Serikali imesema imewekeza fedha kiasi cha shilingi mil. 214.3 kuboresha miundombinu ya barabara katika kivutio cha utalii cha Maporomoko ya Milima ya  Uluguru Mkoani Morogoro.

Hayo yamesemwa leo bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe.Khamis Chillo (Mb) kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Nora Mzeru kuhusu lini Serikali itaweka miundombinu katika kivutio cha utalii cha Mount Uluguru Waterfall.

“Serikali kupitia mradi wa kupunguza athari za UVIKO-19 ilikarabati barabara ya kuelekea kwenye msitu huo wenye urefu wa Kilometa nane kutoka kijiji cha Kibaoni hadi Bunduki kwenye kivutio cha maporomoko ya Hululu kwa lengo la kuwezesha watalii kufika kwa urahisi kwenye kivutio hicho “

Amefafanua kuwa Serikali imeanza kujenga miundombinu mbalimbali ikiwemo ngazi kuelekea kwenye maporomoko ya Hululu, ujenzi wa choo, kuweka miundombinu ya maji, mfumo wa umeme wa jua na mashine ya kusukuma maji na kujenga daraja la mbao kuvuka mto Mgeta.

Aidha, Mhe. Chillo ameongeza kuwa  Serikali inaendelea kuhamasisha wawekezaji kuwekeza miundombinu ya utalii katika msitu huo ikiwa ni pamoja na makambi (camp sites), loji, hotel na maeneo ya burudani.

Share To:

Post A Comment: