Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Bw. Kadari Singo, kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt.Natu El-maamry Mwamba, akifungua warsha maalum wajumbe wa Timu ya Wataalamu iliyoandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na wajumbe wa Timu Kuu za Uandishi na Mapitio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 iliyolenga kubadilishana uzoefu katika kuandaa na kutekeleza Dira mpya, iliyofanyika katika ukumbi wa Julius Nyerere Convenction Centre, jijini Dar es Salaam.

 Na. Saidina Msangi na Joseph Mahumi, WFM, Dar es Salaam.


Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na Taasisi ya Uongozi imekutanisha wajumbe wa Timu ya Wataalamu iliyoandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na wajumbe wa Timu Kuu za Uandishi na Mapitio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili kujadili mafanikio, changamoto na mahitaji muhimu katika kuandaa na kutekeleza Dira mpya ya Maendeleo ya Taifa 2050.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Kadari Singo alisema kuwa warsha hiyo inatoa fursa kwa wajumbe wa Timu Kuu za Uandishi na Mapitio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupata uzoefu kutoka Timu ya Wataalamu iliyoandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025.

" Warsha hii ina lengo la kufanya uchambuzi wa mambo ya msingi ya kuzingatia katika uandaaji mipango kwa miaka 25 ijayo, kwa kuwa nchi yoyote ina mipango ya muda mfupi, wa kati na muda mrefu ambapo sasa Serikali iko katika mchakato wa kuandaa malengo kwa miaka 25 ijayo" alisema Bw. Singo.

Alisema warsha hiyo itatoa fursa kwa wajumbe kufanya uchambuzi wa mafanikio na changamoto katika uaandaaji na utekelezaji wa mipango ya maendeleo kitaifa, maamuzi ambayo yataathiri vizazi vijavyo.

“Mipango ya maendeleo inahitaji utaalamu na ushirikishwaji wa wadau mbalimbali na wananchi kwa ujumla ili kupata mahitaji muhimu ya Taifa, kuandaa na kutekeleza mipango hiyo kwa pamoja’’, alisema Bw. Singo

Alifafanua pia kuwa warsha hiyo itatoa fursa kwa wajumbe kujadili kwa kina kipi kinawezekana na kipi hakiwezekani ili Dira itakayoandaliwa iweze kutoa mwongozo katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo nchini.

Naye Kamishna wa Idara ya Mipango ya Kitaifa Wizara ya Fedha na Mipango ambaye pia ni mwenyekiti wa Sekretarieti ya maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Dkt. Mursali Milanzi, alisema kuwa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 itashirikisha kila mwananchi katika mchakato wa uandaaji na utekelezaji wa Dira na ametoa rai kwa wananchi kujiandaa kushiriki kikamilifu katika mchakato huo utakaoanza hivi karibuni.

Akizungumzia warsha hiyo alisema kuwa inatoa fursa kwa wajumbe wa maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kubadilishana uzoefu na kujifunza kutoka kwa wajumbe wa timu iliyoandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025.

“Warsha hii itasaidia kujenga uwezo wa timu zitakazohusika katika uandaaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambayo ni timu ya sekretarieti, timu ya uandishi na timu ya mapitio kujifunza na kupata uzoefu’’, alisema Dkt. Milanzi.

Alisema mchakato wa maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 umeanza mwezi wa nne baada ya kuzinduliwa na Mhe. Makamu wa Rais Dkt. Philip Isdor Mpango, jijini Dodoma na zoezi linaendelea ambapo ushirikishaji wa wadau umeanza.

Alisema Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 imeweza kusogeza maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, huduma za afya, miundombinu pamoja na maendeleo ya kiuchumi licha ya changamoto mbalimbali ikiwemo covid 19 ambayo imesababisha kuchelewa kwa baadhi ya mipango.

Alisema matarajio ya Serikali katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ni kuwa yale yaliyokuwa changamoto katika utekelezaji wa Dira ya 2025 ili kuweza kujifunza na kuboresha maeneo yaliyokuwa na changamoto.

Dkt. Milanzi alisema kuwa Maendeleo ya sayansi na teknolojia yatachochea kutekeleza Dira 2050 kwa kutoa taarifa kwa urahisi na pia kujifunza ambapo Serikali inalenga kuwekeza zaidi katika rasilimali watu ili waweze kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa dira na kwenda kwa kasi zaidi kimaendeleo.

Kamishna wa Idara ya Mipango ya Kitaifa Wizara ya Fedha na Mipango ambaye pia ni mwenyekiti wa Sekretarieti ya maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Dk. Mursali A. Milanzi, akizungumza katika warsha maalum wajumbe wa Timu ya Wataalamu iliyoandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na wajumbe wa Timu Kuu za Uandishi na Mapitio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 iliyolenga kubadilishana uzoefu katika kuandaa na kutekeleza Dira mpya, iliyofanyika katika ukumbi wa Julius Nyerere Convenction Centre, jijini Dar es Salaam


Wajumbe wa Timu ya Wataalamu iliyoandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na wajumbe wa Timu Kuu za Uandishi na Mapitio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, wakifuatilia mawasilisho katika warsha iliyokutanisha wajumbe hao iliyofanyika katika ukumbi wa Julius Nyerere Convenction Centre, jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya wajumbe wa Timu ya Wataalamu iliyoandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na wajumbe wa Timu Kuu za Uandishi na Mapitio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, wakifuatilia mawasilisho katika warsha iliyokutanisha wajumbe hao iliyofanyika katika ukumbi wa Julius Nyerere Convenction Centre, jijini Dar es Salaam.


Meza kuu ikiongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Bw. Kadari Singo, (walioketi katikati)kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt.Natu El-maamry Mwamba, ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Sekretarieti ya Maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, katika warsha iliyofanyika katika ukumbi wa Julius Nyerere Convenction Centre, jijini Dar es Salaam.(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, WFM, Dar Es Salaam)


Meza kuu ikiongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Bw. Kadari Singo, (walioketi katikati) kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt.Natu El-maamry Mwamba, ikiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Timu ya Wataalamu iliyoandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, katika warsha iliyofanyika katika ukumbi wa Julius Nyerere Convenction Centre, jijini Dar es Salaam.
Share To:

Post A Comment: