Na Immanuel Msumba ; Monduli

Wilaya ya Monduli ni miongoni mwa Wilaya saba za Mkoa wa Arusha ambapo wananchi wa Wilaya hii wanajihusisha na shughuli za ufugaaji, kilimo pamoja na uhifadhi kwa ajili ya kujipatia kipato.

Licha ya wananchi hao kujihusisha na shughuli hizo kama sehemu ya kujipatia kipato wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ukame ambao kwa kiasi kikubwa unasababishwa na uharibifu wa vyanzo vya maji vilivyopo katika wilaya hiyo.

Nimetembelea Chanzo cha maji cha Ziwa Miwaleni kilichopo katika Kitongoji cha Kambi ya Mkaa katika kijiji cha Mungere wilayani humo.Katika ziara hiyo nimejionea uharibifu mkubwa wa chanzo cha maji. Kutokana na shughuli za kibinadamu kufanyika katika chanzo hicho ikiwemo kilimo cha umwagiliaji pamoja na wingi wa mifugo inayokwenda kunywa maji kwenye chanzo hicho na kusababaisha mmomonyoko wa udongo unaojaza tope kwenye chanzo hicho.

Baada ya kufika kwenye chanzo hicho nilikuta baadhi ya wakulima wamelima mpunga,nyanya na migomba hali iliyonilazimu kuwatafuta wakulima hao kwa lengo la kujua ni kwanini wanalima kwenye chanzo cha maji kutokana na sheria ya mazingira hasa ya kwenye vyanzo vya maji inayosema "Uchafuzi wa vyanzo vya maji na mazingira ni kosa kisheria" na kutoruhusu shughuli za kibinadamu ndani ya mita 60 kutoka chanzo cha maji. 

Ziara na mazungumzo yangu na wadau hao yameonesha kuwa “Shughuli za kibinadamu kufanyika katika chanzo hicho ikiwemo kilimo cha umwagiliaji pamoja na wingi wa mifugo inayokwenda kunywa maji kwenye chanzo hicho inasababaisha mmomonyoko wa udongo unaojaza tope kwenye chanzo hicho.

Mary Thomas anayejishughulisha na shughuli za kilimo cha mpunga ndani ya eneo la chanzo hicho cha maji anasema amekuwa akilima katika eneo hilo kwa zaidi ya miaka 15 sasa bila kukutana na adha ya aina yoyote ile kutoka kwa viongozi wa serikali.Pia anashangazwa na kitendo cha hivi karibuni cha Waziri wa Maji, Muheshimiwa Jumaa Aweso kutembelea chanzo hicho akiwa ameambatana na wataalamu kutoka Bonde la Kati na kuagiza kwamba wananchi wote wanaolima ndani ya eneo la chanzo hicho cha maji kuondoka mara moja baada ya kuvuna mazao waliyoyapanda kwenye eneo hilo.

"Nimeshangazwa na wataalamu kutoka Bonde la Kati kuweka bikoni kwenye shamba langu ambalo niliachiwa urithi kwa zaidi ya miaka 15 na nimekuwa nikifanya shughuli zangu za kilimo bila bughudha yoyote. Sasa natakiwa kuondoka nikiondoka hapa nitakwenda wapi wakati shamba hili ndilo ninalolitegemea kama kitega uchumi cha kuendesha maisha yangu na familia yangu"

Kutokana na eneo lake kuwekwa bikoni Mary anaiomba Serikali inapotaka kuchukua eneo kutokana na sababu mbalimbali ni vyema wakatoa elimu kwa sababu wananchi tofauti na hivi sasa ambapo kwa sasa wanatumia ubabe kuwatisha. Hii ni kwasababu wananchi wengi hawana elimu ya kutosha juu ya utunzaji wa vyanzo vya maji kwa maslahi ya Taifa na kwa vizazi vijavyo.

Meshack Lucas ambaye ni Mwenyekiti wa Kitongoji cha Kambi ya Mkaa anakiri uwepo wa uharibifu mkubwaa wa chanzo hicho cha maji kutokana na shughuli mbalimbali za kibinadamu kufanyika ndani ya eneo la chanzo cha maji.

"Ni kweli tuna chanzo cha maji katika kitongoji chetu lakini kimeharibbiwa na shughuli za kibinadamu na kusababisha wingi wa maji kupungua tofauti na miaka ya nyuma ambapo maji yalikuwa yanapatikana kwa wingi na kukidhi mahitaji ya wananchi wa eneo hili lakini kwa sasa hali ni mbaya  sana na chanzo hiki kisipotunza na sheria kusimamiwa kikaamilifu kitatoweka".

"Wakati wataaalamu wa bonde la kati walipokuja kwenye chanzo hiki cha Ziwa Miwaleni walikuta shughuli za kibinadamu zikiendelea hivyo inakuwa vigumu wananchi kukubali kwamba wamevamia na kuharibu chanzo cha maji ambacho ni tegemeo kubwa kwa wananchi wa Kambi ya Mkaa". Alisema na kuongeza

Mwenyekiti huyo anasema wananchi wanaolima katika eneo la chanzo hicho pia wanatumia majenereta kupampu maji kutoka kwenye chanzo kwa ajili ya kilimo hicho cha umwagiliaji. Hali hiyo inasababisha manteki yaliyowekwa na Bonde la Kati kushindwa kujaa maji kwa ajili ya kusambazwa kwa wananchi. 

"Wito wangu kwa serikali itafute njia muafaka na muda mzuri wa kuwaondoa wananchi hawa pamoja na kuimarisha ulinzi shirikishi utakaokwenda sambamba na kutoa elimu kwa wananchi juu ya kuhifadhi ili wasiendelee kuharibu chanzo hiki cha maji na waelewe kuwa sasa eneo hili lote la chanzo lipo chini ya usimamizi wa serikali kwa ajili kukihifadhi chanzo hiki kwa usalama wa watumiaji wote wa huduma ya maji katika eneo hilo".

Anasema ulinzi wa kijiji ni mdogo na kuomba kuongezewa ulinzi na uongozi wa Wilaya ya Monduli pamoja na  uongozi wa  bonde kuja kuweka  uzio wa kuzunguka chanzo chote cha maji ili kuzuia mifugo isiingie ndani ya chanzo kunywa maji.

Naye Mkazi wa kitongoji cha Kambi ya Mkaa Paschal Laizer ambaye ni dereva bodaboda anasema wanalazimika kwenda umbali mrefu kufuata huduma ya maji kutokana na uharibufu unaofanywa na baadhi ya wananchi katika chanzo hicho kwa ajili ya shughuli za kilimo na kunywesha mifugo maji.

"Kilimo na ufugaji vimetuathiri sana katika eneo hili kwa sababu wanafanya shuguli hizo ndani ya eneo la chanzo cha maji tunamshukuru Waziri Aweso kwa ziara yake katika eneo hili hivi karibuni na kujionea uharibufu huu ambapo amaeagiza wakulima wanaolima katika eneo hili waondoke mara moja ili kunusuru chanzo hicho"

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya ya watumiaji wa Mto wa Mbu katika Bonde la Kati William Francis anasema vyanzo vingi vya maji vinakufa kutoka na wafugaji kupeleka mifugo ndani ya vyanzo na kukanyaga kule ndani na kusababisha vyanzo hivyo kijifukia kwa mmonmonyoko wa udongo katika vyanzo hivyo pamoja na walima wanaoendesha shughuli za kilimo ndani ya eneo la chanzo cha maji kwa sababu wanaleta madhara mengine makubwa kwa upungufu wa maji kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya binadamu hivyo nitoe rai kwa serikali ya kijiji kuendelea kutoa elimu ya kutosha kwa jamii na kutumia njia sahihi  za usimamizi wa maji ya mwaka 2009 namba 9.

"Maji ni uhai kila mtu anajukumu la kuyalinda chanzo hiki kinaharibika kwa kasi sana nina taarifa nimepata juzi kuwa pale bado wananchi wanaendeea kuandaa mashamba kwa ajili ya kuendelea na kilimo licha ya Serikali kukataza.Sisi kama Bonde la kati tutahakiksha tunaendelea kulinda kile chanzo cha maji kwa ajili ya wanajumuiya ya watumiaji maji mto wa mbu".

Moja ya miundombinu ya kunyweshea ngombe maji nje ya chanzo hicho ikiwa imekauka kabisa na kuchangia ngombe kuendelea kwenda kwenye chanzo cha maji.




Share To:

Post A Comment: