Na WyEST,BUTIAMA - MARA



Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof. Adolf Mkenda amesema Chuo Kikuu cha Mwalimu Julius K. Nyerere cha Kilimo na Teknolojia (MJNUAT) kilichopo Butiama kitaanza kudahili wanafunzi mwaka huu 2023 katika fani za kilimo na teknolojia.

Ameyasema hayo Wilayani Butiama mkoani Mara wakati alipotembelea kukagua maendeleo ya chuo hicho na kukitaka chuo hicho kujikita kwenye kutoa mafunzo ya kilimo kwa upana wake ambao ndio msingi halisi wa uanzishwaji chuo hicho.

Waziri Mkenda pia ameelekeza chuo hicho kufanya tafiti kwenye eneo la kilimo na kusambaza matokeo ya tafiti hizo ili yaweze kunufaisha wakulima mahali walipo kwa kuongeza tija na uzalishaji

Mkenda ameongeza kuwa mikakati mbalimbali itatumika kuhakikisha wanafikia vigezo vya kupata ithibati ili kuruhusu kutoa mafunzo ikiwemo kuongeza wanataaluma na kuweka mazingira na miundombinu stahiki ya kufundishia na kujifunzia.

"Tutahakikisha MJNUAT Butiama kinaanza kutoa Mafunzo mwaka huu 2023, tayari Serikali imetoa Shilingi bilioni 2.6 kwa ajili ya kukarabati majengo yaliyopo na kujenga hosteli mpya 2 ili wanafunzi watakapoingia wakae katika mazingira bora," amefafanua Waziri Mkenda.

Profesa Mkenda ameongeza kuwa Serikali pia imetenga kiasi cha Shilingi bilioni 102 kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) kwa ajili ya kujenga makao makuu ya Chuo hicho hapo hapo Butiama.

Amesisitiza kuwa uwepo wa MJNUAT ni moja ya njia za kuenzi maono ya Baba wa Taifa kuhusu kutoa elimu ujuzi ikiwemo elimu ya kilimo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Mhe. Mosses Kaegele ameishukuru Serikali kwa kuendeleza Ujenzi wa Chuo Kikuu cha MJNUAT na kuhakikisha kinakwenda kuanza kutoa mafunzo mwaka huu.

"Tunapongeza sana kwa hatua hii ya Wizara kuhakikisha Chuo kinaanza udahili . Na katika kazi ya ukarabati Mhe. katika Wilaya tuna uzoefu na kazi za ujenzi kupitia mfumo wa Force account, tutasaidia kuhakikisha kazi inafanyika kwa ubora ili thamani ya pesa ionekane," ameongeza Mhe. Kaegele.

Mhe. Jumanne Sagini, Mbunge wa Butiama ameipongeza Wizara ya Elimu kwa kutoa fedha kukiendeleza Chuo cha MJNUAT kuhakikisha sasa kinakwenda kuanza kutoa mafunzo, kuunda Baraza, kuteua Mwenyekiti na Mkuu wa Chuo.

"Napongeza pia mtazamo wa Wizara kuhusu mafunzo kuhakikisha yanajenga ujuzi. Hii inaashiria kuwa vijana wakitoka hapo MJNUAT wataweza kujiajiri katika kilimo," ameongeza Mhe. Sagini.

Kwa upande wake Kaimu Makamu Mkuu wa chuo cha MJNUAT, Prof. Lesakit Mellau amesema chuo hicho kinaendeshwa kwa usajili wa muda 'provisional registration license' na kwamba kilianza rasmi Machi 2015 baada ya Rais wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Kikwete kuteua viongozi.

Amesema kuwa tayari wameshaandaa mitaala 29 ikiwemo 20 ya Shahada ya Awali na 9 ya Diploma na kuongeza kuwa udahili unaotarajia kuanza baadae mwaka huu utaanza na wanafunzi 400.

Share To:

Post A Comment: