Na Mwandishi wetu ,Dodoma


Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt Tulia Ackson (Mb), amempongeza na kumshukuru Rais Samia kwa namna alivyoweza kutengeneza rekodi ya kipekee ya uongozi kwa mambo makubwa ya maendeleo aliyoyafanya kwa kipindi kifupi tangu aingie madarakani baada ya aliyekuwa Rais wa awamu ya tano, hayati Dkt.  John Pombe Magufuli kuaga dunia mwezi Machi, 2021.


Mhe. Spika ameyasema hayo wakati wa kufungua kongamano la tathmini ya mwaka mmoja ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan lililofanyika leo Machi 19, 2022 katika chuo kikuu cha Dodoma (UDOM)


"Hatumpongezi Rais Samia kwakuwa ni mwanamke bali ni kwa ujasiri na uwezo wake binafsi kwamaana kwa tathmini ni kwamba kazi anaiweza na amezidi viwango" amesema Dkt. Tulia 


Aidha amesisitiza kwamba, katika kipindi cha mwaka mmoja Rais Samia ameweza kuimarisha kwa kiasi kikubwa ujenzi wa miundombinu,  uwekezaji pamoja na kukuza demokrasia nchini.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Alliance for Democratic Change (ADC), Hamad Rashid, amesema kuwa imefika muda sasa wananchi wote wakiwemo wale wa vyama vya upinzani kuungana na Serikali katika kujengana na kuacha tabia za kuchochea migogoro isiyo na tija kwa Wananchi kwakuwa Rais Samia amejipambanua katika haki na usawa wa kila mtu.


Kongamano hilo limehudhuriwa na viongozi waandamizi wa Serikali, vyama vya siasa, viongozi wa dini, wasanii na vijana  kutoka maeneo tofauti nchini.


Mwisho.

Share To:

Post A Comment: