini kwa ziara ya Siku Tano yenye lengo la kujifunza kuhusu Mfumo wa Usimamizi wa Leseni za Madini Nchini (Mining Cadastre Information Management System – MCIMS).

Pamoja na masuala ya usimamizi wa leseni, ujumbe huo pia umeomba kutembelea na kujifunza kuhusu Kanuni za Usimamizi wa madini ya Uranium pamoja na shughuli za uchimbaji mdogo wa madini.

Akizungumza baada ya kuupokea ujumbe huo Ofisini kwake Mtumba jijini Dodoma, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Madini Msafiri Mbibo amesema ujio huo ni ishara njema kwa nchi za Afrika kuweza kubadilishana uzoefu katika usimamizi wa  rasilimali madini kwa manufaa na  maendeleo  ya nchi zao ikizingatiwa kuwa, kwa kiasi kikubwa nchi hizo zina ufanano wa jiografia, mila,  tamaduni  na desturi  na kuongeza  kwamba,  hali hiyo imekuwa tofauti na ilivyokuwa awali.

Ameongeza kwamba, ni vema nchi za Afrika zikaelekeza nguvu katika shughuli za uongezaji thamani madini katika nchi zao ili kuchochea uchumi wa viwanda unaotokana na rasilimali madini badala ya shughuli hizo kufanywa nje ya nchi zao.

Akizungumza katika kikao hicho, Simbalache amesema nchi hiyo imeona bado ina mengi ya kujifunza kutoka Tanzania kutokana na usimamizi madhubuti wa Sekta ya Madini ili kuiwezesha kupata matokeo zaidi yanayotokana na rasilimali madini.

Amesema pamoja  na kuwa  Sekta ya Madini  ya Zimbabwe  inachangia asilimia 13 katika Pato la Taifa ikichangiwa pia na shughuli za uchimbaji mdogo hususan dhahabu kuchangia asilimia 70, lakini nchi hiyo inaona bado ina mengi ya kujifunza kutoka Tanzania.



Share To:

Post A Comment: