Na John Walter-Manyara

Baada ya vita vya  mwezi mmoja vya kumtafuta nyota wa shindano la kusaka vipaji vya kuimba na kuigiza Strong Talent Search (STS), hatimaye mshiriki Milka Emmanuel Kutoka Dareda Wilaya ya Babati ameibuka kidedea wa shindano hilo.

Ushindi wa Milka umetangazwa na mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Manyara Charles Makongoro Nyerere ambaye aliwakilishwa na Katibu Tawala Wilaya ya Babati Khalifan Mathipula , katika Uwanja wa Kwaraa Mjini Babati  zilipofanyika fainali hizo.

Akizungumza baada ya kumtangaza mshindi, Mathipula ameipongeza Smile FM redio kwa kuandaa Mashindano hayo pamoja na Kampuni ya Mati super Brand Ltd kwa kudhamini shindano huku  akikumbusha wadau wengine kusaidia washiriki wa shindano hilo ili wasipotee kama ambavyo washiriki wa Mashindano kama hayo  wanavyopotea.


"Washiriki wote  ni washindi na wana vipaji vikubwa, Smile fm na Mati Super Brand naomba muwachukue vijana hawa muwasaidie ili wasipotee" Amesema


Mkurugenzi wa Smile fm redio amesema washiriki waliofanikiwa kuingia kwenye Kumi Bora wataunda Band Moja na kukabidhiwa vifaa vitakavyosaidia kufanya kazi kwa Pamoja.

Milka amejinyakulia Shilingi Laki 5  kutokana kwa mdhamini MATI SUPER BRAND kupitia Kinywaji Cha Strong Dry Gin.

Akizungumza na Smile fm Milka ambaye ni muimbaji wa nyimbo za injili, amesema wakati anaingia kwenye shindano hilo hakutegemea kama angeshinda kutokana na ushindani uliokuwepo kutoka kwa washiriki wengine.


Aidha, wakati Milka akishehereka ushindi namba moja, nyuma yake alikuwepo mshiriki Chief Kiara kutoka Nakwa  aliyeshinda nafasi ya pili akipewa shilingi Laki mbili na nusu na nafasi ya tatu ilikamatwa na Abby Nation akichukua Shilingi Laki Moja na nusu.

Kabla ya Milka kutangazwa mshindi hakuonesha dalili za waziwazi kwani watatu hao walikuwa wanachuana vikali.


Kila aliyepanda jukwaani alipagawisha watu na kusababisha shangwe Kubwa  kutoka kwa mamia ya watu waliofurika Uwanjani hapo.


Waigizaji walikuwa wawili, Sadam na Haji ambapo Sadam alitolewa hatua ya nusu fainali huku Haji akifanikiwa kufika fainali na kushia Tano Bora.



Share To:

Post A Comment: