Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu amesema ni marufuku wananchi kutozwa fedha wakati wa kipimo cha malaria cha haraka, dawa za Alu, dawa za SP kwa wajawazito pamoja na sindano ya malaria kali.

Ametoa agizo hilo wakati akizungumza na wakazi wa Wilaya ya Kishapu ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku mbili ambayo imelenga kutembelea na kukagua utoaji wa huduma za Afya Mkoani Shinyanga.

Waziri Mhe. Ummy amesisitiza huduma ya kipimo cha haraka cha malaria ile ya kudungwa sindano, dawa za Alu, dawa za SP kwa wajawazito pamoja na sindano ya malaria kali zifanyike bure isipokuwa kipimo cha BS.

“Kipimo cha Malaria cha haraka kile unadungwa sindano ni bure usilipie hata shilingi ukiombwa hela nipigie simu lakini pia dawa ya Malaria SP  bure, dawa ya Malaria Alu ni bule na sindano ya Malaria kali bure mganga mkuu wa wilaya nataka usimamia maelekezo ya serikali dawa hizo zitolewe bure lakini mwananchi ukiambiwa kile kipimo cha BS kile ndiyo unaweza kulipia”.amesema Waziri Ummy

Waziri Ummy amewahakikishia wananchi wa Wilaya ya Kishapu kuwa serikali itaendelea kutatua changamoto zilizopo kwenye  sekta ya Afya ikiwemo uhaba wa watumishi, ubovu wa miundombinu  pamoja na magari ya kusafirisha wagonjwa (Ambulace).

Aidha Waziri huyo  amewataka wataalam wa Afya wakiwemo madaktari na wauguzi Mkoani Shinyanga, kuzingatia weledi na uadilifu katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi hasa wagonjwa.

Amesema ni muhimu ufanyike uchambuzi kwa Kila Halmashauri ili kubaini kada zinazokwamisha upatikanaji wa huduma za Afya katika Mkoa wa Shinyanga.

 Awali wakati akizungumza mbunge wa jimbo la Kishapu Mhe. Boniphace Butondo ameipongeza serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutatua changamoto za wananchi.

 Mhe. Butondo amesema pamoja na jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali katika sekta ya Afya, zipo baadhi ya changamoto zinazowakabili wakazi wa Kishapu ikiwemo uhaba wa watumishi pamoja na magari ya kusafirishia wagonjwa (Abulace).

Katika taarifa yake Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Joseph Mkude amesema taratibu za kuzuia mianya ya uharifu ikiwemo wizi zinaendelea kuzingatiwa ambapo amemhakikishia waziri Ummy kuwa ataendelea kuimarisha ulinzi na usalama katika sekta ya Afya Wilaya ya Kishapu.

Baadhi ya wakazi wa Wilaya ya Shinyanga wameipongeza serikali kwa kuendelea kuboresha huduma za Afya ambapo wamemuomba waziri wa Afya kushughulikia haraka changamoto zilizopo.

Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu  Julai 14, 2023  amehitimisha ziara yake ya siku mbili Mkoani Shinyanga ambapo katika  wilaya ya  kishapu ametembelea na kukagua utoaji wa huduma za Afya Hospitali ya Wilaya ya Kishapu ambayo inaitwa Jakaya Mrisho Kikwete, Kituo cha Afya Negezi pamoja na Zahanati ya Maganzo.

  

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akizungumza na viongozi mbalimbali kwenye ofisi ya mkuu wa Wilaya ya Kishapu.


Share To:

Misalaba

Post A Comment: