Moja ya mabasi ya wanafunzi likiwa njiani kwenda kuchukua ili kuwapeleka shuleni



Watoto wa shule ya awali wakiwa mchezoni ikiwa ni sehemu ya ratiba yao ya masomo shuleni.
Watoto wa shule ya awali wakiwa wanajifunza kwa makini namna ya kuumba herufi mbalimbali huku wengine wakipeana hadithi ikiwa ni mojawapo ya mafunzo yao shuleni. 

 

Na Abby Nkungu, Singida

 

SERIKALI  imeombwa kutoa mwongozo kwa shule binafsi juu ya muda maalum wa kuwapitia majumbani wanafunzi wa elimu ya awali kwa ajili ya kuwapeleka shule ili kuwalinda watoto hao pamoja na kutowaathiri kimasomo, kiafya, kiakili na kisaikolojia.

Ombi hilo lilitolewa kwa nyakati tofauti na baadhi ya wazazi na walezi katika Manispaa ya Singida wakati wakizungumzia utekelezaji wa Programu Jumuishi ya Taifa juu ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto (PJT- MMMAM) ya miaka mitano iliyoanza mwaka 2021- 2026.

Walisema kuwa pamoja na Programu hiyo kuonesha mafanikio kwa kushughulikia masuala mtambuka kwa mtoto aliye chini ya miaka minane, bado ipo changamoto ya watoto wa shule za awali kwenye shule binafsi kuchukuliwa mapema asubuhi kuliko kawaida hali inayoweza kuwaathiri kiafya na kielimu.

“Mimi mtoto wangu wa chekechea anapitiwa na gari la shule saa 11 alfajiri, hivyo ili kumuandaa inabidi nimuamshe saa 10:30 kwani  kuna muda wa kusumbuana hadi aamke na nimbembeleze aache kulia kwa usingizi ndipo nimuogeshe na kumvalisha nguo” alisema Elibariki Mollel, mmoja wa wazazi eneo la Minga, Manispaa ya  Singida.

"Kuna siku mtoto wangu alirejea nyumbani akiwa na jeraha kwenye paji la uso. Nilipomhoji akaniambia alijigonga kwenye gari asubuhi wakati anaenda shule kwa vile alikuwa anasinzia" alilalamika Mollel na kuongeza kuwa tatizo ni uchache wa magari kwenye shule husika hivyo kulazimika kutoka mapema kuzunguka mji mzima wakifuata wanafunzi hadi saa 2:00 asubuhi ndipo wanaingia darasani.

Mzazi mwingine, Hussein Njenje alisema kutokana na changamoto hiyo amelazimika kutafuta nyumba ya kupanga jirani na shule wanakosoma wajukuu wake ili kuwaondolea adha ya kufuatwa alfajiri na gari hali inayoweza kuwaathiri kiafya watoto kwa kutopata usingizi wa kutosha lakini pia inaweza kusababisha waichukie shule kwa kuona kama vile hiyo ni adhabu kwao.

Mmoja wa  walimu katika shule binafsi ambaye  hakupenda kutajwa jina lake ili kulinda ajira yake, alikiri kuwa kitendo cha watoto wa chekechea kuamshwa mapema kila siku  kinawaathiri kiafya na kielimu.

“Siku moja wewe njoo pale shuleni kwetu saa 4:00 asubuhi baada ya kunywa uji. Utaona huruma kwani  utakuta asilimia kubwa ya watoto wanachapa usingizi na  wengine walio macho wanapiga miayo tu kwa usingizi na uchovu baada ya kuzungushwa mji mzima kwa gari kabla ya kuingia darasani “ alieleza mwalimu huyo.

Ingawa Kaimu Ofisa elimu msingi Manispaa ya Singida, Siah Mtafya alikiri  kuwa kuwachukua wanafunzi wa awali alfajiri sana sio utaratibu mzuri, lakini alisema kuwa  hakuna sheria, kanuni wala Mwongozo wa Serikali unaoelekeza muda muafaka wa kuwapitia wanafunzi hao kuwapeleka shule. Hata hivyo, alisema kuwa watakaa na Uongozi wa shule husika ili kuona namna bora ya kushughulikia suala hilo muhimu.

Naye Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Singida, ACP Lucas Mwakatundu alisema kuwa hakuna utaratibu wa muda uliowekwa wa kuanza safari asubuhi mabasi ya shule kama ilivyo kwa mabasi ya abiria kwani majukumu yake yanafanana sana na mabasi ya wafanyakazi (staff buses); hivyo ni vigumu kuchukua hatua za kisheria.

Hata hivyo, wakati wenye Mamlaka wakibainisha kuwa hakuna sheria wala mwongozo, Daktari Bingwa mshauri wa magonjwa ya wanawake na watoto katika Hospitali ya Rufaa mkoa wa Singida, Dk Suleiman Muttani alieleza kuwa mtoto chini ya miaka minane anatakiwa kulala kwa muda wa saa 9 hadi 10 kwa siku.

Alisema kuwa iwapo watoto wa darasa la awali watalala saa 2:00 au 3:00 usiku na kuamshwa kila siku saa 11 alfajiri au kabla ya hapo kwenda shule, wanaweza kupata madhara kiafya; ingawa nafuu ipo kwa shule zenye utaratibu wa kuwapa fursa ya kulala kwa muda ili kuwapunguzia usingizi.

Kwa mujibu wa PJT- MMMAM, Tanzania ni nchi ya kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki kuifanya elimu ya awali kuwa ya lazima kwenye Sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014 ili kuijumuisha elimu ya awali katika elimu za msingi kwa kuzitaka shule zote kuwa na darasa la elimu ya awali kwa watoto walio na umri chini ya miaka mitano. 

Share To:

dotto mwaibale

Post A Comment: