Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba,  akihesabiwa na Karani wa Sensa, Jasmini Kinga katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi nyumbani kwake Mtaa wa Utemini mkoani hapa leo hii Agosti 23, 2022.
 Karani wa Sensa ya Watu na Makazi, James Rutihinde akijitambulisha kwa Katibu Tawala Mkoa wa Singida, Dorothy Mwaluko kabla ya zoezi hilo lililofanyika nyumbani kwake mkoani hapa.
Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhandisi Paskas Mulagiri  akihesabiwa na Karani wa Sensa, Peter Samike katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi nyumbani kwake mkoani hapa leo hii Agosti 23, 2022.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Singida, Alhajj Juma Killimba akionesha furaha yake kabla ya kuhesabiwa katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi lililoanza leo.
Mratibu wa Sensa ya Watu na Makazi Mkoa wa Singida, Nying'oya Kipuyo, akitoa maelezo mafupi kabla ya Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba ajahesabiwa.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida, Alhajj Juma Killimbah  akihesabiwa na Karani wa Sensa, Flora Mkumbo, katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi nyumbani kwake mkoani hapa leo hii Agosti 23, 2022.

Makarani wa Sensa ya Watu na Makazi, James Rutuhinde (kushoto) na Peter Samike wakiwa tayari kwa kazi.


Dotto Mwaibale na Thobias Mwanakatwe, Singida

 

ZOEZI la Sensa ya Watu na Makazi limeendelea vizuri katika Mkoa wa Singida ambapo makarani walianza kazi ya kuhesabu watu katika maeneo maalum kama nyumba za kulala wageni na vituo vya mabasi na kupata ushirikiano wa kutosha.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba, akizungumza na waandishi wa habari baada ya kushiriki sensa, alisema kutokana na uhamasishaji wa kutosha uliofanyika wananchi wamekuwa wakitoa ushirikiano mzuri kwa makarani wa sensa.

"Maeneo ambayo yalikuwa na changamoto kidogo kama Wilaya ya Singida vijijini,mpaka wa Mkoa wa Manyara na mpaka wa Mkoa wa Dodoma tumeongea na wananchi na wamekubali kuhesabiwa," alisema.

Serukamba amewaomba wananchi wanapotoka waache namba za simu na taarifa sahihi majumbani mwao ili makarani watakapofika wawatafute na kushirikia zoezi la kuhesabiwa.

 Naye Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Singida, Alhaji Juma Killimbah, alisema wananchi watakapojitokeza kuhesabiwa watakuwa wameisaidia serikali inayoongozwa na CCM kupanga mipango yake ya maendeleo.

"Sisi CCM huwa tunatengeneza ilani ya chama kulingana na idadi ya watu kwa hiyo tunawaomba wananchi wajitokeze kuhesabiwa na kwa jinsi serikali ya Mkoa wa Singida ilivyofanya uhamasisha mkoa utafanikiwa katika zoezi hili," alisema.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhandisi Paskas Mulagiri, alisema kulikuwa na changamoto iliyojitokeza katika baadhi ya kata ambapo wananchi walisema hawatahesabiwa kwasababu tu mipaka ya sensa haiendani na mipaka ya kiutawala.

Alisema kutokana na changamoto hiyo, Kamati ya Ulinzi na Usalama ilishughulikia tatizo hilo kwa kutembelea kata husika kuzungumza na wananchi ambao wameelimishwa na wamekubali kuhesabiwa.

"Natoa wito kwa wananchi watambue kuwa mipaka ya sensa si mipaka ya kiutawala mipaka hii imetengwa kwa ajili ya maeneo ya sensa ambayo watu wa takwimu wanaitumia kujua idadi ya watu," alisema.

Maeneo mengi ya mji wa Singida wananchi wameonekana wakiwa majumbani mwao kusubiri makarani kuhesabiwa na hata maeneo ya biashara ushirikiano kwa makarani umekuwa mzuri. 

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: