Balozi ya Uingereza nchini Tanzania Bwana David Concar amefanya ziara kwenye ofisi ya Klabu ya Waandishi wa Habari ya Mkoa wa Mwanza (MPC) na kufanya mazungumzo mafupi juu ya hali ya utendaji kazi wa vyombo vya habari nchini.


Balozi Concar aliwasili kwenye ofisi za MPC na kupokelewa na Mwenyekiti wa MPC bwana Edwin Soko na kisha kupewa kwa ufupi historia na majukumu ya MPC.

Pia balozi alifanya mkutano na waandishi wa habari na kuzungumzia masuala mbalimbali ikiwemo kuimarika kwa uhuru wa vyombo vya habari ndani ya mwaka mmoja.

"Ni vyema MPC kwenye mpango kazi wake ikaongeza jukumu la kuripoti habari zinazowahusu usawa wa kijinsia na haki za wanawake na watoto", alisema Balozi Concar.

Juu ya mzozo wa Ukraine balozi alieleza kuwa, nchi yake inajikita zaidi kwenye kutoa misaada ya kibinadamu na inaamini kuwa, uvamizi wa Russia Ukraine haukuwa wa haki na ndiyo maana mataifa mengi yanapaza sauti na kumtaka Rais Putin kusitisha vita hivyo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa MPC bwana Edwin Soko alimshukuru Balozi kwa ziara yake hiyo na kusisitiza kuwa bado kuna uhitaji wa serikali ya Uongereza kuwa na programu maalumu za kuwajengea uwezo wa waandishi wa habari wa Tanzania.

"Kwa mwaka mmoja wa utawala wa Rais Samia kumekuwa na uimarikaji wa uhuru wa vyombo vya habari", alisema Soko.

Hii ni ziara ya pili kubwa ya mabalozi kuitembelea MPC ikiwa ziara ya kwanza ilikuwa Mwezi Disemba 2021, ambapo Balozi wa Marekani Bwana Donald Wright aliitembelea MPC na kufanya mazungumzo na viongozi na pia mkutano na wanachama wa MPC.

Share To:

Post A Comment: