WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewasihi waislam nchini waendelee kudumisha amani, upendo, umoja, mshikamano, kuhurumiana, utulivu sambamba na kujiepusha na vitendo vinavyoashiria vurugu, uonevu na uvunjifu wa amani waposherehekea Eid El Adha


 

“Tunaposherehekea Eid El Adha ni vema pia tukakumbuka maneno ya Mtume Muhammad Swalla Allahu Alayh Wasallam kwamba “Mwenye kufanya maaswi siku ya Eid ni sawa na kumuasi Allah Sub-hanahu Wata’ala siku ya kiyama”.

 

Mheshimiwa Majaliwa ameyasema hayo leo (Jumapili, Julai 10, 2022) kwenye Baraza la Eid El Adha, lililofanyika katika Msikiti wa Mfalme Muhammad wa Sita wa Morocco uliopo Kinondoni, Dar Es Salaam. Ametumia fursa hiyo kuwasisitiza wananchi umuhimu wa kudumisha amani.

 

Pia, Waziri Mkuu amesema Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan anawasihi waislamu na Watanzania kwa ujumla kuendelea kuonesha upendo, umoja na mshikamano hata baada ya kumalizika kwa masiku kumi bora katika mwaka yanayopatikana kwenye mwezi wa Dhul-Hijja.

Kadhalika, Waziri Mkuu amesema moja ya jambo adhimu katika Eid El Adha ni kuchinja na jambo hilo limethibitika katika Qur’an Tukufu pale Allah Ta’ala aliposema katika surah ya 108 ayah ya pili kwamba basi swali kwa ajili ya Mola wako na chinja kwa ajili yake.


 

“Hivyo basi, nami nahimiza kwamba tutumie fursa hiyo ya kuchinja kwa ajili ya kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa fadhila mbalimbali alizotujalia pamoja na kuwahurumia na kuwaonesha upendo wale wenzetu miongoni mwa maskini na mafakiri. Lengo ni kuhakikisha walionacho na wasionacho tunakuwa kitu kimoja na kufurahi pamoja.”

 

Wakati huo huo, Mheshimiwa Majaliwa amewasisitiza wananchi kushiriki katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi litakalofanyika tarehe 23 Agosti 2022. “Tujitokeze kwa wingi kuhesabiwa na kuunga mkono zoezi hilo. Tutoe ushirikiano kwa Makarani wa Sensa na Watendaji wetu wa Mitaa katika kufanikisha Sensa ya Watu na Makazi kwa mwaka 2022.”







Share To:

Post A Comment: