Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma Bw. Ally Senga Gugu  ameshiriki katika mapokezi ya Mabingwa wa Shule za Sekondari Afrika (CAF) Fountain Gate walioiwakilisha Tanzania na Ukanda wa Afrika mashariki (CECAFA) katika mashindano ya mpira wa Miguu kwa wasichana ngazi ya Shule za Sekondari yaliyofanyika Durban, Afrika Kusini.
 
Mapokezi hayo yamefanyika katika viwanja vya  Chinangali Park jijini Dodoma ambapo shule mbalimbali zilikusanyika na viongozi wa Serikali kwa ajili ya mapokezi ya Mabingwa hao.
 
"Sisi wenzenu wa Sekretarieti ya Mkoa wa Dodoma, Wakuu wa Wilaya na Halmashauri zote za Mkoa wa Dodoma tuna furaha sana na tunawashukuru wenzetu wa Fountain Gate kwa kutuheshimisha na kutupa furaha hii na pengine ni kama vile sisi tulijua dhamira yenu na kazi kubwa  ambayo mmewekeza katika kuwajenga vijana hawa wa wakiume na kike katika kushiriki mashindano siyo tu ya Mkoa bali ngazi ya Kitaifa na Mataifa 
 
"Nakumbuka kabla ya kwenda kwenye mashindano Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ilipata fursa ya kuwakaribisha pale Mkoani tulikutana na tulifurahi tukapata chakula cha pamoja na sisi kama watumishi wa Mkoa huu tumeona baraka wa lile  ambalo Mkuu wa Mkoa alilifanya kwasababu baada ya kuwaaga vizuri kwa kuwapa tuzo na hamasa ambayo Mkoa ulifanya tunawashukuru sana kwa kubeba dhima ile na kuenda kuifanyia kazi leo hii mmekuja kutufurahisha kwa kweli tunawashukuru sana na kuwapongeza kwa dhati. " Amesema Gugu 
 
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Fountain Gates Bw. Japhet Makau amewashukuru wana Dodoma kwa mapokezi mazuri kwani ni nje ya matarajio yao na kuelezea namna walivyoibuka washindi.
 
"Tumetoka Durban, Afrika Kusini ambapo mabinti zetu timu ya Sekondari ya Wasichana ya Mpira wa miguu Fountain Gate wamekuwa mabingwa wa soka wa Afrika kwa shule za Sekondari, mashindano haya yalianza ngazi ya shule ambapo katika Tanzania shule za Mkoa wa Dar-es-Salaam na Tanga zilishirikishwa lakini sisi tuliomba kushiriki kwasababu muda ulikuwa ni mfupi na sisi tukaibuka kuwa washindi  
 
"Tulienda kuiwakilisha Tanzania katika mashindano ya CECAFA ambapo tulijinyakulia Millioni Mia Mbili za Kitanzania kama washindi wa michuano hiyo sambamba na kombe baada ya hapo tukakakiwa kwenda Afrika Kusini ambapo kulikuwa na zaidi ya Mataifa 11 lakini katika timu za wasichana zilikuwa timu sita katika mashindano ambapo mechi ya kwanza tulipangwa kucheza na wenyeji Afrika Kusini na Fountain Gate ilishinda goli 7 kwa moja, mechi ya pili Gambia na Fountain Gate, nusu fainali goli nne kwa sifuri tukapata tiketi ya kucheza fainali na Morocco  ambapo alipata kichapo cha goli tatu kwa sifuri  kwa hiyo timu ya Fountain Gate kutoka Dodoma  wakawa Mabingwa kutoka Tanzania sambamba na  ubingwa tuliweza kupata mchezaji bora, mfungaji bora na goal keeper bora "Amesema Bw. Makau

Katika mashindano hayo timu ya Fountain Gate imejinyakulia kitita cha Dola za Marekani  300,000 pamoja na kombe.

Share To:

Post A Comment: