Naibu Waziri wa Kilimo Mh Anthony Mavunde amewahakikishia wakulima wote nchini kwamba serikali itaendelea kuwalinda na kuchukua hatua stahiki dhidi ya wafanyabiashara wa mazao ambao wanachukua mazao ya kulima na kushindwa kuwalipa na hivyo kurudisha nyuma jitihada za kuinua sekta ya kilimo nchini na kupunguza umaskini kwa wananchi.

Naibu Waziri Mavunde ameyasema hayo kwa nyakati tofauti jana akijibu malalamiko ya wakulima juu ya walanguzi wa mazao katika wilaya za Sumbawanga, Kalambo na Nkasi akiwa katika ziara ya siku 5 ya kukagua shughuli zilizotekelewa na Shirika la Mageuzi ya Kijani Afrika (AGRA ) ambapo ameongozana na Mjumbe wa Bodi ya AGRA AFRIKA na Rais Mstaafu Dr Jakaya M. Kikwete.

“Wakulima wanatumia nguvu,rasilimali na muda wao mwingi kufanya uzalishaji kwa malengo ya kujiinua kiuchumi na kupunguza umaskini.

Serikali kamwe haitaruhusu mtu yoyote kuwafanya wakulima kama mgongo wa kujiipatia mapato na kuwaacha wakulima wakitaabika kwa umaskini.

Tutahakikisha wanunuzi wa mazao ya wakulima wanawalipa kwa wakati wakulima kutokana na mauzo ya mazao yao,tutaendelea kuwabana na kuwashugulikia wale wote ambao wanaonesha ubabaishaji na kujaribu kufifisha jitihada za serikali katika kumuinua mkulima na kukuza sekta ya kilimo nchini.

Kile alichokifanya Waziri Bashe kwa wanunuzi wa Tumbaku waliochelewesha malipo ya wakulima ndio utakuwa muelekeo wetu kama wizara katika kuwalinda wakulima”Alisema Mavunde

Katika ziara ambayo pia yupo Makamu wa Rais wa AGRA Bi. Aggy Konde ,AGRA kwa kushirikiana na serikali imesaidia ujenzi wa maghala ya kuhifadhia mazao,kuwawezesha wazalishaji wa mbegu bora,kuwawezesha wachakataji wa mazao ya kilimo na kuwajengea uwezo wakulima kwa kuwalipa mafunzo juu ya kanuni za kilimo bora.


Share To:

Post A Comment: