Na John Walter-Babati

Zaidi ya watu 50 wamenusurika kifo huku watatu wakijeruhiwa baada ya gari kampuni ya FREY'S COACH yenye namba T 137 DRE waliokua wamepanda kuyagonga magari mawili yaliyokuwa mbele yake.

Ajali hiyo imetokea katika kijiji cha Sigino wilaya ya Babati mkoani Manyara, ikihusisha basi hilo lililokuwa linatokea Shinyanga kwenda mkoani Tanga na Fuso namba T 303 ADL lililokuwa limebeba machungwa pamoja na Scannia namba T 967 DBU.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa mkoa wa Manyara, Dk Valerian Musamba akizungumza na kituo hiki amesema wamewapokea majeruhi watatu wawili wanaume na mmoja Mwanamke wenye umri kati ya miaka 19 hadi 25 wawili wakiwa wamevunjika miguu na mmoja majeraha madogo mwilini na wanaendelea na matibabu.

Afisa kutoka Jeshi la  Zimamoto na uokoaji wilaya ya Babati Sir.Meja Boniphasi Ndaiga akizungumza katika eneo la tukio amesema chanzo cha ajali hiyo ni mwendokasi wa dereva wa gari ya abiria ambaye alikuwa akijaribu kuyapita magari mawili yaliyokuwa mbele yake bila kuchukua tahadhari kwenye eneo lenye mteremko mkali.

Mwenyekiti wa kijiji cha Sigino Paulo Hussein na baadhi ya wananchi wamesema  matukio zaidi ya 20 ya ajali za barabarani yametokea katika eneo hilo miaka ya hivi karibuni.


Share To:

Post A Comment: