Wakati kila jitihada zikifanywa kwa ajili ya kunusuru uhifadhi katika Bonde la Usangu na Hifadhi ya Ruaha , shughuli za binadamu kama vile mifugo na uvuvi, zimeendelea kufanywa usiku, wananchi wakihisi kuwa majira hayo askari wanakuwa hawapo mbugani.

Kufuatia hatua hiyo TANAPA imebaini njama hiyo na tayari Ng'ombe zaidi ya 300 wamekamatwa kwenye Hifadhi ya Ruaha katika Bonde la Usangu /Ihefu Novemba 07, 2022 majira ya saa mbili usiku huku wafugaji wakiamini askari wa uhifadhi watakuwa wamelala.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye kituo cha Ikoga Wilaya ya Mbarali Mkoani Mbeya Afisa Uhifadhi  wa Tanapa Benedict  Mwageni amesema kuwa wanafanya kila jitihada ya kuhakikisha shughuli za kibinadamu hazifanyiki katika bonde hilo.

Amesema wananchi wanaamini kuwa wakati wa usiku askari wanakuwa wamelala hali ambayo kwao kulala sio sehemu ya kazi  zaidi ni kulinda hifadhi ya Ruaha.

"Iwe usiku iwe mchana Tanapa tutahakikisha kuwa tunakamata kila kitu  kitakachoingia katika hifadhi" alisema Mwageni.

Mwageni amesema kuwa wananchi waache kuingiza mifugo kwenye hifadhi kwani kwa sasa nchi iko kwenye mgao wa umeme kutokana na mto Ruaha kukauka huku wanyama wakikosa maji na kufuata mabwawa ambayo kuna watu wanaendesha shughuli za uvuvi.

Amesema licha ya kuwa na wafugaji walioko karibu na hifadhi ,wamekuwa wakiingiza mifugo kuanzia saa mbili na kuitoa saa nane usiku kwa mategemeo ya askari watakuwa wamelala ambayo hiyo mbinu wameshagundua.

Hata hivyo amesema Ng'ombe hao waliokamatwa taratibu za kisheria zitafuatwa ikiwemo kuwapeleka  mahakamani na maamuzi yatatolewa.

Kwa upande wa Mraghabishi na Mdau wa Mazingira Seleman Msindi ((Afande Sele) amesema kuwa suala la mifugo katika hifadhi ndio imesababisha mto Ruaha Mkuu kukauka na wanyama wanapata adha ya upatikanaji maji.

Msindi amesema kuwa kunatakiwa serikali kuangalia eneo la ufugaji na kujirudia wananchi kuingiza mifugo katika mto Ruaha ipo siku Ng'ombe watataifishwa na kugaiwa nyama makundi mbalimbali itakuwa fundisho kutokana na kuzoea faini au kuongeza faini.

Wakati ng’ombe hao wakikamatwa, vijana waliokuwa wakiwachunga hawakuweza kuonekana eneo hilo ila kwa mujibu wa taarifa zilizothibitishwa ni kwamba wanasubiri ng’ombe zao zipelekwe kwenye kituo cha kuwakusanya ili waweze kuwatambua na kisha kulipa faini.

Kwa mujibu na sheria za uhifadhi, kila ng’ombe anatakiwa kulipiwa faini ya shilingi laki moja (Sh100,000) na mara nyingi huwa wanalipa faini na kuondoka na mifugo yao, jambo ambalo limekuwa halipunguzi tatizo bali linafanya jambo hilo kuwa la kujirudia



Share To:

Post A Comment: