IMG-20231031-WA0039-1024x682

Serikali kupitia Wizara ya Afya inatarajia kurejea Bungeni tena hapo kesho Novemba 1,2023 na Muswada wa Bima ya Afya kwa wote ambao ulikwama mnamo Mwezi Februari 2023 kwa hoja iliyotolewa na Bunge ya kutokuwepo kwa chanzo endelevu cha fedha kutekeleza Mpango huo.


Muswada huu ni ndoto ya Serikali ya miaka mingi ambapo Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeboresha huduma bora za afya kuanzia ngazi ya Taifa hadi ya msingi kwa kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya karibu zaidi na maeneo yao. 


“Serikali kupitia Wizara ya Afya, Wadau wa Sekta na Wataalam wengine tayari wamefanyia kazi hoja zote zilizoibuliwa na Bunge pamoja na Wadau, hata hivyo semina zimefanyika kwa makundi mbalimbali ndani ya jamii kuhusu umuhimu wa Bima ya Afya kwa wote na tulipokea maoni yao na kuyafanyia kazi wananchi kesho watege macho na masikio yao Bungeni kujua nini ambacho Waziri wa Afya Mheshiwa Ummy Mwalimu atawasilisha Bungeni” Amesema Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Afya Bw. Englibert Kayombo 


  Amesema kuwa kupitishwa kwa muswada huu kutawezesha kila mtanzania kuwa ndani ya Mfumo wa Bima ya Afya hatua itakayoboresha zaidi upatikanaji wa huduma za matibabu bila kuwa na kiwazo cha fedha. Serikali yetu ni sikivu sana na imefanyia kazi hoja zote zilizoibuliwa na Waheshimiwa Wabunge ambao ndio wawakilishi wa wananchi hivyo yaliyomo ndani ya muswada huo yamelenga kuwasaidia wananchi kupata huduma bora za afya bila ya kikwazo cha fedha” alisema Bw. Kayombo.


Kuhusu gharama za vifurushi, Kayombo amesema kuwa mara baada ya Muswada huo kupita na kuwa Sheria, kanuni zitatungwa ili kuratibu suala ya gharama za vifurushi na kusema kuwa uchambuzi utafanyika ili vifurushi viwe vya gharama nafuu na kila mwananchi aweze kuwa na bima ya afya. 


Ameongeza kuwa kwa upande wa Serikali imeshakamilisha maandalizi ya kutoa huduma kwa wananchi kupitia mfumo wa bima ya afya kwa wote ambapo imeboresha ubora wa huduma katika vituo vyake vya kutolea huduma ikiwemo upatikanaji wa Dawa, ununuzi na usimikaji wa vifaa na vifaa tiba, ajira za watumishi. 


“Kwa sasa nchi yetu iko mbali sana katika utoaji wa huduma, tuna vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa magonjwa, huduma nyingi za kibingwa zinapatikana hapa hapa nchini lakini pia huduma za afya zimesogezwa sana kwa wananchi hivyo kama nchi tupo tayari kutekeleza hili, nia na uwezo wa kufanya hivyo tunao” amesema Bw. Kayombo.

Share To:

Post A Comment: