OR-TAMISEMI


Tanzania inatarajia kunufaika zaidi na ushirikiano baina yake na Serikali ya Korea Kusini katika nyanja za afya, elimu na teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA).


Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais- Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Angellah Kairuki mara baada ya mazungumzo yake na ujumbe wa wabunge kutoka Nchini Korea Kusini 


Mara baada ya mazungumzo hayo yaliyofanyikia jijini Dar es Salaam Jumatano ya Tar 11 Januari 2023, Waziri Kairuki alizungumza na waandishi wa habari kuwaeleza kile walichokubaliana.


Waziri huyo ameanza kwa kuwashukuru wabunge hao na ujumbe walioambatana nao kutoka Ubalozi wa Korea Kusini nchini Tanzania pamoja na Shirika la Good Neighbors ambalo lipo katika mikoa nane nchini.


Alisema wabunge hao wanaongoza kamati mbalimbali zinazohusu masuala ya mashirikiano ya Kimataifa ikiwemo Afrika.


Waziri Kairuki alisema wanawashukuru pamoja na vikao mbalimbali na Wizara ya Elimu na ya Wizara ya Fedha pia wameweza kupata fursa ya kuja kujadiliana na Ofisi ya Rais TAMISEMI kuona maeneo mbalimbali wanaweza kushirikiana.


"Yapo maeneo kadhaa takribani sita tumeweza kuwaeleza kama kipaumbele cha nchi yetu ikiwemo suala la upatikanaji wa vituo vya kutolea huduma za afya, suala la kuhakikisha tunakuwa na nishati mbadala au nishaji jadidifu hasa ikizingatiwa tuna vituo vya kutolea huduma za afya zaidi ya 1000 na wameonesha nia ya kuweza kutusaidia ili vituo hivyo kuweza kupata umeme mbadala wa jua," alisema Waziri Kairuki 


Alisema Pia wamewashukuru kwa kuendelea kuwasaidia kwenye masuala ya afya hasa mama na mtoto na ujenzi wa vituo vya afya jijini Dar es Salaam.


"Tumewaeleza jinsi wanavyoweza kutusaidia kuunganisha vituo vyetu vya afya ikiwemo masuala ya huduma ya dawa na kitabibu hususan Mkoa wetu wa Dodoma na wamekubali kuviunganisha vyote kwa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano na tunaweza kushirikiana katika mikoa mingine zaidi," alisema 


Aidha, Waziri Kairuki alisema eneo jingine ni la upatikaji wa elimu iliyo bora hasa upungufu wa walimu kwa kutumia TEHAMA katika utoaji elimu ama ufundishaji.


"Na katika hili, mmoja wa wabunge amesema inawezekana kwani yeye mwenyewe ameweza kunufaika na mfumo huu wa masomo kwa masafa ya mbali," alisema


Alisema wameonyesha utayari wa kuongeza misaada kwa upande wa Tanzania wa kifedha zaidi ya mara mbili na wamesema watakuwa mabalozi wema kwa upande wa Tanzania.


"Tumewaomba ushirikiano kwa vyuo vyao kushirikiana na chuo chetu cha  Serikali za Mitaa - Hombolo  kuona ni namna gani tunaweza kujenga uwezo wa watendaji wetu," alisema 


Pia, alisema tumewakaribisha wawekezaji kuja Tanzania kuwekeza kwenye halmashauri zetu kwa Tanzania Bara na Zanzibar kwenye sekta mbalimbali kama za elimu, afya, kilimo na mengineyo.


"Tumewaomba ushirikiano ya miji dada ya Tanzania na Korea kuona tunavyoweza Kushirikiana" alisema


Katika Hatua nyingine Mbunge Park Jenng kutoka Nchini Korea ya Kusini ametoa Kiasi cha Dola 72000 kusaidia Kaya 1000 kupitia mradi wa ufugaji Mbuzi kupitia Shirika la Good Neighbors.

Share To:

Post A Comment: