Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Polisi Tarime Rorya Mrakibu Mwandamizi wa Polisi SSP Denis Kunyanja amepiga marufuku waendesha pikipiki maarufu Bodaboda kuendesha pikipiki bila kuvaa kofia ngumu,kubeba abiria zaidi ya mmoja (Mishikaki),kubeba watoto chini ya umri wa miaka 9, mwendo kasi hasa kwenye vivuko vya watembea kwa miguu,kuendesha pikipiki zisizokuwa na namba za usajili na kuendesha bila leseni.


Mkuu huyo wa Usalama Barabarani amepiga marufuku hiyo kwenye mkutano wa Polisi Jamii na Viongozi wa vijiwe vya waendesha pikipiki (Bodaboda) wilaya ya Tarime uliofanyika Agosti,16,2022 katika ukumbi wa wa Kantini ya Polisi mjini Tarime.


Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Mkuu wa Polisi wilaya ya Polisi Tarime Mrakibu Mwandamizi wa Polisi SSP Ramadhani Sarige,  Mkuu wa Polisi Jamii Mkoa , Mrakibu wa Polisi SP Daud Ibrahimu, Polisi Jamii Wilaya ya Tarime, askari wa usalama barabarani na viongozi wa vijiwe vya  waendesha pikipiki Wilaya hiyo.


Waendesha pikipiki wameomba kutokamatwa na askari ambao hawajavaa sare za Polisi kwamadai kuwa wanawashtukiza wakati wanaposhusha abiria maeneo ya stendi ya mabasi.


 Mkuu wa Usalama ameeleza kuwa waendesha bodaboda wamekuwa na tabia ya kuwaona askari na kisha kuongeza mwendo ili kuwakwepa huku wakiwa wabeba abiria jambo ambalo ni hatari linaweza kusababisha ajali na kwamba Polisi wasio na sare ni moja ya mbinu ya Jeshi la hilo katika ukamataji salama.


Viongozi wa vijiwe vya waendesha pikipiki waliohudhuria mkutano huo wameomba kusogezewa huduma karibu ya leseni wilayani Tarime badala ya kwenda kuifuata Musoma hali inayosababisha washindwe kumudu gharama za usafiri na kusababisha wafanye kazi bila leseni.



 Mkuu huyo wa Usalama Barabarani  SSP DENIS KUNYANJA ametoa siku tano kwa waendesha pikipiki kujirekebisha ili wasikamatwe na Polisi ikiwa ni Pamoja na kutoendesha pikipiki usiku wa manane,kuvaa kofia ngumu,kuacha kubeba mishikaki,kupunguza mwendo kasi, kutobeba mizigo haramu au ya uhalifu.







Share To:

Post A Comment: