Kilimo cha bustani kinahusika na uzalishaji wa mazao ya aina ya mboga, matunda, viungo na mimea ya mapambo.

Kilimo cha bustani ni chanzo cha ajira na pato kwa wakulima na watu wengine. Mboga na matunda vinatupatia virutubisho vya kujenga, kutia nguvu na kulinda mwili.

Zaidi ya hivyo, mimea ya mapambo hutumika katika kuremba na kuboresha sehemu za makazi, majengo, barabara na sehemu nyingine za wazi za jumuia.

Hata hivyo, unapowaangalia wakulima wengi mazao ya bustani hasa yale ya mbogamboga, utagundua wengi wamejikita katika uzalishaji wa mazao hayo, kwa lengo la kukidhi mahitaji ya familia pekee.

Hawa ni wakulima wasio na wigo mpana wa kuzalisha kwa kulenga soko kubwa na kupata kipato cha kudumu, japo mazao hayo yana sifa ya kuwa na soko zuri.

Ni muhimu kuhakikisha kunakuwapo mifumo mizuri kuanzia kwenye uzalishaji, uhifadhi, usindikaji na upatikanaji wa taarifa sahihi za masoko.

Haya yakifanyika, kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuwawezesha wakulima kuuza mazao yao kwa faida kubwa na kuwawezesha kukua kiuchumi.

Mambo muhimu ya kuzingatia katika uzalishaji

Hata hivyo, ili kuzalisha kwa kiwango kikubwa, mkulima wa mazao ya bustani anapaswa kuzingatia baadhi ya mambo muhimu ikiwamo kuwa na taarifa sahihi na za kutosha kuhusu zao analolima.

Mkulima anatakiwa kuwa na taarifa zote muhimu zinazohusiana na zao analotegemea kushughulika nalo.

Taarifa hizi zinajumuisha upatikanaji wa mbegu bora, hali ya hewa inayopendekezwa kwa zao husika.

Mengine ni taarifa kuhusu magonjwa na wadudu wanaoweza kulishambulia zao hilo na namna ya kuyakabili, pamoja na uhitaji wake katika soko la ndani na la nje.

2.Misingi ya uzalishaji: Ili mkulima aweze kuzalisha kwa tija na kwa gharama nafuu wakati huo

huo akilinda afya yake na ya walaji, ni muhimu kuzalisha kwa misingi ya kilimo hai.

Fanya uzalishaji wa mazao kwa kuzingatia misingi hii kuanzia kwenye mbegu kwa kutumia mbegu zilizozalishwa kwa misingi ya kilimo hai, matumizi ya mbolea hai, dawa za kudhibiti magonjwa na wadudu pamoja na uhifadhi wa mavuno au mazao yako ghalani au katika usindikaji.

Kilimo hai ni aina ya kilimo kisichotumia madawa wale kemikali za viwandani. Bidhaa zitokanazo na kilimo hai zinaelezwa kuwa na ubora maradufu kuliko bidhaa zitokanazo na madawa na mbolea za viwandani.

3.Eneo na hali ya hewa:

Kabla mkulima hajafikiria juu ya kulima zao fulani, ni lazima ahakikishe kuwa ana eneo la kutosha kwa ajili ya mazao yake

Lakini pia ahakikishe kuwa hali ya hewa ya eneo hilo inaoana na zao analotaka kulima.

4.Gharama za uzalishaji:

Jambo hili ni la msingi kwani huwezi kufanya kilimo bila kuingia katika gharama za uzalishaji.

Gharama hizi ni pamoja na ununuzi wa mbegu, maandalizi ya shamba, utunzaji wa zao shambani kwa kudhibiti wadudu na magonjwa, uvunaji na upelekaji sokoni au usindikaji.

5.Upatikanaji wa soko

Suala la soko ni la msingi na ni la wakati wote, kuanzia kipindi cha utafutaji taarifa ya zao husika, wakati zao likiwa katika hatua ya awali ya uzalishaji na hata linapokuwa tayari kwenda sokoni.

Ni muhimu kwa mkulima kutafuta soko la mazao yake ili aweze kuuza kwa bei iliyopo sokoni na ikiwa bei

imeshuka kwa ghalfa bila kutarajiwa, aweze kufikiri namna nyingine ya kutatua tatizo hilo hasa kwa kutumia njia mbadala kama vile kufanya usindikaji wa zao lake.

6.Mikataba ya ununuzi:

Mbali na upatikanaji wa taarifa za masoko kwa wakulima wa bustani, ni muhimu pia wakulima kuhakikisha kunakuwapo mikataba inayoeleweka baina yao na wanunuzi.

Mikataba hii itawawezesha kujua wanazalisha nini, watapata huduma wapi, watauza wapi, watauza kwa nani na watauza kwa bei gani.

Aidha, kabla wakulima hawajaingia katika kufanya mikataba, ni muhimu wakawa na uelewa mkubwa wa namna ya uuzaji wa mazao hayo ya bustani ndani ya nchi na hata nje ya nchi, bila kudanganywa na bila kudidimizwa ili kuendeleza uchumi wao wenyewe na wa nchi kwa jumla.

7: Kulima kulingana na uhitaji

Hili linawagusa wakulima wengi hasa wanaolima kwa kufuata mkumbo kama ilivyozoeleka hivi sasa katika jamii zetu.

Ni kweli hamasa za kutaka watu wajiingize kwenye kilimo ni nyingi, kubwa na zina umuhimu, lakini wakulima hawana budi kutafakari kabla ya kuamua kuingia kwenye kilimo flani.

Lazima wakulima wahakikishe wanalima kulingana na uhitaji wa walaji na si kulima kwa mazoea au kwa vile kila mmoja analima.

Kwa mfano, sio busara kutaka kulima matikiti kwa kuwa ndilo zao linalolimwa na kila mtu eneo uliopo. Tatuta zao ambalo mahitaji yake ni makubwa, kwa kuwa unakuwa na uhakika wa soko lake.
Share To:

Post A Comment: