SERIKALI ya Tanzania imesema kuwa elimu ya Msingi hadi Kidato cha Sita itatolewa bila malipo ili kuwapa nafasi Wanafunzi wote wanaotoka kwenye familia maskini ili kukabiliana na mimba za utotoni, mwamko duni wa elimu kwa baadhi ya jamii na utoro sanjari na wale wasioendelea kufuatana kwa mujibu wa sheria (Ufaulu).

Hayo yameelezwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Mwigulu Nchemba wakati akisoma Bajeti ya Serikali ya mwaka wa Fedha 2022-2023 iliyosomwa Bungeni jijini Dodoma. Pia Dkt. Mwigulu amesema Serikali itaendelea kujenga Mabweni kwenye maeneo hatari kwa watoto wa kike.

“Kwa sasa wanafunzi wa kidato cha tano ni takriban 90,825 na kidato cha sita ni 56,880. Mahitaji ya Fedha ni zaidi ya Shilingi Bilioni 10 (10,339,350,000). Ili kuwapunguzia gharama watoto hao kama Mhe. Rais alivyoielekeza Wizara, napendekeza kufuta ada kwa wanafunzi wa kidato cha tano na sita. Kwa hatua hiyo, Elimu bila Ada ni kuanzia shule za msingi mpaka kidato cha sita”, amesema Dkt. Nchemba

Amesema Serikali itaendelea kuimarisha elimu ya ufundi hususan katika vyuo vya kati kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kujiajiri ama kuajiriwa. “Mpaka sasa Wilaya 77 zina vyuo vya Ufundi VETA kati ya Wilaya 138 nchini kote. Tuna mikoa 25 ina Vyuo vya Ufundi kati ya mikoa 26. Bado mkoa wa Songwe hauna kabisa Chuo cha VETA na wabunge wa mkoa wa Songwe wamekuwa wakishinda Ofisini wakifuatilia ahadi waliopewa na Mheshimiwa Rais”.

“Bado kuna wilaya 36 ambazo hazina vyuo wala vyuo vya Mkoa. Napendekeza kutoa bilioni 100 kwa ajili ya ujezi wa vyuo vya ufundi kwa Mkoa wa Songwe na wilaya 36 ambazo hazina vyuo ili kufanya wilaya zote 138 kuwa na chuo cha Ufundi (VETA). Waheshimiwa wabunge, Huyo ndio Samia”. amesema Dkt. Nchemba.
Share To:

Post A Comment: