Mratibu wa Miradi wa Shirika lisilo la Kiserikali la Trees for the Future Tanzania Mkoa wa Singida Ibrahim Mghama, akizungumza  na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Upandaji miti ili kulinda vyanzo vya maji na uhifadhi wa mazingira mkoani hapa ulioongozwa na Mkuu wa Mkoa, Peter Serukamba uliofanyika jana katika Halmashauri ya Wilaya ya  Singida Ilongero.

Na Dotto Mwaibale, Singida

SHIRIKA lisilo la Kiserikali la Trees for the Future Tanzania linalojishughulisha na kilimo mseto, kilimo endelevu kwa wakulima wenye kipato cha chini vijiji ili kutokomeza njaa, Umaskini na Ukataji wa miti lenye makao yake makuu mkoani Singida limetoa miche 3,000 kwa ajili ya kampeni ya kupanda miti ili kulinda vyanzo vya maji na kutunza mazingira iliyozinduliwa jana na Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba.

 Akizungumza katika hafla ya uzinduzi  wa kampeni hiyo iliyofanyika makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida Ilongero Mratibu wa Miradi wa shirika hilo Ibrahim Hassan Mghama alisema miche hiyo ikiwemo ile wanayoigawa kwa wakulima imetolewa na shirika hilo kwa kushirikiana na wadau wao  Taasisi za kiraia za Adese na Waendelee zote za Singida.

Mghama alisema tangu shirika hilo lianze kufanya kazi mkoani hapa mwaka 2016 limeshiriki katika matukio kadhaa likiwemo la upandaji wa miti Msitu wa Mughola mwaka jana huku mwaka 2019 lilifanikiwa kupanda miti 2.5 milioni, mwaka 2020 miti milioni 3.2.

” Tangu shirika hili lianze kufanya kazi limepanda miti zaidi ya 8 milioni ikiwa ni utekelezaji wa mradi wa Bustani Msitu ndani ya Mkoa wa Singida,” alisema Mghama.

Alisema katika miti hiyo iliyopandwa ipo miti ya matunda, mbao, uzio, miti ya kurutubisha ardhi na malisho kwa ajili ya mifugo.

Mghama  alisema mwaka huu wamejipanga kupanda miti milioni 3 na kuwa mpaka sasa wana miche takribani Milioni mbili na laki tisa iliyopo kwenye vitalu 211 na kuwa lengo lao ni kupunguza umaskini wa kipato kwa kufanya shughuli endelevu za upandaji wa miti ili kukomesha njaa, umaskini wa kipato na kuboresha afya za wanajamii na uhifadhi wa mazingira.

Alisema kati ya miche hiyo 570 itapandwa kando ya barabara ya Singida kwenda Mwanza, mingine itapandwa maeneo ya Karakana na kwenye chanzo cha maji cha Mwankoko jumla ikiwa ni 1500.

Mghama alitumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi kuitunza miti hiyo inayopandwa kwenye maeneo yao na kuacha tabia ya kuacha mifugo kwenda kuiharibu..

Kwa upande wake Msimamizi Msaidizi wa Miradi wa Shirika hilo, Nurudin Kambulage alisema mkakati wa shirika hilo kwa mwaka huu ni kupanda miche mingi zaidi ambapo kwa wadau wao wana zaidi ya miche milioni moja  hivyo wakulima watapata ya kutosha na kuweza kuhifadhi mazingira na ardhi katika mashamba yao.

Msimamizi wa Miradi Msaidizi wa shirika hilo Mkoa wa Singida, Nurudin Kambulage akizungumza kwenye uzinduzi huo.
Miche ya miti ikipandwa.
Miche ya miti ikipandwa.
Mtaalam wa Shirika hilo, Abisai Malela akishiriki upandaji wa miche katika uzinduzi huo.
Mratibu wa Miradi wa shirika hilo, Ibrahim Mghama  akishiriki zoezi la upandaji wa miche ya miti.

 Wafanyakazi wa Shirika la Tree for the Future lenye makao yake makuu mkoani Singida na wadau wao kutoka mashirika ya Adese na Waendelee wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kushiriki zoezi la upandaji miche ya miti. 

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: