Naibu Waziri Maji, Mhandisi, Maryprisca Mahundi (kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Obinna Anyalebechi (kulia), wakifurahia baada ya uzinduzi wa mradi wa maji wa Kwamaizi, wilayani Handeni mkoani Tanga.

Naibu Waziri Maji, Mhandisi, Maryprisca Mahundi akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Obinna Anyalebechi, cheti cha kutambua mchango wa kampuni hiyo baada ya uzinduzi wa mradi wa maji wa Kwamaizi, wilayani Handeni mkoani Tanga. 

NAIBU Waziri wa Maji, Mhandisi, Maryprisca Mahundi ametoa pongezi kwa Kampuni ya Serengeti Breweries Limited (SBL) kwa mchango wake wenye bidii katika kufadhili miradi ya maji inayolenga kutoa maji safi na salama kwa watanzania katika maeneo ya vijijini yenye upungufu wa maji.

Hii inakwenda sambamba na juhudi za serikali za kuongeza upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo ya vijijini kufikia asilimia 85 ifikapo mwaka 2025.

Mhandisi Mahundi ametoa pongezi hizo hivi karibuni katika kata ya Kwamaizi, wilaya ya Handeni, mkoani Tanga wakati wa hafla ya kukabidhi mradi wa bwawa la maji kwa kata ya Kideleko baada ya kukamilika kwa mradi huo.

Utekelezaji wa mradi huu ulianza mwezi Februari mwaka huu kwa ushirikiano na WaterAid Tanzania na Wizara ya Maji kama watekelezaji wa kiufundi kwa msaada wa kifedha wa Tsh. Milioni 380 kutoka SBL.

Akiongea katika hafla hiyo, mhandisi, Mahundi amesema serikali inafanya kazi kwa bidii kujenga, kukarabati, na kupanua vyanzo vya maji ili kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama katika maeneo ya vijijini, hivyo jambo ambalo SBL imefanya ni la kupongezwa kwa sababu linakwenda sambamba na juhudi za serikali za kukabiliana na uhaba wa maji safi na salama katika maeneo ya vijijini.

"Nimefurahi kuona sekta binafsi ikiwa kinara katika kushughulikia masuala muhimu kama ukosefu wa upatikanaji wa maji safi na salama katika jamii zetu na sasa wakazi wa kijiji cha Kwamaizi watakuwa wanapata wa maji safi na salama bila malipo". Amesema Mhandisi Mahundi.

"Naipongeza sana SBL kwa kufadhili mradi huu kwa kiasi cha Sh. milioni 380, hivyo kuruhusu utekelezaji mafanikio wa miradi hii ndani ya miezi 5 tu," amesema Mhandisi Mahundi, akishukuru Water Aid, Handeni Trunk Main, na RUWASA kwa usimamizi wa utekelezaji wa mradi huo.

Aidha Mhandisi Mahundi amewapongeza SBL na WaterAid kwenda mbali zaidi kwa kutoa mafunzo kuhusu masuala yanayohusiana na huduma za usafi na maji (WASH) kwa wanawake wa Kwamaizi ili kuwapa ujuzi wa jinsi ya kusimamia bwawa la maji jambo ambalo inalingana na programu ya serikali ya ulinzi wa vyanzo vya maji 2021-2035.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Dkt. Obinna Anyalebechi amesema, ufadhili wa mradi wa Handeni uliotolewa na kampuni hiyo ni sehemu ya nguzo moja ya msaada wa jamii ya SBL inayojikita katika kutoa huduma ya maji kwa jamii zilizopokonywa rasilimali hiyo ijulikanayo kama 'Maji ni Uhai.

"Programu hii inalenga kurejesha au kujaza upya jamii sawa na kila tone la maji linalotumiwa na kampuni yetu katika shughuli zake, Mwaka huu, kwa mfano, tuna jukumu la kurejesha mita za ujazo 87,000 za maji, sawa na jumla ya maji yanayotumiwa katika viwanda vyetu vya bia vitatu vya huko Dar es Salaam, Moshi, na Mwanza," amesema Anyalebechi.

Aliongeza, "Tumeenda hatua ya ziada kwa kufadhili mafunzo ya maji na usafi (WASH) kwa wanawake walengwa katika eneo hili ambao sasa wana vifaa vya kutosha vya kushughulikia mradi huu na kuhakikisha kuwa unadumu kwa miaka mingi ijayo."

Naye, Anna Mzinga, Mkurugenzi wa WaterAid nchini Tanzania, amesema, "SBL imekuwa mmoja wa washirika wao muhimu katika utekelezaji wa miradi ya maji nchi nzima na kwamba utayari wao katika kusaidia kazi hiyo ni wa kuvutia.

"Kupitia ushirikiano wetu, zaidi ya Watanzania milioni mbili hasa katika maeneo ya vijijini kama Kwamaizi sasa wanapata maji safi, na salama bila malipo." Amesema Mzinga

"Mradi wa usambazaji maji wa bwawa la Kwamaizi ni mfano wa kile tulichokuwa tukifanya kwa miaka 40 iliyopita na kile tutakachokifanya kuendeleza malengo yetu lengo likiwa ni kusaidia kuleta maendeleo katika maisha ya watu, jamii na uchumi kwa kufanya maji, usafi na usafi wa mazingira kuwa jambo la kawaida kwa kila mtu na kila mahali" amesema.

Ameongeza kuwa kufanya hivyo kutaimarisha uwezo kwa njia ambazo zinadumu - kuweka kipaumbele kwenye mifumo endelevu, taasisi na huduma. Kwa pamoja, tuna dhamira, uzoefu, ubunifu wa rasilimali, na uhusiano wa kubadilisha maisha ya mamilioni zaidi.
Share To:

Post A Comment: