Na Elizabeth Joseph,Monduli.
MKUU wa Wilaya ya Monduli Bw Frank Mwaisumbe amewaomba Viongozi wa Dini na Wazee wa Mila kushirikiana na Serikali ya Wilaya hiyo katika kuhamasisha mchango wa ujenzi wa Mabweni katika Shule za Sekondari wilayani humo.
Ombi hilo amelitoa wakati akiongea na viongozi hao katika mkutano wake pamoja na viongozi wa Ulinzi na Usalama Wilaya ya Monduli ambao ulilenga kuwashukuru viongozi hao kwa ushirikiano wa maendeleo kwa wananchi pamoja na kusikiliza kero zao.
Mwaisumbe alisema kuwa hali ya mabweni katika Shule za Sekondari ni mbaya kwakuwa Kuna ongezeko kubwa la idadi ya wanafunzi hivyo kusababisha wanafunzi kulala wawili Hadi watatu katika kitanda kimoja.
"Lakini Kuna wengine wanalala kwenye Floor,chini kabisa wakati wa bariki na mvua watoto wanaumwa vichomi,Shule zetu za Sekondari Zina hali mbaya sana hazina mabweni ya kutosha"aliongeza Mwaisumbe.
Aidha alibainisha kuwa Mchango wa shilingi elfu 10 ambao awali Wilaya hiyo iliweka utaratibu huo ili kusaidia ujenzi wa madarasa ni muhimu wananchi wakachangia ipasavyo ili kuweza kusaidia ujenzi wa Mabweni kwa shule hizo.
"Mchango wa elfu 10 ulikuwa ni wa madarasa tukaelekeza nguvu kwenye kujenga madarasa lakini idadi ya watoto inazidi kuongezeka kila siku na kwa mwaka huu idadi imedouble katika Wilaya yetu.
"Ukisema unapunguza kiwango Cha elfu 10 hata hiyo iliyopo bado haitoshi , tunahitaji sana hizo fedha kwaajili ya ujenzi wa Mabweni na ikiwezekana ujenzi huo uende sambamba na vitanda sababu Kuna wakati Mimi na Kamati ya Ulinzi na Usalama tulienda hospitali kumuona DMO tukachagua vitanda vilivyochoka tukaenda kuchomelea na kupaka rangi ili tutawanye kwenye shule lakini vikawa havitoshi" kwe"alisisitiza Mkuu wa Wilaya.
Hata hivyo alisema kwa upande wa Shule za Msingi nako hali ni mbaya kwakuwa baadhi ya Majengo kuta zake zimeoza huku nyingine zikiwa hazina sakafu hivyo watoto kusoma masomo yao kwenye vumbi jambo ambalo alisema ni lazima wananchi kuweka kipaumbele kuchangia Elimu wilayani humo.
"Zipo Shule kuta zake zimeoza na nyingine tumepiga marufuku watoto kusomea sababu paa zimeoza hivyo baada ya kumaliza zoezi la ujenzi wa Mabweni tutakwenda kwenye shule za Msingi sababu hali sio nzuri.
"Wananchi wa Monduli hatuna mtu wa kumbebesha mizigo hii,ni ya kwetu pamoja na janga tulilonalo la njaa na Ukame lazima tuangalie tunafanyaje kuhusu watoto wetu"aliongeza Be, Mwaisumbe.
Kwa upande wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli Bw Isack Kadogoo aliwashukuru wananchi wanaendelea kuchangia fedha za ujenzi huo wa Mabweni na kusema tayari Milioni 66 zimekusanywa hivyo kuwaomba wananchi wengine kuongeza juhudi katika uchangiaji ili kuweza kukamilisha zoezi hilo.
Naye Shekhe Ibrahim Abdallah Kutoka Mto wa Mbu aliwaomba wazazi na walezi kuwa wadau wa kwanza katika kuchangia michango mbalimbali ya Elimu kuliko kuiachia serikali peke yake itekeleze.
Katika mkutano huo Wakuu wa Idara mbalimbali za Halmashauri ya Wilaya hiyo ikiwemo TANESCO,TARURA,TASAF, RUWASA,,Elimu Msingi na Sekondari na Afya walitoa taarifa as utekelezaji wa majukumu yao.
Post A Comment: