Mkuu wa Idara ya  Mpango wa Uendelezaji wa Vipaji na Ajira kwa Vijana  wa Taasisi ya Uhasibu Tanzaia (TIA), Imani Matonya, akitoa mada kwa wanafunzi wapya wa  taasisi hiyo  Kampasi ya  Singida walioanza msimu wa masomo wa 2023/ 2024 yenye lengo la  kuwaandaa kukabiliana na changamoto ya upungufu wa soko la ajira iliyofanyika Novemba 16, 2023.

............................................................

 

Na Dotto Mwaibale, Singida

 

TAASISI ya Uhasibu Tanzaia (TIA), Kampasi ya  Singida imetoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wanafunzi wapya wa  Taasisi hiyo walioanza msimu wa masomo 2023/ 2024 kwa lengo la kuwaandaa kukabiliana na changamoto ya upungufu wa soko la ajira baada ya kumaliza masomo yao.

Akizungumza Novemba 16, 2023 kwenye mafunzo hayo Mkuu wa Idara ya Mpango wa Uendelezaji wa Vipaji na Ajira kwa Vijana wa Taasisi hiyo nchini, Imani Matonya  alisema Taasisi ya Uhasibu Tanzania imeanzisha mpango huo kwa malengo matatu moja likiwa ni kuwajengea uwezo wanafunzi na kuwasaidia kupata mbinu za kitaalam ambazo wanatakiwa kuwa nazo zaidi ya taaluma waliosomea.

Matonya alitaja lengo la pili ni kuwafundisha wanafunzi hao mbinu za kuwa wajasiriamali bora kwa kuwaruhusu kuonesha biashara mbalimbali wanazozifanya bila kujali ukubwa wa biashara hiyo hata kama watakuwa wanauza ubuyu.

"Sisi tunaamini ujasiriamali ni tabia na maarifa na ndio maana kuna baadhi ya watu wanatuambia inakuwaje tunafundisha masuala ya ujasiriamali lakini hatujishughulishi nao ndio maana utakuta kuna mtu hajasoma lakini ni mbobezi katika ujasiriamali," alisema Matonya.

Alisema jambo la tatu wanalolifanya ni kuchagiza ubunifu ili wanafunzi waweze kuja na utatuzi wa kitaalam kwenye mambo ya msingi yanayolikabili taifa letu na kuwa jambo la nne wanafanya uhatamizi wa mawazo bunifu mwanafunzi akiwa na wazo fulani la biashara wanampa nafasi ya kulihatamia na kumsaidia bure kupata usajili na mahitaji mengine kama ya kupata mwanasheria muhuri wa chuo hivyo kumrahisishia mambo yake,

Alisema kupitia mpango huo wamejipanga kutoa mafunzo hayo mara kwa mara kwa ajiliya kuwajengea uwezo wa kupata mawazo ya biashara ambayo yatawasiadia katika kujiajiri.

Alisema wanafunzi wenye mawazo mazuri watashindanishwa na mawazo yatakayoshinda yatapelekwa mbele zaidi kwa kutafutiwa mitaji na kukutanishwa na taasisi za kifedha ili waweze kupata mikopo ya kuanzisha biashara.

"Leo tumekuja Singida kuwaelekeza vijana kuhusu maisha yao kwa ujumla na kuwapa hamasa kwamba wanaweza kuwa bora na kuwajuza mambo mawili la kwanza ni suala la kujiajiri kupitia ubunifu na ujasiriamali na kuwafundisha namna ya kuandika mipango biashara inayoshinda ambayo watafundishwa na watu kutoka mitaani wenye ujuzi wa hayo mambo na wanayafanya kwa vitendo," alisema Matonya.

Alisema watu hao watawaeleza kwa vitendo na kuwapa chagizo la kuweza kushiriki kwenye mashindano mbalimbali ya kuomba ufadhili na kuwafanya wawe na ujasiri wa kusimama mbele ya wawekezaji kuwaomba waweke uwekezaji kwenye miradi yao.

Alisema vijana wengi wanamawazo mazuri na biashara nzuri lakini changamoto waliyonayo wameshindwa kuwavutia wawekezaji kwa sababu hawana mbinu za kuwasilisha wazo mbele ya watu wenye fedha na kuona kama mawazo yao yana tija kwa siku za usoni.

Matonya alisema lengo lingine la mpango huo ni kuwataka wanafunzi hao nini wategemee kutoka kwenye soko la ajira kwani wapo watakao jiajiri lakini kwa wale watakao taka kuajiriwa wanapaswa kuwa na vitu vya ziada ili iwe rahisi kupita kwenye usaili na kuchaguliwa kuingia katika ajira.

Alisema leo hii ikitangazwa nafasi moja ya ajira watajitokeza watu kuanzia 100 hadi 200 kuigombea nafasi hiyo hivyo ni lazima mgombea awe na vitu vya ziada ambavyo TIA wanavifundisha.

Naye Mwalimu wa Stadi za Mawasiliano na Lugha ya Kiingereza kutoka Chuo cha Utumishi wa Umma Singida Eliasi Mchomvu alisema hivi sasa soko la ajira limekuwa na changamoto ndio maana wapo TIA kwa ajili ya kuwafundisha wanafunzi hao mbinu za kufanya vizuri wanapofanyiwa usaili.

Alisema hivi sasa lugha ya kiingereza imekuwa ndiyo ya ajira lakini changamoto iliyopo watu wengi hawana uwezo mzuri kwenye lugha hiyo ambapo walifundishwa mbinu ambayo itawasaidia kuijua vizuri na kuwa wakati wanaomba kazi kuna baadhi ya vitu ni muhimu kuvizingatia.

Alisema jambo la kwanza wanapaswa kulisoma tangazo la kuomba kazi vizuri na hapo ndipo watapata muongozo wa kuomba hiyo kazi yenyewe na mtu atakayekuwa akifanya usaili atajua kuwa mwombaji ni mtu anayeelewa hivyo ni muhimu kuitwa kwenye usaili.

Alisema jambo la pili ni muombaji kuandika wasifu wake ambapo mtu akiusoma atajua aliyeuandika ameandika vitu vya msingi hivyo anafaa kuitwa kwenye usaili.

Mchomvu alitoa angalizo katika uandikaji wa wasifu wake kuwa ni vema akaandika maneno machache ya msingi badala ya kuandika maneno mengi ya kujisifia kwani ndio utakaoleta maswali mengi wakati wa mahojiano ya hana kwa hana na wasaili.

Aidha Mchomvu alishauri viandikwe vitu vya msingi ambavyo muombaji ataweza kuvijibu kwa ufasaha wakati wa mahojiano ya ana kwa ana kwani mara nyingi huwa inatokea mwombaji kuandika maneno mengi na wakati wa mahojiano anashindwa kuyatolea ufafanuzi.

Akielezea mtu anayeandikwa pale chini kuwa wanaweza kuwasiliana naye kwa maana anajua taarifa za muombaji wa kazi ' Refer ' alisema anatakiwa kuwa ni mtu mwenye vitu vya ziada vya muombaji ambavyo havipatikani kwenye vyeti wala kwenye wasifu wake na havitakuwepo mezani kwa watu wanaomfanyia usaili na amjue kwa undani muombaji.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Ksa arts and Decors Company, Allen Kazungu alisema licha ya kuwa mwanafunzi katika Taasisi hiyo akishirikiana na wenzake wawili waliweza kutumia jukwaa la shule kama fursa ya kuweza kupata mafunzo na kujiendeleza na kuweza kufungua kampuni hiyo.

Alisema mwanafunzi akiwa chuoni anapata fursa ya kushiriki majukwaa mbalimbali kiurahisi na bure na akitoka nje anaweza kuilipia kuanzia Sh.100,000 hadi 200,000 hivyo aliwashauri wanafunzi hao na vijana wengine popote pale walipo kwa hali na mtaji wowote walionao wanaweza kuukuza wakiwa chuoni kupitia walimu wa programu hiyo na kufungua kampuni zao.

Alisema kufungua kampuni na biashara ni jambo moja na kuwa  vijana wengi wanakuja kukwama na kushindwa kuendelea kwa kukosa muelekeo na mipango thabiti hasa pale wanapokutana na changamoto badala ya kupambana nazo wao hukata tamaa.

Mkufunzi wa Stadi za Mawasiliano na Lugha ya Kiingereza kutoka Chuo cha Utumishi wa Umma Singida Elias Mchomvu, akitoa mada kuhusu usaili kwa wanaoomba nafasi za kazi.

Mkurugenzi wa Ksa arts and Decors Company, Allen Kazungu , akizungumza kwenye mafunzo hayo.

Watoa mada wakiwa kwenye mafunzo hayo.

Wanafunzi wapya wa  TIA Kampasi ya Singida wakiwa kwenye mafunzo hayo.

Mafunzo yakiendelea.

Taswira ya mafunzo hayo.

Mafunzo yakiendelea.

Watoa mada wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Serikali ya Wanafunzi (TIASO) wa taasisi hiyo Kampasi ya Singida.


Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: