OR- TAMISEMI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Mohamed Mchengerwa amewataka  Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya waliokabidhiwa magari ya usimamizi shirikishi kutoka Ofisini na kwenda kuwahudumia wananchi.

Waziri Mchengerwa ameyasema hayo leo wakati akikabidhi magari 13 kwa  ajili ya Usimamizi Shirikishi wa Shughuli za Afya kwa Mkoa wa Arusha (magari 5) na Manyara ( magari 8) katika hafla fupi iliyofanyika kwenye viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha.

"Ni lazima viongozi mfanye kazi za kuwatumikia wananchi haswa nyie Waganga Wakuu wa Wilaya mtoke ofisini nendeni field mkasimamie miradi ya Afya mkakague ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi  muwe na taarifa za vituo vyenu na kujua ubora wa huduma na sio kukaa ofisini kusubiria taarifa za kuletewa,"amesema.

Amesema hatasita kuwachukulia hatua za kinidhamu wale Waganga wote watakaothibika kusababisha vifo vya mama na mtoto kwa uzembe wakati vifaa vyote muhimu na miundombinu imeshaletwa na Serikali ya Awamu ya sita kwenye maeneo yao.

"Mhe. Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ameshatekeleza wajibu wake ameleta kila kitu, miundombinu bora, vifaa tiba, madawa na sasa ametupatia usafiri huu kwa ajili ya kuboresha utendaji kazi wetu sasa kwanini wewe usifanye kazi nendeni mkahudumie wananchi,"amesema.

Naye, Naibu Katibu Mkuu  anayeshulikia sekta ya Afya,  Ofisi ya Rais TAMISEMI, Dk. Wilson Mahera amesema "Ole wenu watumishi wa afya mnaofanya uzembe kwa wagonjwa tutachukua hatua na nyie wahudumu wa afya wenzenu wakichukuliwa hatua halafu nyie mkalalamika kuwa hawakustahili adhabu husika na nyie tutawachukulia hatua haiwezekani mgonjwa anataka huduma za afya halafu mnazembea na kupelekea vifo."

Waziri Mchengerwa anaendelea na ziara ya Kikazi kwenye Singida, Shinyanga, Kagera, Mwanza na Geita.


Share To:

Post A Comment: