NA NAMNYAK KIVUYO, ARUSHA.


Bodi ya maji ya bonde la mto Pangani limekuta shughuli za kilimo cha mboga aina ya saladi ukifanyika katikati ya mito  pamoja utupaji wa chupa za maji na taka mbalimbali za majumbani zikiendelea kutupwa kwenye vyanzo vya maji jambo linaloadhiri utuzaji wa vyanzo vya maji.



Akizungumza na waandishi wa habari  afisa maendeleo ya jamii, bodi ya maji bonde la mto Pangani Jane Kaboga  alisema kuwa wapo katika ufuatiliaji wa mpango kazi uliotengenezwa na wadau katika mkutano uliofanyika August mwaka huu ambapo katika ufuatilia huo wamekuta shughuli za kilimo cha mboga aina ya saladi ukifanyika katikati ya mito pamoja utupaji wa takataka mbalimbali.


"Katika ufuatiliaji huu tumetembelea vyanzo mbalimbali ikiwemo chanzo cha mto Themi Kule katika kijiji cha Olgilai ambapo tumekuta kuna ulimaji wa saladi ndani yamito na utupaji wa taka katika mito na vijito vyake",Alisema Jane Kaboga.


Alieleza kuwa baada ya kuona changamoto  wamejaribu kuongea na wananchi wa maeneo hayo katika kuelimisha lakini pia wana mpango wa kuandaa mikutano katika ngazi za vitongoji na vijiji ili kuelimisha juu ya utunzaji wa rasilimali za maji.



Stela Mwanga mwanachi wa kata ya Moivo halmashauri ya Arusha Dc ambaye ni mnufaika wa mto Makiri unaotokea salema kata ya Olturoto  alisema kuwa vyanzo vya maji vinaharibiwa sana na wao kama akina mama ndio wahanga wakubwa kutokana na kuwa na matumizi makubwa  na maji hayo kwa kufanyia shughuli za majumbani hivyo watu waache kuchafua mito.


"Tusipovitunza vyanvyo hivi vizazi vijavyo havitanufaika navyo hivyo nashauri watu waache kutupa taka badalayake  watuvitunze kwa manufaa ya sasha na baadae," alisisitiza  Stella Mwanga.




Geoffrey Frank mkazi wa kata hiyo  alieleza kuwa ni vyema  wananchi waelimishwe kwani wakati wa mvua mafuriko yanapopita katika mto huo unakuwa na uchafu mwingi uliotupwa na binadamu ikiwemo vinyesi hali inayohatarisha afya za watu ambao hawana mbadala wa maji  mengine.




Kwa upande wake Mwenyekiti wa jumuiya ya watumiaji maji ya kidakio cha mto Themi Ismail Marunda alisema kuwa katika shughuli zao za usimamizi wa rasilimali za maji wamejaribu kuwaelimisha wananchi juu ya utunzaji wa vyanzo vya maji kwani kuna madhara pale watu wanapochafua maji pamoja na wanapolima pembezoni mwa mito.


"Madhara ni makubwa kwani watu wa Upande chini wanaweza wakawa wanayatumia maji haya hali inayopelekea kupata magonjwa lakini watu wakitunza mito hii wataoshi kwa amani na afya njema,"alisema.


Naye mwenyekiti wa foram za kijamii ukanda wa juu mto Themi Lazaro Mollel alifafanua watu wamejaza uchafu ndani ya mto ikiwemo makaratasi, chupa za maji na wengine kujisaidia ndani ya maji hivyo ofisi za kata  zichukue hatua kwa kuwaelimisha wananchi pamoja na Kuchukuliwa hatua za kisheria kwa wale watakao bainika kufanya uharibifu huo kwani kinachopelekea uharibifu huo kuendelea ni watu kupuuza elimu wanazopewa.


"Watu wanapuuza elimu wanazopewa hivyo hatua za kisheria zichukuliwe ikiwa ni pamoja kuendelea kutoa elimu " alisema.

Share To:

msumbanews

Post A Comment: