Meneja wa TARURA Wilaya ya Kilindi Mhandisi Martin Mwashambwa, akisoma bajeti ya TARURA mbele ya Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi. (Picha na Yusuph Mussa).
Mkandarasi akiwa kwenye hatua za mwisho za kukamilisha barabara ya  Bokwa -Lengatei kipande cha lami chenye urefu wa mita 400. Barabara hiyo ni ya urefu wa kilomita 5.1 kutoka Kata ya Bokwa Wilaya ya Kilindi hadi Kata ya Lengatei, Wilaya ya Kiteto mkoani Manyara. Lakini kwa kuanzia wamejenga mita 400 katika Mji wa Songe yalipo Makao Makuu ya Wilaya ya Kilindi. (Picha na Yusuph Mussa).

Hiyo ni barabara inapita  kata ya Kilwa vijiji vya Tamota, Kilwa, Majengo,  na Kwadundwa. Pia inapita kata ya Lwande vijiji vya Lwande, Lulago na Kwamfyomi katika Wilaya ya Kilindi. Barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 33.7 ambayo imetengenezwa kwa kiwango cha changarawe na TARURA, ni muhimu kwa wakulima na wafanya biashata sababu huko wanalima ndizi,  Iriki, pilipili manga, magimbi , karafuu na mahindi, na kusafirishwa Handeni, Korogwe na mikoa ya Dar es  salaam, Kilimanjaro na Arusha. (Picha na Yusuph Mussa).

Mahindi na iliki kutoka Kata ya Kilwa na Lwande wilayani Kilindi. (Picha na Yusuph Mussa).


Na Yusuph Mussa, Kilindi




MADIWANI wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi mkoani Tanga kwa kauli moja wamepitisha bajeti ya Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) baada ya kuridhika na namna watakavyotengeneza barabara, kuweka makalavati na madaraja.

Ni baada ya TARURA Wilaya ya Kilindi kutengewa sh. bilioni 1,039,153,784 kwa mwaka wa fedha 2022/2023 kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya kawaida, sehemu korofi, muda maalumu na madaraja na kalavati.


Akisoma bajeti hiyo juzi Februari 2, 2022 kwenye kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo, Meneja wa TARURA Wilaya ya Kilindi Mhandisi Martin Mwashambwa alisema fedha za matengenezo ya barabara ya kawaida ni sh. milioni 91.4, ambazo zinatarajiwa kufanya matengenezo ya kilomita 17.80.


Mhandisi Mwashambwa alisema matengenezo ya barabara sehemu korofi  ni sh. milioni 342.6 jumla ya kilomita 3.98, matengenezo ya muda maalumu sh. 213,790,000 kilomita 29.70, madaraja mfuto 13 na makalavati mistari 15 zimetengwa sh. 290,720,000, na Usimamizi na Ufuatiliaji ni sh. 100,640,000.


"Pia sh. 1,381,000,000 (nje ya bajeti) ni za utekelezaji wa Mfuko wa Barabara miradi ya maendeleo, sh. milioni 500 ni utekelezaji wa barabara miradi ya maendeleo fedha za nyongeza (Jimbo), na sh. bilioni moja ni utekelezaji wa barabara miradi ya maendeleo fedha za tozo za mafuta" alisema Mwashambwa.


Fedha za Mfuko wa Barabara kwa matengenezo ya kawaida barabara za Mkusanyo, Muungano- Kilindi- Kimbe kilomita 17 sh. milioni 76.9, Darajani mita 500 sh. milioni 6.5, Kanisa la Pentecoste mita 300 sh. milioni nane (8), jumla ndogo  sh. milioni 91.4.

Matengenezo Barabara za Mjazo sehemu korofi, Stendi Kwamadoti mita 28 sh. milioni 241.5, Sambuche kilomita moja sh. milioni 22,  Sophia mita 500 sh. milioni 32, na Mtambo kilomita 2.2 sh. milioni 47.1, jumla ndogo sh. milioni 342.6.

Matengenezo ya muda maalumu Mafisa- Huyaga 6.2 sh. milioni 28, Muungano- Kimbe- Tamota- Vyadigwa kilomita 13 sh. milioni 70, Kibirashi- Gombero- Komhingo kilomita 10 sh. milioni 91.2, na Sekondari ya Mafisa mita 500 sh. milioni 24.5 jumla ndogo sh. 213,790,000.

Mwashambwa alisema katika ukarabati na ujenzi wa madaraja mfuto, Mafisa- Huyaga manane (8) sh. milioni 51, Muungano- Kimembe- Tamota- Vyadigwa sita sh. milioni 114, Kibirashi- Gombero- Komhingo manane (8) sh. milioni 107.72, na Shule ya Sekondari Mafisa Daraja Mfuto moja sh. milioni 18, jumla ndogo sh. 290,720,000.


Mhandisi Mwashambwa alisema kwa mwaka wa fedha 2021/2022, hadi kufikia Desemba 2021, wameweza kupokea sh. 250,174,888 kati ya sh. 1,039,153,784 zilizopangwa sawa na asilimia 24.07 kwa ajili ya matengenezo ya kazi za barabara kutoka Mfuko wa Barabara. Fedha za tozo wamepokea sh. 83,268,423 kati ya sh. bilioni moja zilizopangwa, hiyo ikiwa ni sawa na asilimia 8.32. Hakuna fedha ya Jimbo iliyopokelewa hadi Desemba 2021.


Mhandisi Mwashambwa amebainisha changamoto kadhaa za wilaya hiyo katika utekelezaji wa miradi. Na hiyo ni kulingana na jiografia ya wilaya hiyo ambapo barabara nyingi hupita kwenye milima na mabonde makubwa, hivyo zinahitaji matengenezo makubwa pamoja na ujenzi wa madaraja.


 "Moja ya ya changamoto ni uharibifu wa barabara unaosababishwa na mifugo, hii inatokana na Wilaya ya Kilindi kuwa na mifugo mingi, na upungufu wa vitendea kazi hasa magari, kwani mahitaji ni mawili, lakini lililopo sasa ni moja.


"Katika utatuzi wa changamoto, ni kuomba fedha kutoka vyanzo vingine vya fedha mbali na Mfuko wa Barabara ili kutatua changamoto ya baadhi ya barabara zinazohitaji matengenezo makubwa pamoja na ujenzi wa madaraja, kuendelea kuiomba wizara kupitia Mfuko wa Barabara kuongeza fedha za bajeti ya matengenezo ya barabara ili ziendane  na hali halisi ya barabara na urefu wa mtandao wake, kuwaelimisha wananchi kutunza barabara kwa kutopitisha mifugo, na kuomba kuongezewa magari na vitendea kazi" alisema Mwashambwa.



Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: