Na Mwandishi wetu, DODOMA

BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini (HESLB) imetakiwa kuangalia namna bora ya  kuwasaidia wanafunzi wa vyuo vya ufundi ili waweze kupata mikopo ili kusoma kwa bidii.


Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia,Prof Adolf Mkenda amesema hayo jana Jijini hapa wakati wa  kufunga  maonesho ya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi na kuongeza kuwa kuna haja ya kuangalia namna ya kuwapunguzia mzigo wa ada wazazi na walezi wanaosomesha watoto wao katika Vyuo vya ufundi.


Waziri Mkenda amesema kwa kuwa Bodi ya mikopo sheria inawaruhusu wanapaswa kushughulikia suala hilo ili kuwasaidia vijana wa kitanzania kuwa na mwelekeo wa maisha mazuri.


"Tumewapa kazi, tunataka kuona utekelezaji wenu kwa wakati, nashukuru, jitihada za Katibu  Mkuu wa wizara  kwa kuwasiliana na Mabenki mbalimbali na tayari NMB imekubali kutoa bilioni 200 kwa ajili ya  mikopo na tutaona tunailekeza vipi katika elimu  ya  ufundi,”alisema Waziri Mkenda.



Naye Waziri wa Nchi   Ofisi ya Makamu wa Rais ,Muungano na Mazingira  Seleman Jafo   amewataka vijana wanaomaliza elimu ya kidato cha nne na kushindwa kuendelea na kidato cha tano kujiunga na vyuo vya kati na ufundi.


"Sote tunatambua umuhimu wa Vyuo vya kati na ufundi hivyo ni wajibu wetu kuwahamasisha vijana wetu kutokata tamaa ya maisha na badala yake wahiendeleze kwenye Vyuo hivi kupata ujuzi ili wajiajiri,"amesema na kuongeza;


Rais Samia Suluhu Hassan amefanya uwekezaji mkubwa katika maeneo mengi,kati ya hayo yanahitaji vijana ambao wamepata elimu ya ujuzi na sasa Serikali  imeanza mchakato wa kufufua shirika la ndege ambapo hadi sasa kuna ndege 11 na itanunua nyingine hivyo wataitajika vijana wenye ujuzi,”amesema.


Kwa upande wake Katibu  Mtendaji wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTIVET) Dkt. Adolf Rutayuga amesema hadi kufikia juni 2022 baraza lilikuwa limesajiri vyuo 454 vya elimu ya ufundi ili kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa elimu ya mafunzo stadi yenye ubora .


Amesema kati ya vyuo 454  vyuo 179 ni vya serikali na vyuo 275 ni vya sekta binafsi na kwamba idadi ya wanafunzi wanaojiunga na vyuo hivyo imeongezeka kutoka 1,17474 katika mwaka wa masomo 2014/2015  hadi kufikia 2,10775 mwaka 2020/2021 .


"Hili  ni ongezeko la wanafunzi wengi zaidi hasa katika vyuo vya sekta binafsi ambavyo vimekuwa na mchango mkubwa,”amesema.


Mwishoo

Share To:

Post A Comment: