Na Mosses Mashala,Arusha


Wanawake walioshinda Tuzo za Malkia wa Arusha waeleza chanzo cha ushindi wao kuwa ni Bidii Kujituma na Nidhamu katika kazi ndio chanzo cha kuibuka malkia wa nguvu mkoani Arusha 2022


Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana jijini Arusha mara baada ya kutunukiwa tuzo hizo washindi hao wamewashauri wanawake nchini kujituma na kuacha tabia ya utegemezi.

Mkurugenzi wa kampuni ya Heritage Microfinance, Sia Kassian ambaye alijinyakulia tuzo mbili katika nyanja ya taasisi ya kifedha sanjari na huduma ya vinywaji alisema kwamba nidhamu,bidii na kujituma ndivyo vimemfanya afike mahali alipofika.


Mkurugenzi wa kampuni ya ViolaTours,Violet Mfuko  ambaye alinyakua tuzo katika nyanja ya utalii aliwataka wanawake kujituma na kuacha tabia ya kulalamika mara kwa Mara.


"Tunamshukuru sana Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutuonyesha njia sisi wanawake lakini wanawake tufanye kazi sasa tuache kulalamika" alisema Mfuko



Hata hivyo,mfanyabishara Aika Kessy ambaye ni mmiliki wa duka la Aika Classic  aliyejinyakulia tuzo katika nyanja ya ubunifu na mitindo alisema kwamba tuzo hiyo imempa hamasa katika kufanya kazi kwa juhudi na bidii tofauti na hapo awali.


Mshindi katika tuzo ya mgahawa bora  Leah Assenga mmiliki wa mgahawa wa Kitamu Afrika  alisema kwamba tuzo aliyoipata ni mwendelezo wa tuzo nne alizopata ambapo tuzo mbili alizipata kimataifa na zimezidi kumpa hamasa ya kufanya vizuri zaidi.




"Nimefurahi kushinda hii tuzo hii inakuwa ya nne sasa maana tuzo mbili nilishinda kimataifa na mojawapo ni Traveller's Choice Award hakika mgahawa wetu wa Kitamu umeniletea heshima ndani na nje kimataifa" alisema Assenga 


Eva Nyambura aliyenyakua tuzo katika nyanja ya kikundi bora cha mazingira  aliwataka wanawake nchini kutambua kuwa hakuna siri ya ushindi katika maisha yao zaidi ya kujituma katika kazi na bidii.

Mmiliki wa kampuni ya African Wear & Design Jeniffer Alphayo ambaye alijinyakulia tuzo katika nyanja ya ushonaji aliwashukuru waandaji wa tuzo hizo kwa kuwa zinawapa hamasa katika kufanya kazi zao na zinatambua mchango wao katika jamii.


Awali mwandaaji wa tuzo hizo,Phide Mwakitalima alisema uhaba wa wadhamini ni changamoto kubwa wanayokumbana nayo na kuiomba serikali kuwaunganisha wanawake hususani wajasiriamali nchini.

Share To:

Post A Comment: