WIZARA ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa pamoja na Wizara ya Fedha na Mipango zimeziagiza kukaa kwa pamoja kujadiliana namna ya kuhakikisha ujenzi wa Stendi katika Manispaa ya Moshi unakamilika kwa haraka kwani wananchi wamesubiria kwa muda mrefu bila mafanikio.


Ushauri huo umetolewa leo na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Daniel Chongolo alipokuwa akizungumza na wananchi wa Manispaa ya Moshi mkoani Kilimanjaro ambapo ametumia nafasi hiyo kueleza kuwa ujenzi wa stendi hiyo ulianza mwaka 2018 na ulitakiwa kukamilika mwaka 2020 .

“Na mpaka leo stendi haijakamilika , bado wasafiri wanajibana kwenye stendi ya zamani na sababu za msingi hakuna huyu anasema ilikuwa hivi , mara kimeenda vile , kimerudi pale, lakini sababu zinazotolewa hazisaidii kutatua changamoto za wananchi.Naagiza Wizara zinazohusika na hili jambo TAMISEMI na Wizara ya Fedha wakae wakubaliane namna kumaliza stendi kwa haraka.

“Wananchi hawataki maneno hatawaki hadithi, wanachotaka ni huduma iliyokusudiwa itolewe kwa wakati , tuliwahiwaadi kuwajengea stendi na stendi imeenza na fedha zimetolewa kwa kiwango fulani , nipongeze Serikali kwa kutoa fedha kiasi fulani.

“Nimeambiwa tayari Sh.bilioni saba mpaka tisa na zimeshatolewa na sasa zinahitajika zifike Sh.bilioni 17 ili stendi iweze kukamilika , mwanzo katika ujenzi ilitakiwa kujengwa na jengo la hoteli hivyo ikawa inatakiwa Sh.bilioni 28, sasa wametoa hoteli zinatakiwa Sh. bilioni 17 ili stendi ianze kutoa hduma za kisasa.

“Wananchi wanaosafiri na hasa kwenye Manispaa hii ya Moshi lazima hiyo stendi tuifikishe huko , iondoke ilivyo sasa iwe uhalisia, nataka niwahakikishie jambo hili nitalibeba na nitalifikisha kwa wahusika na leo nimezungumza na Waziri wa TAMISEMI amenihakikishia jambo analishughulikia wanaendelea na mawasiliano na Hazina ili fedha zishuke huku.

“Na agizo langu litawafikia hata kabla sijafika, sisi ndio wenye Ilani hatutaki ifike mwaka 2025 kuja kuulizwa tena stendi , tunataka stendi ya Moshi ikamilike watu waanze kuitumia ili tuanze mipango mingine na sio hadithi za muda mrefu za stendi,”amesema Chongolo.

Ameongeza kuwa yeye amepewa dhamana ya kumsaidia Mwenyekiti ambaye ndio Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania , hivyo hawezi kukubali kuja kukutana na maswali ambayo majibu yake ni rahisi kwani yanataka utekelezaji.

“Niwahakikishie tutavutana mashati , tutavutana huko waliko ili waje watekeleze lifike mwisho, hatutaki kuwa na miradi ambayo inakaa kwenye makaratasi muda mrefu. Ni lazima tuifikishe ukomo ili tuhangaike na mambo mengine, na hili na libeba mimi, kesho mniulize mimi na nitaendelea kulisukuma nikiona linanishinda nitakwenda kumwambia Mwenyekiti wetu watu wako wananishinda, na ninyi mnavyonona hivi naona ni mtu wa kushindwa?”


Share To:

Post A Comment: